KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, March 8, 2012

Bingwa Kombe la NSSF kuzoa mil 3.5/-



MENEJA Kiongozi Idara ya Uhusiano na Huduma za Wateja wa Shirika la Taifa la Hifadhi ya Jamii (NSSF), Eunice Chiume (kulia) akikabidhi jezi kwa mwakilishi wa timu ya soka ya Uhuru, Gule Mandago (kushoto) katika halfa iliyofanyika jana kwenye hoteli ya JB Belmont, Dar es Salaam. Wa pili kulia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Mashindano ya Kombe la NSSF, Rashid Zahor na wa pili kushoto ni mratibu wa mashindano hayo kutoka NSSF, Juma Kintu. (Picha na Emmanuel Ndege).
BINGWA wa mwaka huu wa michuano ya soka ya kombe la Shirika la Taifa la Hifadhi ya Jamii (NSSF) atazawadiwa kitita cha sh. milioni 3.5 wakati bingwa wa netiboli atazawadiwa sh. milioni tatu.
Zawadi hizo zilitangazwa jana na Meneja Uhusiano wa NSSF, Eunice Chiume alipozungumza na waandishi wa habari kwenye hoteli ya JB Belmont mjini Dar es Salaam.
Eunice alisema mshindi wa pili wa mashindano hayo katika soka atazawadiwa sh. milioni tatu wakati mshindi wa tatu atazawadiwa sh. milioni 2.5.
Kwa mujibu wa Eunice, mshindi wa pili katika netiboli atazawadiwa sh. milioni mbili na wa tatu atazawadiwa sh. milioni moja.
Mbali na zawadi hizo, Eunice alisema kutakuwepo na zawadi maalumu ya sh. 300,000 kwa mwanasoka bora na mcheza netiboli bora.
Eunice alisema mashindano hayo yamepangwa kuanza kesho asubuhi kwenye viwanja vya klabu ya Sigara, Chang’ombe, Dar es Salaam na mgeni rasmi anatarajiwa kuwa Waziri wa Kazi na Ajira, Gaudencia Kabaka.
Katika mechi ya ufunguzi ya soka, mabingwa watetezi Jambo Leo watamenyana na TBC wakati katika netiboli, IPP itamenyana na Mwananchi.
Eunice alisema NSSF imepanga kutumia sh. milioni 150 kwa ajili ya kuandaa mashindano ya mwaka huu na fedha hizo zitatumika kwa zawadi za washindi, vifaa vya michezo, malipo ya viwanja, waamuzi na ulinzi.
Meneja Uhusiano huyo wa NSSF pia alikabidhi vifaa vya michezo kwa timu zote 18 zitakazoshiriki katika soka na timu 12 zitakazoshiriki kwenye netiboli.
Vifaa hivyo ni seti 20 za jezi, pea 20 za soksi, jozi 20 za viatu, shineguards 20 na mipira miwili kwa timu za soka na jezi 12, viatu 12, soksi pea 12, mipira miwili na beaps saba kwa timu za netiboli. Alisema lengo la NSSF kuandaa mashindano hayo ni kuwapa fursa wafanyakazi wa vyombo vya habari kufahamiana na pia kuimarisha afya zao kwa njia ya michezo.
Alizitaka timu shiriki kukubaliana na matokeo wakati wa mashindano hayo na kuepuka kutoa visingizio vya timu pinzani kuchezesha mamluki baada ya kutolewa.
Eunice alisema iwapo timu itakuwa na malalamiko kuhusu jambo lolote, inapaswa kuyawasilisha kwa kamati inayosimamia mashindano hayo badala ya kuiandika vibaya NSSF kupitia kwenye vyombo vyao vya habari.
Alisema katika mashindano hayo, timu za NSSF zitashiriki kama wenyeji, lakini hazitachukua pesa za zawadi iwapo zitashika nafasi tatu za kwanza.
Naye mratibu wa mashindano hayo, Juma Kintu alisema mwaka huu, wameamua kuwatumia waamuzi wa kituo cha Twalipo, ambao wamekuwa wakitumika kuchezesha mechi za kombe la Uhai na Copa Cocacola.

No comments:

Post a Comment