KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, October 20, 2011

Wachezaji Yanga wapigwa mkwara



UONGOZI wa klabu ya Yanga umewapiga marufuku wachezaji wake kutoka nje ya kambi ya timu hiyo bila idhini ya uongozi.
Agizo hilo limekuja baada ya baadhi ya wachezaji wa timu hiyo kukutwa wakitanua katika maonyesho ya muziki wa dansi ya bendi za FM Academia na Twanga Pepeta International yaliyofanyika mwishoni mwa wiki iliyopita.
Habari za kuaminika kutoka ndani ya Yanga zimeeleza kuwa, wachezaji hao walikutwa wakitanua kwenye kumbi za klabu ya TCC, Chang’ombe na Msasani Beach huku baadhi yao wakiwa wamelewa chakari.
Kutokana na kukutwa katika maeneo hayo, baadhi ya wanachama waliamua kuwasilisha majina ya wachezaji hao kwa uongozi na Kocha Sam Timbe ili waweze kuchukuliwa hatua.
Kwa mujibu wa habari hizo, timu hiyo sasa imeingia rasmi kambini juzi makao makuu ya klabu hiyo mitaa ya Twiga na Jangwani, Dar es Salaam.
“Ni kutokana na matukio hayo, uongozi sasa umeamua timu iingie kambini mara moja na kuwapiga marufuku wachezaji kutoka nje ya kambi bila ruhusa ya uongozi,” kimesema chanzo cha habari.
Wakati huo huo, mabingwa hao watetezi wa ligi kuu ya Tanzania Bara, leo wanatarajiwa kushuka dimbani kumenyana na Toto African katika mechi itakayopigwa kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Pambano hilo linatarajiwa kuwa kali na la kusisimua kwa vile kila timu itapania kushinda ili kutoka uwanjani na pointi zote tatu.
Yanga inashika nafasi ya nne katika msimamo wa ligi hiyo, ikiwa na pointi 15 baada ya kucheza mechi tisa wakati Toto African ni ya tisa ikiwa na pointi 10 kutokana na idadi hiyo ya mechi.
Kocha Mkuu wa Yanga, Sam Timbe alisema juzi kuwa, wanaipa mechi hiyo umuhimu mkubwa kwa vile wamepania kushinda mechi zao zote zilizosalia za mzunguko wa kwanza wa ligi hiyo.
“Kwa kweli sitaki kuona tunapoteza mechi yoyote ya mzunguko wa kwanza, na tutaanzia kwa Toto African,”alisema kocha huyo raia wa Uganda. Kwa upande wake, Kocha John Tegete wa Toto African amejigamba kuwa, kikosi chake kimejiandaa vyema kwa ajili ya kukabiliana na Yanga.
Tegete aliwaonya mashabiki wa Yanga kuwa, wasitarajie kupata mteremko katika mechi hiyo kwa vile wana uhakika mkubwa wa kufanya vizuri.

No comments:

Post a Comment