KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Sunday, March 25, 2012

Simba yawaua Waalgeria

Kikosi cha Simba kilichoiua ES Setif ya Algeria

Hivi ndivyo ubao wa matangazo ulivyokuwa ukisomeka baada ya mchezo kumalizika

Baadhi ya vigogo wa serikali na michezo waliohudhuria mechi hiyo. Kutoka kushoto ni Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Samuel Sitta, Waziri Mkuu mstaafu Fredrick Sumaye, mjumbe wa heshima wa Shirikisho la Soka Afrika (CAF), Said Hamad El-Maamry, Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe na Mwenyekiti wa Simba, Ismail Aden Rage.


Mshambuliaji Emmanuel Okwi (kulia) wa Simba akimtoka beki wa ES Setif ya Algeria


Makocha Milovan Cirkovic (kushoto) wa Simba akisalimiana na Alain Geiger wa ES Setif ya Algeria kabla ya timu hizo kumenyana jana.

Hekaheka kwenye lango la ES Setif ya Algeria katika pambano lao dhidi ya Simba


Machaku Salum wa Simba akimtoka beki wa ES Setif ya Algeria


SIMBA imeendelea kuwa kiboko ya timu za Waarabu, baada ya kuifunga timu ya Es Setif ya Algeria mabao 2-0 katika mechi ya raundi ya kwanza Kombe la Shirikisho iliyochezwa jana Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Mechi hiyo ilitawaliwa na kukosa mabao mengi kwa upande wa Simba, ambapo mshambuliaji Emmanuel Okwi, Felix Sunzu na Patrick Mafisango waliongoza mashuti yao kushindwa kulenga lango la wapinzani wao hao kutoka Afrika Kaskazini.
Dakika 43 Mafisango alishindwa kuunganisha wavuni pasi ndefu ya beki Kelvin Yondan aliyepanda kuongeza nguvu, ambapo mchezaji huyo alipiga shuti ambalo lilitoka nje, huku Okwi naye alirudia kosa hilo kwa kutoa nje mpira aliopewa pasi na Salum Machaku.
Timu hizo zilikwenda mapumziko zikiwa suluhu na wenyeji Simba walipata kona tatu wakiwa nyuma kwa kona moja dhidi ya Es Setif waliokuwa wanajihami muda mwingi wa mchezo.
Baada ya mashabiki wa Simba kuishia kushangilia 'gonga' za timu yao iliyokosa mabao mengi kipindi cha kwanza, raha yao ilikamilika dakika 72 baada ya Okwi kufunga bao la kwanza kwa shuti lililojaa wavuni kufuatia kuwababatiza mabeki wa Es Setif na kipa kuchanganywa na mwelekeo wa mpira huo.
Kuingia kwa bao hilo kuliongeza hamasa kwa Simba iliyokuwa na kila dalili ya ushindi kipindi cha pili kutokana na kulisakama lango la wapinzani wao kama nyuki.
Mchezo wa Es Setif kujihami hadi kipindi cha pili uliwafaidisha Simba ambao walicheza mpira nusu uwanja na kupata bao la pili dakika 79 lililowekwa wavuni na Haruna Moshi 'Boban' aliyewahi mpira uliopanguliwa na kipa Mohamed Benhamou, ambaye alitema mpira wa adhabu iliyopigwa vizuri na Machaku.
Adhabu hiyo ilitolewa na mwamuzi Hudu Munyemana kutoka Rwanda baada ya Okwi kuangushwa nje ya eneo la hatari na Machaku akapiga kiufundi na kumlazimu kipa huyo kupangua ndipo ulipomkuta Boban akauzamisha wavuni na kuibua shangwe kubwa kwa mashabiki wa klabu hiyo ya Msimbazi, huku upande wanaokaa mashabiki wa Yanga ukiwa kimya na baadhi yao kuondoka wakionyesha kutofurahi mahasimu wao kupata matokeo hayo.
Katika kipindi hicho, Es Setif walifanya mashambulizi machache likiwemo la dakika 49 Youcef Ghezzali kupiga shuti la mbali ambalo lilipaa katika lango la Simba na mchezaji huyo alikosa bao kipindi cha kwanza baada ya kupiga mpira uliodakwa na Juma Kaseja licha ya kubaki naye uso kwa uso.
Boban alijibu mapigo kwa kufumua kombora lililopanguliwa na kipa Benhamou na kuwa kona butu, naye Abderrahmane Hachoud alimjaribu Kaseja, lakini shuti lake lilitoka nje dakika 60. Pia, Sunzu alishindwa kuunganisha wavuni krosi ya Okwi aliyeongoza kwa kukosa mabao.
Wachezaji Racid Ferrahi, Akram Djanit wa Es Setif walionyeshwa kadi za njano na mwamuzi Munyemana kwa utovu wa nidhamu na wachezaji wa Simba hawakuonyeshwa kadi yoyote katika mechi hiyo ya raundi ya kwanza Kombe la Shirikisho. Simba iliyowahi kuweka historia ya kuzifunga timu za Arab Contractors na mabingwa Afrika mara tano klabu ya Zamalek, itakwenda Algeria kurudiana na Setif wiki mbili zijazo.
Simba: Juma Kaseja, Shomari Kapombe, Amir Maftah, Juma Nyoso, Kelvin Yondan, Patrick Mafisango/Gervas Kago, Salum Machaku, Mwinyi Kazimoto, Felix Sunzu /Jonas Kago, Haruna Moshi 'Boban' na Emmanuel Okwi.
Es Setif: Mohame Benhamou, Riadh Benchadi, Smain Diss, Farouk Belkaid/Akram Djanit, Mourad Delhoum, Mokhtar Benmoussa, Racid Ferrahi,Youcef Ghezzali, Youssef Sofiane/Mohamed Tiouli, Mokhtar Megueni na Abderrahmane Hachoud/Said Arroussi,

No comments:

Post a Comment