KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, October 27, 2011

Seagull kudhamini ligi kuu Z'bar kwa mil. 41/-


KAMPUNI ya boti ya Seagull imejitokeza kudhamini michuano ya soka ya ligi kuu ya Zanzibar.
Meneja Masoko wa kampuni hiyo, Rehema Yusuf aliwaambia waandishi wa habari mjini hapa jana kuwa, Seagull itadhamini ligi hiyo kwa sh. milioni 41.5.
Rehema alisema, udhamini huo utakuwa ni wa msimu mmoja wa ligi, ambayo inatarajiwa kuanza Novemba Mosi mwaka huu.
Hata hivyo, Rehema alisema wanatarajia kuendelea kuidhamini ligi hiyo kwa kutegemea ushirikiano mzuri utakaojitokeza na Wazanzibari katika kuiunga mkono boti hiyo.
Kwa mujibu wa Rehema, katika udhamini huo, watagharamia usafiri wa ndani, vifaa vya michezo kwa timu shiriki na zawadi za bingwa na mshindi wa pili.
Alisema wameamua kudhamini ligi hiyo kutokana na kujali mchango mkubwa wanaoutoa Wazanzibari katika kuitumia boti hiyo.
Rehema alisema katika udhamini huo, sh. milioni 15 zitatumika kama zawadi kwa bingwa na mshindi wa pili. Alisema bingwa atapata sh. milioni 10 na mshindi wa pili sh. milioni tano.
Alisema sh. milioni saba zitatumika kwa ajili ya vifaa vya michezo wakati sh. milioni 18 zitatumika kwa ajili ya usafiri wa timu kwenda vituoni.
Akizungumza katika hafla hiyo, Katibu Msaidizi wa Chama Cha Soka Zanzibar (ZFA), Masoud Attai alisema kuwa ligi hiyo itaanza kwa mechi ya ufunguzi kati ya Jamhuri na Super Falcon. Alisema mchezo huo utachezwa Uwanja wa Gombani uliopo Pemba.
Attai alisema ligi hiyo itazishirikisha timu 12, tatu kutoka Pemba na tisa kutoka Unguja. Alisema ligi hiyo itazinduliwa na Waziri wa Habari, Utamaduni, Utalii na Michezo, Abdilahi Jihadi Hassan.

No comments:

Post a Comment