KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, March 29, 2012

SMZ yawashukia viongozi wa ZFA


Na Aboud Mahmoud, Zanzibar
MAKAMU wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Maalim Seif Sharrif Hamad amekiri kuwa, Chama cha Soka cha Zanzibar (ZFA) kinakabiliwa na matatizo makubwa na kinahitaji kusaidiwa ili kibadilike.
Maalim Seif alisema hayo mwishoni mwa wiki iliyopita baada ya kukutana na wadau wa michezo katika mkutano uliofanyika kwenye hoteli ya Bwawani mjini hapa.
Makamu wa Kwanza wa Rais alisema matatizo yanayokikabili chama hicho si ya mtu mmoja, bali Wazanzibar wanaoguswa na kudorola kwa maendeleo ya michezo.
Hata hivyo, Maalim Seif alisema tatizo kubwa linalokikabili chama hicho ni upungufu uliomo kwenye katiba yake, ambayo haikidhi matakwa ya Wazanzibar na pia kwenda na wakati.
Alilitaka Baraza la Michezo la Zanzibar (BMTZ) kufanyakazi bega kwa bega na ZFA ili kuyafanyiakazi mapungufu yaliyomo kwenye katiba ya chama hicho kwa lengo la kuifanya iende na wakati. Maalim Seif aliwataka viongozi wa chama hicho kuacha kujenga chuki na watu wanaowakosoa kwa vile lengo la watu hao ni kuona mchezo wa soka unapiga hatua mbele kimaendeleo badala ya kurudi nyuma.
"Eleweni kuwa, anayekukosoa anakupenda, lakini asiyekupenda atakupa sifa tu hata kama ukifanya mabaya," alisema Maalim Seif.
Aliahidi kuyafanyiakazi maoni mbalimbali yaliyotolewa na wadau wa michezo katika mkutano huo na kusisitiza kuwa, lengo la serikali ni kuona hadhi ya michezo visiwani humo inarejea.
Katika mkutano huo, wadau mbalimbali wa michezo waliwalalamikia viongozi wa ZFA kwa kutokuwa na fikra na mtazamo mpya katika kuendeleza soka, badala yake wametawaliwa na ubinafsi na kuweka mbele zaidi maslahi yao.
Wadau hao pia waliwalalamikia viongozi wa chama hicho kwa kushindwa kuisimamia na kuilinda katiba ya chama chao, badala yake wamekuwa wakiendesha soka shaghalabaghala.

No comments:

Post a Comment