KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Wednesday, March 7, 2012

Osita: Sina papara ya kufunga ndoa




LAGOS, Nigeria
MCHEZA filamu machachari wa Nigeria, Osita Iheme amesema hana papara ya kufunga ndoa kwa sababu suala hilo linahitaji umakini mkubwa.
Osita, ambaye ni maarufu zaidi kwa jina la Ukwa ameueleza mtandao wa nigeriafilms wiki hii kuwa, kila kitu kinakwenda na wakati na kwamba muda wa kufunga ndoa utakapowadia, atafanya hivyo.
“Muda utakapofika, nitawapa taarifa na bila shaka mtapata mwaliko,”alisema mcheza filamu huyo mwenye umbo dogo.
Hivi karibuni, swahiba mkubwa wa mwigizaji huyo, Chinedu Ikedieze alifunga ndoa na Nneomwa kabla ya kwenda kutanua naye Arabuni na Marekani.
Osita ni mmoja wa wacheza filamu wanaoheshimika nchini Nigeria na hivi karibuni alitunukiwa tuzo ya hedhima ya MFR na Rais wa nchi hiyo, Jonathan Godluck.
Alisema anaona fahari kutunukiwa heshima hiyo na kuongeza kuwa, kamwe hawezi kuisahau siku aliyopata tuzo hiyo.
“Siku hiyo haitasahaulika maishani mwangu na naishukuru serikali kwa kutambua mchango wangu,”alisema.
Osita alisema tuzo hiyo imeonyesha jinsi serikali inavyofuatilia mchango wa wasanii wa fani hiyo katika kuleta maendeleo nchini humo kupitia filamu.
Mcheza filamu huyo mwenye mvuto kutokana na umbo na machachari yake, pia ameanzisha mradi maalumu kwa ajili ya kuendeleza utamaduni wa nchi hiyo katika shule za sekondari.

No comments:

Post a Comment