KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Wednesday, October 26, 2011

Mussa Kijoti afunika uzinduzi wa Five Stars

Mussa Kijoti

Mariam Mohamed

Mwamvita Shaibu


MWIMBAJI anayechipukia kwa kasi katika muziki wa taarab nchini, Mussa Ally 'Kijoti' ametamba kuwa, atahakikisha analiziba vyema pengo lililoachwa na marehemu kaka yake, Issa Kijoti.
Mussa alisema hayo mwishoni mwa wiki iliyopita wakati wa uzinduzi wa kundi la Five Stars Modern Taarab 'Watoto wa Bongo' uliofanyika kwenye ukumbi wa Travertine, Magomeni, Dar es Salaam.
Issa, ambaye alijizolea sifa kemkem kutokana na uimbaji wake wa kuvutia, alifariki dunia Machi 13 pamoja na wasanii wengine 13 wa kundi hilo katika ajali ya gari iliyotokea katika eneo la Mikumi mkoani Morogoro.
Wasanii hao walifariki dunia baada ya basi dogo aina ya Toyota Coaster walilokuwa wakisafiria kutoka Mbeya kwenda Dar es Salaam, kulivaa lori lililokuwa limeegeshwa pembeni ya barabara na baadaye kupinduka.
Mussa, ambaye kwa sasa anaimba nyimbo zote zilizokuwa zikiimbwa na marehemu kaka yake, ameanza kugusa hisia za mashabiki wengi kutokana na uimbaji wake kushabihiana na marehemu kaka yake.
Mwimbaji huyo alionyesha cheche zake na kuwaacha hoi mashabiki baada ya kuimba kwa ukamilifu wimbo wa 'Wapambe msitujadili', uliompatia umaarufu mkubwa kaka yake.
Mussa alipanda jukwaani kwa mara ya kwanza katika uzinduzi wa albamu mpya ya ‘Mwenye hila habebeki’, uliokwenda sambamba na uzinduzi wa kundi hilo. Uzinduzi huo ulihudhuriwa na umati mkubwa wa mashabiki.
Akiwa amevaa suruali nyeupe, shati jeusi, koti jeupe na viatu vyeusi, Mussa alionekana lulu kutokana na uwezo mkubwa wa uimbaji aliouonyesha.
Kupanda jukwaani kwa mwimbaji huyo chipukizi kuliufanya ukumbi ulipuke mayowe ya kumshangilia huku baadhi ya mashabiki wakijimwaga stejini kucheza.
Akizungumza na Burudani wakati wa onyesho hilo, Mussa alisema lengo lake ni kuwa mwimbaji maarufu ndani na nje ya nchi na kusisitiza kuwa, hilo linawezekana.
Alisema akiwa katika kundi hilo, atahakikisha anakitumia kipaji chake ili kufikia malengo aliyojiwekea, ambayo ni kuwa mwimbaji nyota katika tasnia ya muziki wa taarab.
"Nitahakikisha ninatumia kipaji nilichojaaliwa na Mungu kufikia malengo yangu. Ninawaomba wapenzi na mashabiki wangu wazidi kuniunga mkono," alisema.
Mwimbaji huyo mwenye umri wa miaka 19, aliyemaliza darasa la saba mwaka 2008 alisema, anaushukuru uongozi wa kundi hilo kwa kumpa ushirikiano mzuri na ameahidi kufanya mambo makubwa zaidi.
Mbali na Mussa, wasanii wengine waliong’ara wakati wa onyesho hilo ni mpiga gita maarufu, ambaye alijiunga na kundi hilo hivi karibuni, Shaban Mafloo, aliyeonekana kugusa hisia za mashabiki wengi kutokana na kulikung'uta kwa umahiri mkubwa.
Kutokana na umahiri wake huo, baadhi ya mashabiki walishindwa kujizuia na kuanza kumzunguka huku wakimshangilia na kumtunza pesa.
Waimbaji wengine waliotia ni Zena Mohammed, aliyeimba kibao cha ‘Watu na tabia zao’ kilichowafanya mashabiki kuviacha viti vyao kwa muda na kujitosa jukwaani kucheza.
Naye Mariam Mohamed, mshindi wa shindano la BSS mwaka jana, aliwateka mashabiki kwa kibao chake cha ‘Mwenye hila habebeki’ wakati Saidi Yussuf aling’ara kwa kibao chake cha ‘One mistake, one goal’ akishirikiana na Mwamvita Shaibu.
Mpiga kinanda wa kundi hilo, Ally J kama ilivyo kawaida yake, alifanikiwa kuwateka mashabiki kutokana na kuipapasa ala hiyo kwa ufundi wa hali ya juu.
Uzinduzi wa kundi hilo ulipambwa na bendi ya muziki wa dansi ya Mapacha Watutu, inayoundwa na wanamuziki Jose Mara, Khalid Chokoraa na Kalala Junior.

No comments:

Post a Comment