KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, March 29, 2012

Nina uwezo wa kuimba aina zote za muziki-BI CHEKA

Ni Bi Kizee aliyejitosa kwenye bongo fleva
Anatamba kwa kibao chake cha Ni wewe

MSANII mkongwe wa muziki wa kizazi kipya nchini, Mwahija Cheka ‘Bi Cheka’ amesema ana uwezo wa kuimba aina zote za muziki, isipokuwa taarab.
Bi Cheka (55) amesema aliyebaini kipaji chake ni msanii Amani Temba wa kundi la TMK Wanaume Family, baada ya kukutana naye miaka mitatu iliyopita mjini Morogoro.
Mama huyo mwenye watoto na wajukuu kadhaa alisema hayo hivi karibuni alipokuwa akihojiwa katika kipindi cha Friday Night Live kilichorushwa hewani na kituo cha televisheni cha East Africa.
“Baada ya kukutana na Temba, nilikaa miaka mitatu bila kuwasiliana naye hadi nilipostukia naitwa Dar es Salaam kwa ajili ya kufanyiwa usaili,”alisema.
Bi Cheka alisema alifanyiwa usaili chini ya usimamizi wa kiongozi wa kundi la TMK Wanaume Family, Saidi Fela na siku hiyo hiyo alipelekwa studio kwa ajili ya kurekodi wimbo wake wa kwanza unaojulikana kwa jina la Ni wewe.
Bibi huyo amerekodi wimbo huo, unaozungumzia masuala ya mapenzi kwa kushirikiana na Temba.
“Nashukuru nilipokewa vizuri na ninapata ushirikiano mkubwa kutoka kwa wasanii wenzangu wa kituo cha kuendeleza vipaji cha Mkubwa na Wanawe,”alisema mama huyo.
“Kilichonipa moyo zaidi ni kuona kuwa mara baada ya kujaribiwa, wote walisema huyu bibi anajua kuimba, atatufaa, nikapewa nafasi, nikaonyesha vitu vyangu, ”aliongeza.
Bi Cheka alisema mara baada ya wimbo wake kuanza kuonekana kwenye luninga, baadhi ya wazee wenzake walionekana kumshangaa, lakini kwa sasa wameizoea hali hiyo.
“Kila nilipokuwa nikipita mitaani, walikuwa wakiitana na kuonyeshana yuleee, ndiye yeye, mara Tembaaa,”alisema mama huyo.
Pamoja na kuanza kupata umaarufu kimuziki, Bi Cheka alisema maisha yake hayajabadilika na kwamba ataendelea kubaki yule yule na kufanya yote aliyokuwa akiyafanya awali.
Bi Cheka alisema kwa sasa anajiandaa kutoa albamu, lakini haelewi ni lini itakamilika kwa vile hilo litategemea upatikanaji wa wadhamini kwa ajili ya kurekodi audio na video.
Akizungumzia ujio wa albamu ya bibi huyo, Fela alisema kwa sasa wanataka kumtambulisha kwanza kwa mashabiki ili nyimbo zake zijulikane.
Fela alisema wamepanga kumtambulisha Bi Cheka wakati wa sikukuu ya Pasaka katika onyesho litakalofanyika mkoani Morogoro. Alisema onyesho hilo litapambwa na wasanii mbalimbali nyota wa bongo fleva. Kiongozi huyo wa TMK Wanaume Family alisema maandalizi kwa ajili ya onyesho hilo litakalofanyika kwenye Uwanja wa Jamhuri mjini Morogoro, yamekamilika.
Alisema mbali na kibao chake cha Ni wewe, katika onyesho hilo, Bi Cheka atautambulisha wimbo wake mwingine mpya, lakini hakuwa tayari kutaja jina lake.
“Huu wimbo utapigwa kwa mara ya kwanza siku ya onyesho hilo, hatutaki kuutangaza hivi sasa kwa vile ni mapema kufanya hivyo. Tunataka kumtoa kiaina,”alisema.
Bi Cheka anavutiwa na wasanii wengi wa muziki wa kizazi kipya, lakini zaidi ni Diamond, Bob Junior, Ali Kiba na Dully Sykes. Kwa wasanii wa kike, alisema anavutiwa nao wote.

No comments:

Post a Comment