KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, March 29, 2012

Ligi Kuu Zenji yapata mdhamini mpya


Na Mwandishi Wetu, Zanzibar
WIZARA ya Habari, Utamaduni, Utalii na Michezo ya Zanzibar imesema, kuanzia sasa italivalia njuga tatizo la kukosekana kwa udhamini katika michezo visiwani Zanzibar.
Waziri wa wizara hiyo, Abdilah Jihad Hassan alisema hayo mwishoni mwa wiki iliyopita mjini hapa wakati wa mkutano wa wadau wa michezo na Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Maalim Seif Sharrif Hamad.
Alisema ukosefu wa udhamini katika michezo, umechangia kwa kiasi kikubwa kudorola kwa michezo na pia kushusha ari ya wachezaji.
Waziri Jihad amesema tayari ameshafanikiwa kuishawishi kampuni moja ili idhamini michuano ya ligi kuu ya Zanzibar msimu ujao, lakini hakuwa tayari kuitaja.
Alisema amelazimika kujitosa mwenyewe kutafuta mdhamini wa ligi hiyo baada ya kushauriwa mara kadhaa na viongozi wa Chama cha Soka cha Zanzibar (ZFA).
Jihad alisema kujitokeza kwa malumbano ya mara kwa mara kati ya viongozi wa ZFA na wadau wa michezo ni ishara ya kutaka yawepo mabadiliko katika uendeshaji na usimamizi wa soka.
Hata hivyo, aliwataka wadau wanaokikosoa chama hicho, kutoa maoni yenye mtazamo chanya badala ya kujenga chuki dhidi ya viongozi wake.
Alisema tayari tofauti zilizokuwepo kati ya ZFA na Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) zimemalizwa na kwa sasa kumekuwepo na ushirikiano mkubwa kati ya vyama hivyo.
Kwa upande wake, Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Utalii na Michezo, Ali Mwinyikai alisema, michezo katika karne hii ni fedha, hivyo ili kuwashawishi wadhamini kubeba gharama, ni lazima wanaobebwa wawe wakweli na wawazi na kuepuka ubabaishaji. Mwinyikai Kampuni ya Simu za Mkononi ya Zantel iliamua kujitoa kudhamini ligi kuu ya Zanzibar kutokana na ubabaishaji wa viongozi wa ZFA na pia kutokuwa wazi kuhusu mapato ya matumizi ya pesa za udhamini.
Alikumbusha kuwa, ZFA ndicho chama pekee kinachopata pesa nyingi kutoka serikali kuliko vyama vingine, hivyo viongozi wake wanapaswa kuwa makini katika matumizi ya pesa hizo.
ZFA imekuwa ikipewa ruzuku ya sh. milioni tano kila mwaka huku serikali ikitenga sh. milioni 100 kwa ajili ya kuihudumia timu ya Zanzibar.

No comments:

Post a Comment