KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, March 29, 2012

Ndoa ya Omotola yatimiza miaka 16


LAGOS, Nigeria
MCHEZA filamu nyota wa Nigeria, Omotola Jalade wiki iliyopita alisherehekea ndoa yake kutimiza miaka 16 na mumewe kepteni Matthew Jalade Ekeinde.
Omotola na kepteni Matthew walifunga ndoa Machi 23, 1996 na sherehe yao ya harusi ilifanyika ndani ya ndege aina ya Dash 7 iliyosafiri kutoka Lagos kwenda Benin siku ya Aprili 21, 2001.
Wanandoa hao wamefanikiwa kupata watoto wanne, wawili wa kike na wawili wa kiume. Watoto hao ni Princess, M.J, Meriaih na Michael Ekeinde.
Ndoa ya Omotola na mumewe imekuwa ikikumbwa na misukosuko mingi ikiwa ni pamoja na tuhuma za kuachana ama kutembea nje, lakini wote wawili wamekuwa ngangali kukabiliana nayo.
Omotola na mumewe walisherehekea siku hiyo kwa staili ya aina yake, ikiwa ni pamoja na kuwaalika ndugu na marafiki wachache kwa ajili ya chakula na vinywaji.
Akihojiwa na mtandao wa naijerules, Omotola alisema anamshukuru Mungu kwa kumwezesha ndoa yake kudumu kwa miaka 16 hadi sasa.
“Kwangu mimi, tulipokutana kwa mara ya kwanza, haikuwa suala la mapenzi. Lakini kwake, alisema ilikuwa ni mapenzi zaidi,”alisema Omotola.
Omotola alisema kabla ya kufunga ndoa, mumewe alimweleza kuwa, alikuwa akiomba dua usiku na mchana aweze kukutana na mwanamke wa aina yake.
“Kwa mujibu wa maelekezo yake, aliwasilisha majina ya wasichana aliowahi kuhusiana nao kimapenzi kwa wachungaji ili waweze kuyasalia na kubaini yupi alikuwa sahihi kwake,”alisema.
Omotola alisema yeye na mumewe hawapendi kuwa na marafiki wanaoweza kuyaathiri maisha yao. Alisema hakuna kati yao anayependa kujadiliana jambo mbele ya marafiki.
Mwanadada huyo alisema pia kuwa, mumewe hapendi kusoma habari za udaku na hakuna mtu anayeweza kumwonyesha habari zozote zilizochapishwa kwenye gazeti kuhusu yeye.
“Wakati picha za filamu ya ‘The Prostitutes’ (Malaya) zilipochapishwa gazetini, ilikuwa kama vile hivyo ndivyo nilivyofanya kwenye filamu hiyo. Ilikuwa ni siku mbaya kwangu. Tulizungumza kuhusu hilo. Ilikuwa kama ananipoza kwa sababu nilichanganyikiwa. Tukio hilo halikutuathiri kitu,”alisema.
Omotola alisema kamwe hajawahi kuwa na uhusiano wa kimapenzi na mcheza filamu yeyote wa Nigeria. Alisema amekuwa akipokea maombi ya aina hiyo kutoka kwa watu mbalimbali, lakini amekuwa akiwapuuzia.
Alisema hapendi kuwa adui wa watu kwa sababu ameolewa. Alisema wanaume wote waliowahi kumtongoza kwa sasa wamebaki kuwa rafiki zake wa kawaida na wanamuheshimu.
“Mume wangu hana tatizo na kazi yangu na kamwe hawezi kuwa hivyo. Ananiunga mkono. Ni shabiki wangu namba moja. Anapenda kutazama filamu zangu,”alisema.

No comments:

Post a Comment