KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Wednesday, March 14, 2012

SINA HAMU NA LIGI KUU-NIYONZIMA

KIUNGO nyota wa klabu ya Yanga, Haruna Niyonzima amesema hana hamu na michuano ya soka ya ligi kuu ya Tanzania Bara kutokana na wachezaji wengi wa timu pinzani kupania kumuumiza.
Niyonzima amesema amebaini kuwa, baadhi ya wachezaji wa timu pinzani wamekuwa wakimchezea rafu kwa makusudi kwa lengo la kupunguza kasi yake.
Mwanasoka huyo wa kimataifa wa Rwanda alisema hayo mjini Dar es Salaam juzi kufuatia vurugu zilizotokea mwishoni mwa wiki iliyopita wakati Yanga ilipomenyana na Azam katika mechi ya ligi kuu iliyochezwa kwenye Uwanja wa Taifa.
Katika mechi hiyo, ambapo Yanga ilichapwa mabao 3-1, Niyonzima alitolewa nje kwa kadi nyekundu na mwamuzi Israel Nkongo wa Dar es Salaam kwa kosa la kucheza rafu na kutoa lugha chafu.
Kufuatia Niyonzima kuonyeshwa kadi hiyo, baadhi ya wachezaji wa Yanga walipinga na kuanza kumzonga Nkongo kabla ya kumshushia kipigo kizito.
Kitendo hicho kilisababisha Nkongo amtoe nje kwa kadi nyekundu beki Nadir Haroub Cannavaro kwa kosa la kumpiga. Wachezaji wengine waliotuhumiwa kumpiga mwamuzi huyo ni Stephano Mwasika na kiungo Nurdin Bakari.
Tayari kamati ya mashindano ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) imeshatangaza kuwafungia wachezaji watano wa Yanga pamoja na kuwatoza faini kwa kosa la kumshambuliaji Mkongo.
Wachezaji waliofungiwa ni Cannavaro, Nurdin, Omega Seme na Jerryson Tegete, ambao wamefungiwa kwa kipindi cha kati ya miezi mitatu hadi sita na wengine mechi tatu.
Stephano Mwasika amefungiwa mwaka mmoja na kutozwa faini ya sh. milioni moja kwa kumpiga. Adhabu zote zimetolewa kwa mujibu wa Kanuni za Ligi Kuu. Kamati ya ligi imempongeza nahodha wa Yanga, Shadrack Nsajigwa na mshambuliaji wa timu hiyo Hamis Kiiza kwa kuwa mstari wa mbele kuzuia wenzao kumshambulia mwamuzi. Pia imempongeza kocha Kostadin Papic wa Yanga kwa kukemea vurugu zilizofanywa na wachezaji wake.
Niyonzima amewataka wachezaji wa Yanga kukubaliana na uamuzi huo wa TFF na kuendelea kucheza kwa bidii katika mechi zilizosalia za mzunguko wa pili ili timu hiyo iweze kutetea taji lake.
Alikiri kuwa ligi ya msimu huu ni ngumu kutokana na kila timu kupania kushinda ili ziweze kutwaa ubingwa na zingine kuepuka kuteremka daraja.

No comments:

Post a Comment