KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Saturday, March 10, 2012

Waziri Kabaka awafagilia waamuzi kombe la NSSF




TBC hoi kwa Jambo Leo, Habari Z’bar yatoa onyo



WAZIRI wa Kazi na Ajira, Gaudencia Kabaka amewamwagia sifa waamuzi wa soka wa kituo cha Twalipo Academy kwa kuonyesha umahiri mkubwa katika uchezeshaji wa mchezo huo.
Gaudencia alitoa pongezi hizo jana wakati akifungua michuano ya soka na netiboli ya kuwania kombe la Shirika la Taifa la Hifadhi ya Jamii (NSSF) kwenye viwanja vya klabu ya Sigara, Dar es Salaam.
Alisema uamuzi wa kituo cha Twalipo kuwapa mafunzo vijana hao ya kuchezesha soka tangu wakiwa mdogo, unastahili kupongezwa kwa vile wameanza kuandaliwa mapema kuwa waamuzi wa baadaye wa michuano mikubwa.
“Hawa vijana (waamuzi) peke yao ni burudani, ni vijana wadogo sana, lakini wanaifahamu vyema kazi yao, napongeza uamuzi wa kuwapa vijana hawa mafunzo ya uchezeshaji soka tangu wakiwa wadogo,”alisema.
Waziri Gaudencia alizitahadharisha timu shiriki katika michuano hiyo kuheshimu sheria za soka na kuepuka kutoa vitisho kwa waamuzi hao kwa sababu ya umri wao. Waamuzi hao kutoka Twalipo Academy wamekuwa wakitumika pia kuchezesha mechi za michuano ya Kombe la Uhai na Copa Cocacola.
Waziri huyo pia aliipongeza NSSF kwa kuendelea kuandaa michuano hiyo, ambayo hutoa fursa ya kuwakutanisha wafanyakazi wa vyombo vya habari nchini na pia kujenga afya zao kupitia michezo.
Viongozi wengine waliohudhuria ufunguzi wa mashindano hayo ni Naibu Waziri wa Kazi na Ajira, Makongoro Mahanga, Mkurugenzi Mkuu wa NSSF, Dk. Ramadhani Dau na maofisa mbalimbali wa shirika hilo.
Katika mechi za ufunguzi zilizochezwa jana, mabingwa watetezi Jambo Leo walianza vyema kuutetea ubingwa wao baada ya kuichapa TBC mabao 2-1.
Katika mechi za netiboli, IPP iliichapa Mwananchi mabao 16-12 wakati Habari Zanzibar iliinyuka bila huruma Global kwa kuitandika mabao 64-0.

No comments:

Post a Comment