KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, October 20, 2011

Simba yazidi kupaa

Emmanuel Okwi

Haruna Moshi 'Boban'


SIMBA jana iliendelea kupaa katika michuano ya soka ya ligi kuu ya Tanzania Bara, baada ya kuicharaza Ruvu Shooting mabao 2-0 katika mechi iliyochezwa kwenye uwanja wa Chamazi, Dar es Salaam.
Ushindi huo ulikuwa wa saba kwa Simba katika ligi hiyo na uliiwezesha kuwa na pointi 24 baada ya kucheza mechi 10. Ruvu Shooting ni ya nane ikiwa na pointi 11 baada ya kucheza idadi hiyo ya mechi.
Pambano hilo lilianza kwa kasi huku wachezaji wa Simba wakigongeana pasi fupi fupi wakati Ruvu Shooting walitumia pasi ndefu na kucheza kwa kutumia nguvu zaidi.
Simba ilikuwa ya kwanza kubisha hodi kwenye lango la Ruvu Shooting dakika ya 26 wakati kipa Benjamin Haule wa Ruvu Shooting alipoutema mpira na kumkuta Uhuru Selemani, lakini shuti lake liligonga mwamba wa goli na mpira kuokolewa.
Timu hizo ziliendelea kushambuliana kwa zamu katika kipindi cha kwanza, lakini umaliziaji mbovu wa washambuliaji wake ulikuwa kikwazo kupata mabao. Timu hizo zilikwenda mapumziko zikiwa suluhu. Simba ilikianza kipindi cha pili kwa kumpumzisha Uhuru Selemani na kumwingiza Haruna Moshi, ambaye aliongeza uhai kwenye safu ya ushambuliaji ya timu hiyo.
Bao la kwanza la Simba lilifungwa na Emmanuel Okwi dakika ya 47, kufuatia gonga safi kati yake na Haruna Moshi ‘Boban’. Kipa Benjamin Haule wa Ruvu Shooting alishindwa kuokoa shuti hilo.
Boban aliiongezea Simba bao la pili dakika ya 53 baada ya kugongeana vizuri na Okwi. Kabla ya kufunga bao hilo zuri na la aina yake, Okwi alimchungulia kipa Haule na kuukwamisha mpira wavuni.
Simba sasa imesaliwa na mechi tatu dhidi ya JKT Ruvu, Yanga na Moro United kabla ya kukamilisha mechi za mzunguko wa kwanza.
Ligi hiyo inatarajiwa kuendelea leo wakati mabingwa watetezi Yanga watakapomenyana na Toto African kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam na kesho Azam itavaana na Polisi Dodoma kwenye uwanja wa Chamazi.
Simba: Juma Kaseja, Saidi Cholo, Juma Jabu, Juma Nyoso, Obadia Mungusa, Patrick Mafisango/Shomari Kapombe, Jerry Santo, Ulimboka Mwakingwe, Emmanuel Okwi, Felix Sunzu, Uhuru Selemani/Haruna Moshi.
Ruvu Shooting: Benjamin Haule, Michael Pius, Paul Ngalema, George Michael, Shabani Zuzan, Iddi Nyambiso, Ayoub Kitala, Hassan Dilunga, Abdalla Juma/Abdalla Abdulrahman, Kassim Linde, Raphael Keyala.

No comments:

Post a Comment