KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, March 29, 2012

COS B:Ali Kiba amerekodi wimbo wangu

MSANII chipukizi wa muziki wa kizazi kipya, Marius Rashid ameibuka na kudai kuwa, wimbo wake wa Single Boy umeibwa na msanii nyota wa muziki huo, Ali Kiba.
Akizungumza mjini Dar es Salaam wiki hii, msanii huyo ambaye ni maarufu zaidi kwa jina la Cos B alisema, aliutunga wimbo huo miezi mitano iliyopita.
Cos B alisema hakuwahi kuurekodi wimbo huo kwenye studio yoyote zaidi ya kumpatia Kiba kwa lengo la kumsaidia kuurekodi.
“Wakati nikihangaika kutafuta mfadhili ili anisaidie kuurekodi wimbo huo, nikakutana na Ali Kiba kwenye studio za G Records,”alisema Cos B.
“Baada ya kukutana naye, nilimuomba anisaidie nipate nafasi ya kurekodi kwenye studio hiyo, akaniomba nimwimbie kwanza wimbo wangu niliotaka kuurekodi,”aliongeza msanii huyo.
Cos B alisema baada ya kuuimba wimbo huo kwa mara ya kwanza, Kiba alitokea kuvutiwa nao na akamuomba auimbe kwa mara ya pili ili ausikilize tena.
“Wakati nikifanya hivyo, sikujua kwamba alikuwa akiurekodi wimbo huo maana alikuwa ameshika simu yake ya mkononi na kuibonyezabonyeza,”alisema.
Chipukizi huyo wa muziki wa kizazi kipya alisema, baada ya hapo Kiba alimpatia namba yake ya simu ili wawe wakiwasiliana, lakini kila alipokuwa akimpigia, hakuweza kumpata.
Alisema siku moja alipokuwa safarini kwenda nyumbani kwao Mpanda mkoani Rukwa, alishangaa kuusikia wimbo huo ukipigwa redioni ukiwa umeimbwa na Kiba.
“Kwa kweli nilishtuka na kushangaa sana kwa sababu haukuwa umebadilishwa sana mashairi yake. Ni yale yale ya kwangu na jina la wimbo ni lile lile la single boy,”alisema.
Cos B alisema kitendo cha Kiba kuurekodi wimbo wake bila ridhaa yake kimemshangaza kwa vile hawakuwa na makubaliano yoyote ya aina hiyo.
Amewataka mashabiki wa muziki wa kizazi kipya nchini kuuchukulia wimbo huo kuwa ni mali yake na kwamba Kiba alitumia hila kuuiba wakati alipomuomba amuimbie walipokutana kwenye studio za G Records.
Alipoulizwa kwa njia ya simu iwapo tuhuma hizo ni za kweli, Kiba aliomba kwanza apewe Cos B ili azungumze naye kabla ya kujibu swali hilo.
Alipobanwa zaidi na kuelezwa mazingira ya kuupata kwake wimbo huo kutoka kwa Cos B, Kiba alikana kumjua msanii huyo na kudai kuwa, hajawahi kuiba wimbo wake.
‘Huu wimbo ni wa kwangu na ingekuwa vizuri iwapo ningekutana na msanii huyo ili anieleze ni lini nilimwibia wimbo wake,’ alisema Kiba akionekana kuwa na hasira.

No comments:

Post a Comment