KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, October 27, 2011

SIMBA, YANGA NGOMA INOGILE

Kikosi cha Yanga

Kikosi cha Simba


Okwi, Boban, Sunzu wapania kupeleka kilio Jangwani

Tegete, Asamoah, Gumbo kukata ngebe za mnyama?

Papic, Basena watamba kuwapa raha mashabiki wao


MIAMBA ya soka nchini, Simba na Yanga inakutana kwa mara ya kwanza msimu huu keshokutwa Jumamosi katika mechi ya ligi kuu ya Tanzania Bara itakayopigwa kwenye Uwanja wa Taifa. Dar es Salaam.
Hii ni mara ya tatu kwa Simba na Yanga kukutana katika kipindi cha miezi minne iliyopita. Zilipokutana Julai 10 mwaka huu katika mechi ya fainali ya Kombe la Kagame, iliyochezwa kwenye uwanja huo, Simba ilipigwa mweleka wa bao 1-0.
Yanga ilipata bao hilo la pekee na la ushindi kupitia kwa mshambuliaji wake wa kimataifa kutoka Ghana, Kenneth Asamoah dakika ya 108. Mshindi ilibidi apatikane dakika za nyongeza baada ya timu hizo kumaliza dakika 90 zikiwa suluhu.
Asamoah alifunga bao hilo kwa kichwa, akiunganisha mpira wa krosi uliochongwa na kiungo wa zamani wa wapinzani wao hao, Rashid Gumbo aliyeingia kipindi cha pili kuchukua nafasi ya Godfrey Taita aliyeumia.
Gumbo aliambaa na mpira wingi ya kushoto na kuwatoka mlinzi Nassor Said ‘Chollo’ na kumimina krosi ambayo ingeweza kuokolewa na mlinzi Kelvin Yondani, lakini katika harakati za kufanya hivyo, aliteleza na kuanguka na mpira kumkuta mfungaji, aliyekuwa nyuma yake na kugonga kichwa ambacho kilijaa wavuni na kumwacha kipa Juma Kaseja akiwa hana la kufanya.
Watani hao wa jadi wa soka nchini walikutana tena Agosti 12 mwaka huu katika mechi ya kuwania Ngao ya Hisani, maalumu kwa ajili ya ufunguzi wa ligi. Katika mechi hiyo, iliyopigwa tena kwenye uwanja huo, Simba ililipa kisasi baada ya kuichapa Yanga mabao 2-0.
Mabao yote mawili ya Simba yalipachikwa wavuni katika kipindi cha kwanza. Bao la kwanza lilifungwa dakika ya 16 na Haruna Moshi 'Boban' wakati la pili liliwekwa kimiani dakika ya 37 kwa njia ya penalti na Mzambia, Felix Sunzu.
Je, ni Simba au Yanga itakayotoka uwanjani na ushindi keshokutwa kwa kuchukua pointi zote tatu na kuwapa raha mashabiki wake?
Swali hilo ndilo linaloelekea kuviumiza vichwa vya mashabiki wa soka nchini, ambao mojawapo kati ya timu hizo ikifungwa, hutawaliwa na simanzi zito huku wale walioshinda wakisherehekea ushindi kwa mbwembwe za aina zote.
Tayari presha imeshaanza kuwa juu kwa viongozi, wanachama na mashabiki wa klabu hizo huku kukiwa na taarifa kwamba, Yanga ilipanga kwenda kuweka kambi nchini Msumbiji kwa ajili ya kujiandaa na pambano hilo, lakini baadaye ilifuta mpango huo na kuamua kwenda kuweka makazi Mwanza.
Kwa mujibu wa taarifa hizo, kambi hiyo ya Yanga imegharamiwa na mfadhili wao, Yussuf Manji, ambaye amekubali kurejea kuifadhili timu hiyo baada ya kuombwa kufanya hivyo na uongozi, chini ya Mwenyekiti, Lloyd Nchunga.
PAPIC AREJESHWA
Pia kuna habari kuwa, Yanga itacheza mechi hiyo ikiwa chini ya kocha wake wa zamani, Kostadin Papic, ambaye ameingia mkataba wa miaka miwili wa kuinoa timu hiyo baada ya Sam Timbe kutoka Uganda kumaliza mkataba wake.
Hata hivyo, uamuzi wa Yanga kumrejesha Papic umeonekana kuwakera wachezaji wa timu hiyo kwa madai kuwa, kocha huyo alikuwa akiwagawa wachezaji wake na pia alikula pesa za usajili za baadhi ya wachezaji.
Papic, ambaye ni raia wa Serbia, alijiunga na Yanga kwa mara ya kwanza Oktoba mwaka 2009, akirithi mikoba ya Mserbia mwenzake, Profesa Dusan Kondic. Papic alitua Yanga akitokea Hearts of Oak ya Ghana, ambako alitumuliwa kwa sababu ya matokeo mabaya.
Kocha huyo, aliyewahi kuzinoa timu za Orlando Pirates, Kaizer Chiefs, Martzburg United za Afrika Kusini, Enyimba, Kwara United na Lobi Stars za Nigeria, alitupiwa virago Februari mwaka huu na nafasi yake kuchukuliwa na Timbe.
Timbe alikaririwa juzi akisema kuwa, mkataba wake na Yanga unatarajiwa kumalizika Mei mwakani, hivyo anashangazwa na taarifa zinazoripotiwa kuwa, mkataba wake umemalizika. Alisema bado uongozi haujampa taarifa yoyote kuhusu kusitisha mkataba wake.
"Mimi sina tatizo la kukatisha mkataba wangu, cha msingi ni kwamba nataka wanilipe haki zangu zote,"alisema kocha huyo.
Timbe alileta heshima kubwa Yanga msimu uliopita baada ya kuiwezesha kutwaa ubingwa wa ligi kuu na ule wa Kombe la Kagame. Tatizo kubwa lililosababisha Timbe aondolewe ni madai kuwa, amekuwa akikataa kutekeleza ushauri wa mabosi wake.
Papic alikuwepo uwanjani, akiwa ameketi jukwaani wakati Yanga ilipocheza na JKT Oljorokwenye uwanja wa Chamazi. Wakati wa mechi hiyo, kocha huyo aliwaeleza waandishi wa habari kwamba, ameshafanya mazungumzo ya awali na uongozi wa Yanga ili ainoe kwa mkataba wa muda mfupi.
Mserbia huyo alijigamba kuwa, hana wasiwasi na Simba kwa vile anaifahamu vyema na ameahidi kuwapa raha mashabiki wa Yanga kwa madai kuwa, anayo dawa ya kuwafunga wapinzani wao.
Pamoja na majigambo yake hayo, Papic ameshaonja ladha ya vipigo viwili kutoka kwa Simba. Mara ya kwanza ilikuwa Oktoba 31, 2009 wakati Yanga ilipochapwa bao 1-0 na Simba. Bao hilo la pekee lilifungwa na Mussa Hassan 'Mgosi'.
Papic aliendelea kuonjeshwa ladha nyingine ya kipigo Aprili 18 mwaka jana wakati Yanga ilipochapwa mabao 4-3 na wapinzani wao hao, mabao ya Simba yakifungwa na Uhuru Selemani, Mgosi aliyefunga mawili na Hillary Echessa. Mabao ya Yanga yalifungwa na Athumani Iddi 'Chuji' na Jerry Tegete, aliyefunga mawili.
Kocha huyo aliweza kuiongoza Yanga kushinda dhidi ya Simba katika mechi ya kwanza ya ligi iliyochezwa Oktoba 16 mwaka jana kwenye Uwanja wa CCM Kirumba mjini Mwanza. Katika mechi hiyo, Yanga ilishinda bao 1-0, lililowekwa kimiani na Jerry Tegete dakika ya 70.
Papic pia aliiwezesha Yanga kuifunga Simba mabao 2-1 katika mechi ya nusu fainali ya michuano ya Kombe la Tusker na baadaye kuwalaza watani wao hao kwa penalti 3-1 katika mechi ya kuwania Ngao ya Hisani msimu uliopita.
Kwa upande wa Simba, hali inaonekana kuwa shwari huku kocha wake, Moses Basena kutoka Uganda akijigamba kuwa, wataendeleza ubabe kwa watani wao hao. Basena anajivunia kikosi chake kwa madai kuwa, hivi sasa kimeanza kushika maelekezo yake.
Basena alisema timu yake ilikuwa ikiibuka na ushindi kiduchu katika mechi za awali za ligi hiyo kutokana na washambuliaji wake kuwa na papara kila wanapokaribia lango la timu pinzani. Alisema tayari ameshalirekebisha tatizo hilo na ndio sababu waliweza kushinda mechi za hivi karibuni kwa mabao mengi.
Hata hivyo, Basena alikiri kuwa kwa kawaida mechi kati ya Simba na Yanga huwa hazitabiriki, lakini kwa jinsi alivyowaona mahasimu wao katika siku za hivi karibuni, uhakika wa ushindi kwa timu yake ni mkubwa.
MSIMAMO WA LIGI
Timu hizo mbili zinaingia uwanjani huku Simba ikiwa inaongoza ligi kwa tofauti ya pointi sit kati yake na Yanga, inayoshika nafasi ya tatu. Simba inazo pointi 27 baada ya kucheza mechi 11 wakati Yanga imeambulia pointi 21 kutokana na idadi hiyo ya michezo.
Simba ilianza ligi hiyo kwa kuichapa JKT Oljoro mabao 2-0 mjini Arusha, ikaichapa Coastal Union bao 1-0 mjini Tanga, iliilaza idadi hiyo ya bao Villa Squad mjini Dar es Salaam,ikatoka suluhu na Azam kabla ya kuichapa Polisi Dodoma bao 1-0 mjini Dar es Salaam.
Katika mechi zingine, Simba ililazimishwa sare ya bao 1-1 na Kagera Sugar mjini Bukoba, ikatoka sare ya mabao 3-3 na Toto African mjini Mwanza, iliichapa Mtibwa Sugar bao 1-0 mjini Dar es Salaam, iliicharaza African Lyon mabao 4-0, iliichapa Ruvu Shooting mabao 2-0 kabla ya kuifunga JKT Ruvu idadi hiyo ya mabao.
Watani wao wa jadi Yanga walianza ligi hiyo vibaya baada ya kuchapwa bao 1-0 na JKT Ruvu mjini Dar es Salaam, wakalazimishwa sare ya bao 1-1 na Moro United, walitoka suluhu na Mtibwa Sugar mjini Morogoro, walilazimishwa sare ya bao 1-1 na Ruvu Shooting kabla ya kuzinduka na kuichapa African Lyon mabao 2-1 mjini Dar es Salaam.
Katika mechi zingine, Yanga ilikwaa kisiki kwa Azam baada ya kukubali kichapo cha bao 1-0, ikaibwaga Villa Squad mabao 3-2, ikaibamiza Coastal Union mabao 5-0, iliichapa Kagera Sugar bao 1-0, iliicharaza Toto African mabao 4-2 kabla ya kuichapa JKT Oljoro bao 1-0. Mechi zote hizo zilichezwa mjini Dar es Salaam.
Kwa mujibu wa takwimu, safu za ushambuliaji za Simba na Yanga zinaonekana kuwa na ukali unaolingana baada ya kila timu kufunga mabao 18 katika mechi 11. Hata hivyo, safu ya ulinzi ya Yanga imeruhusu nyavu zake kutikisika mara tisa wake ile ya Simba imeruhusu mabao manne.
Mshambuliaji Kenneth Asamoah ndiye anayeongoza kwa kuifungia Yanga mabao saba wakati Emmanuel Okwi wa Simba anaongoza kwa kuifungia timu yake mabao matano.
JINO KWA JINO
Vikosi vyote viwili vitashuka dimbani huku vikiwa havina majeruhi. Kocha Basena alisema anashukuru kwamba, wachezaji wake, Mwinyi Kazimoto na Machaku Salum, ambao walikuwa majeruhi, wamepona. Isipokuwa bado ana wasiwasi na hali za afya za mabeki Victor Costa na Amir Maftah.
Costa aliumia wakati akiwa kwenye mazoezi ya timu ya Taifa, Taifa Stars iliyokuwa ikijiandaa kwa pambano lake la mwisho la michuano ya kuwania kufuzu kucheza fainali za Afrika dhidi ya Morocco wakati Maftah aliumia katika mechi ya ligi dhidi ya Kagera Sugar.
Katika mechi za hivi karibuni, Basena amekuwa akiwatumia zaidi Nassoro Cholo, Juma Jabu, Juma Nyosso na Obadia Mungusa katika safu ya ulinzi, wakiongozwa na kipa Juma Kaseja. Katika kiungo, amekuwa akiwachezesha zaidi Jerry Santo, Shomari Kapombe na washambuliaji ni Gervas Kago, Haruna Moshi, Felix Sunzu, Uhuru na Machaku.
Kwa upande wa Yanga, wachezaji wake Shadrack Nsajigwa, Nurdin Bakari, Stephano Mwasika, Davis Mwape na Idrisa Rashid, ambao nao walikuwa majeruhi, wameripotiwa kuwa fiti baada ya kupona.
Kupona kwa Mwasika kumeipa ahueni kubwa Yanga kutokana na uwezo wake wa kucheza nafasi ya beki wa kushoto huku akipanda mbele kusaidia mashambulizi. Nafasi yake ilikuwa ikizibwa na Oscar Joshua.
Kocha Timbe alikuwa akiwatumia zaidi kipa Yaw Berko, Godfrey Taita, Joshua, Bakari Mbegu na Nadir Haroub kucheza safu ya ulinzi huku viungo akiwachezesha Juma Seif, Rashid Gumbo na Haruna Niyozima. Safu ya ushambuliaji inaundwa na Tegete, Hamiza Kiiza, Asamoah na Pius Kisambale.
MSIMAMO WA LIGI KUU TANZANIA BARA
P W D L GF GA PTS

Simba SC 11 8 3 0 18 4 27 2

Young Africans 11 6 3 2 18 9 21 3

Azam 10 6 3 1 11 3 21 4

JKT Oljoro 11 5 4 2 9 6 19 5

Mtibwa Sugar 10 4 3 3 11 9 15 6

JKT Ruvu 11 3 6 2 13 12 15 11

African Lyon 11 3 3 5 8 15 12 7

Kagera Sugar 10 2 5 3 11 11 11 8

Ruvu Shooting 10 2 5 3 8 9 11 9

Toto African 10 2 4 4 12 14 10 10

Moro United 10 2 4 4 13 17 10 13

Coastal Union 11 3 1 7 11 17 10 12

Polisi Dodoma 11 1 5 5 10 14 8 14

Villa Squad 11 1 3 7 9 23 6

No comments:

Post a Comment