KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, October 20, 2011

ASLAY: Chipukizi anayetamba na kibao cha Nitakusemea




KWA umri, msanii Aslay Isihaka bado ni kijana mdogo. Ni mwanafunzi wa kidato cha kwanza katika shule ya sekondari ya Tandika, Dar es Salaam. Umri wake ni miaka 15.
Aslay ni mmoja wa watoto wanaolelewa katika kituo cha Mkubwa na Wanawe, kinachomilikiwa na Saidi Fela, mmiliki wa kikundi cha TMK Wanaume Family. Kituo hiki kipo maeneo ya Temeke-Mwembe Yanga, Dar es Salaam.
Fela ameanzisha kikundi hiki kwa lengo la kuibua na kuendeleza vipaji vya wasanii chipukizi. Amekusanya vijana wadogo kutoka maeneo mbalimbali ya Dar es Salaam, hasa Temeke na wengine kutoka mikoani.
Katika kituo hicho, mbali na kufundishwa muziki, watoto hao pia hufundishwa masomo mbalimbali ya darasani. Mwalimu wao wa muziki ni msanii, Mheshimiwa Temba.
Tangu alipojiunga na kituo hicho kwa ridhaa ya wazazi wake, Aslay amedhihirisha wazi kuwa muziki upo kwenye damu yake na ni kipaji alichozaliwa nacho.
Kibao chake cha ‘Nitakusemea’, ambacho amekirekodi chini ya usimamizi wa Fela, ni uthibitisho wa wazi kuwa, kijana huyu amejaliwa sauti murua, inayoweza kumshawishi na kumvuta mtu yeyote kuisikiliza.
Kwa sasa, kibao hicho kimekuwa kikitamba kwenye vituo mbalimbali vya radio na televisheni nchini. Pia kinapendwa sana na watoto wa umri wake na hata watu wazima, hasa kina mama.
Video ya wimbo huo imenakshiwa zaidi na msanii wa maigizo, maarufu kwa jina la Pembe, ambaye ameigiza kama baba yake Aslay. Lakini sauti halisi ya maneno yanayotamkwa na Pembe ni ya Fela.
Akihojiwa katika kipindi cha Jambo, kilichorushwa hewani na kituo cha televisheni cha TBC 1 hivi karibuni, Aslay alikiri kuwa, kibao hicho kimemfanya awe maarufu.
“Kuna siku nilipokwenda shule, mwalimu wangu alinitizama kisha akaniuliza, ‘kumbe wewe unaweza kuimba’,” alisema Aslay.
“Lakini kwangu mimi, umaarufu huo unazidi kuniongezea hamasa ya kufanya vizuri zaidi. Watu wengi wananiunga mkono, hasa akina mama, ambao wimbo huo ni kama vile unawatetea.
“Baadhi ya akina mama wamesema nimeimba vizuri, lakini kwa wanaume, wanaona kama vile nimewaharibia. Baadhi yao wamekuwa wakinilaumu kwa kuimba wimbo huo,”aliongeza.
Kwa mujibu wa Aslay, anatarajia kurekodi albamu yake ya kwanza mwezi ujao na itakuwa na vibao 10. Alisema lengo lake ni kurekodi vibao vikali vitupu badala ya vile vya kujazia albamu.
Aliwataja baadhi ya wasanii maarufu wa muziki wa kizazi kipya aliowashirikisha kurekodi nyimbo zake kuwa ni pamoja na Saidi Chege, Diamond, Mheshimiwa Temba, Zahir Ally Zorro na Linah.
Aslay alitamba kuwa, licha ya kuwepo wasanii wengi wazuri wa umri wake kama vile Dogo Janja na Young D, hawana uwezo wa kumfikia kimuziki.
“Hawa madogo wote ni watoto kwangu. Wao wanachana, mimi naimba,”alisema Aslay.
“Dogo Janja amekuwa akiongea sana kuhusu mimi, lakini bado sana, haniwezi,”aliongeza.
Hata hivyo, Aslay amekiri kuwa, bado ni mapema kwake kupata manufaa kutokana na muziki, lakini wazazi na ndugu zake wameyafurahia mafanikio yake.
Alisema anachokipata kwa sasa ni pesa ndogo ndogo kwa matumizi yake ya shule. Alisema huduma ya malazi na chakula anaipata katika kituo anachoishi.
Aslay anamzimia sana msanii mwenzake wa kituo hicho anayejulikana kwa jia la Dula, ambaye amemwelezea kuwa ni mkali wa kuimba na ana kipaji cha aina yake.
Msanii huyu pia ni shabiki mkubwa wa soka. Kwa timu za hapa nchini, anavutiwa sana na Simba na kwa timu za nje, anaishabikia zaidi Chelsea.
Lengo la Aslay ni kuwa mwanamuziki wa kimataifa. Anapenda kuwa maarufu duniani, kama ilivyokuwa kwa nyota wa pop nchini Marekani, marehemu Michael Jackson.

No comments:

Post a Comment