KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Wednesday, March 14, 2012

INI EDO:Siogopi kupoteza uzuri kwa kuzaa



LAGOS, Nigeria
MCHEZA filamu wa kike anayeongoza kwa utajiri nchini Nigeria, Ini Edo amesema amepanga kuanza kuzaa hivi karibuni.
Ini amesema haogopi kuzaa kwa hofu kwamba atapoteza uzuri wa umbo lake na kuongeza kuwa, kwa mwanamke aliyeolewa, kuzaa ni jambo la lazima na kwamba anapenda kuwa na watoto
“Sihofuu kupoteza umbile langu kwa sababu ya kuzaa. Wakati utakapofika, nitaanza kuzaa. Napenda watoto. Siwezi kusubiri muda mrefu kupata watoto,”alisema mwanadada huyo mwenye umbo na sura yenye mvuto alipohojiwa na mtandao wa naijerules hivi karibuni.
Hata hivyo, Ini amesema kama ni uzuri, alikuwa nao alipokuwa kijana zaidi. Alisema aliziona baadhi ya picha zake alipokuwa mdogo na kuvutiwa nazo kiasi cha kumfanya aiamini kama ni yeye.
Ini alisema hana njia yoyote anayoifanya ili aonekane mrembo zaidi ya kufanyakazi zake kwa bidii, kula vizuri, kuiweka ngozi yake katika hali nzuri na kuwa mwenye furaha muda wote.
Mwanadada huyo alisema anamshukuru Mungu kwamba maisha yake ya ndoa yanakwenda vizuri na kuongeza kuwa, kwa sasa ameamua kuacha kuigiza nafasi, ambazo zinaweza kuitia doa ndoa yake.
Alisema kamwe hajawahi kuigiza filamu za ngono na hawezi kufanya kitu kama hicho katika maisha yake yote. Alisema anapenda zaidi kuigiza filamu zinazoelezea maisha halisi ya jamii kwa vile ndizo zinazokuwa na mvuto zaidi kwa jamii.
Alipoulizwa iwapo bado anaendelea kuvuta sigara, Ini alisema amekuwa akifanya hivyo katika baadhi ya filamu alizocheza, lakini kwa kawaida si mvutaji wa sigara.
Ini alisema skendo pekee iliyowahi kumchukiza katika maisha yake ni ile iliyoandikwa na baadhi ya vyombo vya habari, ikimuhusisha na uvutaji wa dawa za kulevya.
Mwanadada huyo mwenye macho ya mwito alikataa kutaja kiasi cha pesa, ambacho amekuwa akilipwa katika uigizaji wa filamu. Hata hivyo, alikiri kwamba amekuwa akilipwa fedha nyingi.
Ini alikiri kuwa si rahisi kumudu kuwa mke wa mtu na mwigizaji. Alisema anajitahidi kadri ya uwezo wake kumudu mambo hayo mawili na kwa kiasi fulani amefanikiwa.
“Nimekuwa nikipanga mapema ni lini niwe mahali fulani na lini nisiwe mahali hapo. Siweki vitu vingi kwenye sahani moja kwa wakati mmoja kwa sababu nikifanya hivyo, nitashindwa kufanya vitu vingine wakati ninapaswa kuvifanya. Bado nafanya kila kitu ambacho mwanamke anapaswa kukifanya. Kila ninapotoka kazini, nafanyakazi ya kupika nyumbani,”alisema.
Ini, ambaye ni msomi wa shahada ya sanaa alisema iwapo asingekuwa mwigizaji, angependa kuwa mwanasheria au mwanahabari.
Hata hivyo, Ini alisema upo uwezekano pia angeweza kufanyakazi nyingine yoyote ilimradi tu awe anaipenda.
“Mimi ni mtu makini katika kila jambo. Kila kitu ninachokiseti kukifanya katika akili yangu, kama ninakipenda, lazima nikifanye,”alisema.
Hivi karibuni, Ini alizindua filamu yake mpya ya I Will Take My Chances, ambayo Ini ameielezea kuwa, ana hakika itafanya vizuri sokoni na kupendwa na mashabiki.
Ini alisema ilimchukua miezi miwili kutengeneza filamu hiyo, mwezi mmoja kwa ajili ya mazoezi na mwezi mwingine kwa ajili ya kupiga picha za filamu hiyo.
Mwanadada huyo alisema licha ya kuolewa, hafikirii kustaafu kucheza filamu kwa sasa na kwamba hakuna kinachoweza kumfanya afikie uamuzi huo.
Alisema kwake, uigizaji wa filamu hautokani na kutafuta pesa, bali mapenzi kwa kazi hiyo.
Mumewe Ini kwa sasa anaishi nchini Marekani. Lakini mwanadada huyo amesisitiza kuwa, hilo si tatizo kwao kwa sababu wamekuwa wakikutana mara kwa mara.
Katika kujiweka safi kimwili, Ini amesema siku zote amekuwa akipenda kusafisha uso wake na kuuweka safi. Alisema anapokuwa hana kazi ama tukio lolote, hatumii vipodozi kutengeneza uso wake.

No comments:

Post a Comment