KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, March 22, 2012

Uhuru uso kwa uso na Jambo Leo

TIMU ya soka ya Uhuru leo inashuka dimbani kumenyana na Jambo Leo katika mechi ya robo fainali ya michuano ya Kombe la Shirika la Taifa la Hifadhi ya Jamii (NSSF) itakayochezwa kwenye uwanja wa klabu ya Sigara, Chang’ombe, Dar es Salaam.
Pambano hilo ni miongoni mwa mechi mbili za robo fainali ya michuano hiyo zitakazochezwa leo. Katika mechi nyingine, NSSF itamenyana na mojawapo kati ya Tumaini, Mwananchi na Changamoto kwenye uwanja wa DUCE.
Uhuru ilifuzu kucheza robo fainali baada ya kutwaa uongozi wa kundi A wakati NSSF ilitwaa uongozi wa kundi B. Jambo Leo imeshika nafasi ya kwanza ya ‘best-looser’ wakati Mwanahalisi na Tumaini Media zilikuwa zikiwania nafasi ya pili ya ‘best-looser’.
Timu zingine zilizofuzu kucheza robo fainali ya michuano hiyo kwa upande wa soka ni Business Times, Habari Zanzibar na TBC. Timu nyingine ilitarajiwa kupatikana jana baada ya pambano kati ya Mwananchi na Changamoto.
Kwa upande wa netiboli, timu zilizofuzu kucheza robo fainali ni NSSF na IPP kutoka kundi A, Habari Zanzibar na Business Times kutoka kundi B na TBC na Uhuru kutoka kundi C.
Washindi wengine wawili watakaocheza hatua hiyo kama ‘best-loosers’ walitarajiwa kupatikana jana baada ya mechi kati ya Uhuru na Tumaini Media na kati ya NSSF na Mwananchi.
Akizungumzia pambano la leo, nahodha wa Uhuru, Mussa Hassan alijigamba kuwa, vijana wake wamejiandaa vyema kukabiliana na wapinzani wao.
Katika michuano ya mwaka jana, Jambo Leo iliitoa Uhuru katika mechi ya nusu fainali kwa ushindi wa bao 1-0.
Mussa alisema watalitumia pambano hilo kulipa kisasi kwa Jambo Leo na pia kujisafishia njia ya kufuzu kucheza fainali.

No comments:

Post a Comment