KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, March 29, 2012

Simba kutua Algeria Jumanne

KIKOSI cha wachezaji 20 na viongozi saba wa klabu ya Simba kinatarajiwa kuondoka nchini Jumatatu kwenda Algeria kwa ajili ya mechi ya marudiano ya michuano ya Kombe la Shirikisho dhidi ya ES Setif.
Ofisa Habari wa Simba, Ezekiel Kamwaga alisema mjini Dar es Salaam jana kuwa, timu hiyo itaondoka kwa ndege ya Shirika la Ndege la Egypt Air na kulala Misri siku moja.
Kamwaga alisema watalazimika kulala Misri kwa siku moja kwa ajili ya kubadili ndege itakayowapeleka Algeria. Alisema timu hiyo itaondoka Misri siku ya Jumanne.
Pambano hilo la marudiano kati ya Simba na ES Setif limepangwa kufanyika kati ya Aprili 6,7 na 8 katika mji wa Setif.
Kamwaga alisema wameamua kwenda Algeria mapema ili wachezaji waweze kuizoea hali ya hewa ya huko, ambayo kwa sasa ni baridi kali.
Simba inakwenda Algeria ikiwa kwenye mazingira mazuri ya kusonga mbele baada ya kuibuka na ushindi wa mabao 2-0 katika mechi ya awali iliyochezwa wiki iliyopita mjini Dar es Salaam.
"Timu itakwenda Algeria ikiwa na wachezaji 20 na viongozi saba, lakini tunaamini idadi inaweza kuwa kubwa zaidi kwa sababu wapo wanachama na mashabiki wengi waliojitokeza kutaka kwenda kutushangilia,”alisema.
Taarifa zilizopatikana wiki hii kutoka katika mji wa Setif zimeeleza kuwa, baridi ya huko kwa sasa ni nyuzijoto 13 hadi 15.
Kamwaga alisema kwa sasa, timu inaendelea na mazoezi kwa ajili ya mechi yao ya ligi kuu dhidi ya African Lyon, itakayochezwa keshokutwa kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Alisema wachezaji wote wapo katika hali nzuri, isipokuwa beki Juma Jabu, ambaye anaendelea kupatiwa matibabu baada ya kuumia mguu.
"Jabu anaendelea vizuri, lakini sina hakika kama ataweza kwenda Algeria. Kulingana na taarifa ya daktari wa timu, nadhani ataanza mazoezi Jumatatu,” alisema Kamwaga.
Simba imeweka kambi kwenye hoteli ya Mbamba Beach iliyopo Kigamboni, Dar es Salaam.

No comments:

Post a Comment