KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Wednesday, March 14, 2012

Yanga: Tumeonewa



Yasema hawana imani na Kaburu, Ndumbaro

Yalipishwa mil 5/- za viti vilivyovunjwa U/Taifa
Na Mwandishi Wetu
UONGOZI wa klabu ya Yanga umesema haukubaliani na adhabu zilizotolewa na Kamati ya Ligi ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) kwa wachezaji watano wa timu hiyo.
Yanga imedai kuwa, adhabu hizo ni za kiuonevu na imewatupia lawama baadhi ya wajumbe wa kamati hiyo kwa madai kuwa ni wanachama wa Simba.
Akizungumza na Burudani mjini Dar es Salaam jana, Mwenyekiti wa Yanga, Lloyd Nchunga alisema uamuzi wa TFF kuwafungia wachezaji hao haukubaliki.
Nchunga alisema waliitarajia kamati hiyo kutoa uamuzi wa kionevu kwa Yanga kwa sababu baadhi ya wajumbe, Geofrey Nyange na Damas Ndumbaro ni wanachama wa Simba.
Nyange, ambaye ni maarufu zaidi kwa jina la Kaburu ni makamu mwenyekiti wa klabu ya Simba wakati Ndumbaro ni makamu mwenyekiti wa kamati ya uchaguzi ya wekundu hao wa Msimbazi. “Sasa hapo unategemea nini? Ni wazi kwamba kamati ya TFF inapokuwa na viongozi kutoka Simba, haiwezi kutenda haki kwa Yanga,”alisema.
Nchunga alisema anaamini wajumbe hao walitoa mapendekezo ya kuwafungia wachezaji hao watano wa Yanga kwa lengo la kupunguza kasi yake ya kutetea ubingwa wa ligi kuu msimu huu.
Kamati ya ligi ya TFF inaongozwa na Wallace Karia, Said Mohamed kutoka Azam, ambaye ni makamu mwenyekiti. Wajumbe wengine ni Ndumbaro, ambaye ni mwanasheria na Yahya Ahmed kutoka Kagera Sugar.
Wajumbe wengine wanaounda kamati hiyo ni Meja Charles Mbuge kutoka JKT Ruvu, Steven Mnguto kutoka Coastal Union, Kaburu kutoka Simba, Seif Ahmed wa Yanga, ACP Ahmed Msangi kutoka Polisi Dar na Henry Kabera wa Majimaji.
Yanga imeelezea msimamo wake huo siku moja baada ya kamati ya ligi ya TFF kuwafungia wachezaji wake watano na kuwatoza faini kwa kosa la kumpiga mwamuzi Israel Nkongo.
Tukio hilo lilitokea mwishoni mwa wiki iliyopita wakati Yanga ilipomenyana na Azam katika mechi ya ligi kuu kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam. Katika mechi hiyo, Yanga ilichapwa mabao 3-1.
Kamati hiyo imeitoza Yanga faini ya sh. 500,000 kutokana na mashabiki wake kufanya vurugu katika mechi namba 132 dhidi ya Azam na faini ya sh. 500,000 kufuatia wachezaji wake watatu kuonyeshwa kadi nyekundu katika mechi moja kwa kosa la kumpiga mwamuzi Nkongo.
Wachezaji wa Yanga waliokumbwa na adhabu hiyo ni Nadir Haroub ‘Cannavaro’, aliyefungiwa mechi sita za ligi na kutozwa faini ya sh. 500,000 na Jerryson Tegete, aliyefungiwa mechi sita na kutozwa faini ya sh. 500,000.
Wachezaji wengine ni Nurdin Bakari na Omega Seme waliofungiwa mechi tatu kila mmoja na kutozwa faini ya sh. 500,000 na Stephano Mwasika, aliyefungiwa mwaka mmoja na kutozwa faini ya sh. milioni moja.
Katika hatua nyingine, TFF imesema Yanga itapaswa kulipa sh. milioni tano kwa ajili ya kufidia gharama za kutengeneza viti 119 vilivyoharibiwa wakati wa mechi yake ya ligi dhidi ya Azam.
Ofisa Habari wa TFF, Boniface Wambura alisema mjini Dar es Salaam jana kuwa, wamepokea barua kutoka Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo kuhusu uharibifu huo kutokana na vurugu za mashabiki wa Yanga.
Wambura alisema kwa mujibu wa tathmini ya serikali, katika vurugu hizo, jumla ya viti 119 viliharibiwa na gharama za kuvitengeneza upya ni sh. milioni tano, ambazo serikali imeagiza zilipwe mara moja. “Kwa vile mashabiki wa Yanga ndiyo waliohusika na vurugu na uharibifu huo, gharama hizo zitabebwa na klabu hiyo ili serikali iweze kufanya ukarabati haraka,”alisema Wambura.

No comments:

Post a Comment