KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, October 27, 2011

Simba haina imani na Mbaga


KLABU ya Simba imesema haina imani na mwamuzi Oden Mbaga wa Dar es Salaam, aliyepangwa kuchezesha mechi ya ligi kuu kati yao na Yanga.
Ofisa Habari wa Simba, Ezekiel Kamwaga alisema mjini Dar es Salaam jana kuwa, uongozi umetatizwa na uamuzi wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), kumteua Mbaga kuchezesha mechi hiyo.
Kamwaga alisema Mbaga ndiye aliyechezesha mechi ya mwisho ya ligi kuu kati ya timu hizo na kusababisha linusurike kuvunjika kutokana na uamuzi wake wa utata.
Alisema katika pambano hilo, Mbaga alikataa bao la wazi la kusawazisha la Simba lililofungwa na Mussa Hassan Mgosi na baadaye kulikubali, hali iliyosababisha vurugu kubwa.
“Udhaifu huu wa kimaamuzi ungeweza kusababisha maafa makubwa uwanjani. Ndio maana Simba imetatizwa na uamuzi wa TFF kumteua tena Mbaga kuchezesha mechi hiyo,”alisema Kamwaga.
Hata hivyo, Kamwaga alisema hawatasusia pambano hilo kwa namna yoyote, lakini wanapenda kuweka wazi msimamo wao kwamba, hawana imani na mwamuzi huyo.
Katika mechi hiyo, Mbaga atasaidiwa na Hamisi Chang'walu wa Dar es Salaam na John Kanyenye wa Mbeya. Kamisaa wa mchezo huo atakuwa Mohamed Nyange wa Dodoma.
Nayo Yanga imesema, hawana uwezo wa kupinga maamuzi ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) kumteua Mbaga kuchezesha mechi hiyo.
“Ni kweli tulikutana na kumjadili, lakini tumeona hatuna sababu ya kumpinga na tunapaswa kuheshimu maamuzi ya TFF maana hata tukimtaka mwamuzi mwingine, tukifungwa, hadithi itakuwa ni ileile,”alisema.

No comments:

Post a Comment