KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, October 27, 2011

JOTI: Mimi ni jembe kweli kweli






UNAPOWATAJA ama kuwazungumzia wasanii wa fani ya maigizo ama vichekesho hapa nchini, huwezi kukosa kutaja jina la Lucas Mhavile, maarufu zaidi kwa jina la Joti.
Ni msanii mwenye vipaji lukuki kwani ana uwezo wa kuigiza kiufasaha nafasi ya mzee, binti mdogo, mwanafunzi, mwanamke, mpemba na hata mlemavu.
Uwezo wake wa kuigiza nafasi hizo ni miongoni mwa mambo yaliyomfanya apate umaarufu na kuwa kivutio kikubwa kwa mashabiki kupitia kundi lake la Ze Komedi Orijino.
Awali, kundi hili lilikuwa likionyesha vitu vyake kupitia kituo cha televisheni cha East Africa, lakini baadaye kilihamishia maonyesho yake kupitia kituo cha TBC 1.
Joti amekuwa kivutio kwa watazamaji kutokana na ubunifu wake katika kuigiza nafasi, ambazo huwa akishiriki kuigiza.
Kwa mfano, siku za nyuma alikuwa akivutia watazamaji kutokana na kusoma taarifa ya habari ya Orijino Komedi akiigiza sauti ya Kipemba. Alisoma taarifa hiyo kwa kushirikiana na Masanja Mkandamizaji.
Msanii huyu mfupi lakini machachari, pia alijipatia sifa kemkem alipoigiza kipande cha ‘Aliyefulia’ na baadaye, Asha Ngedele. Joti pia ndiye msanii anayevutia zaidi anapoigiza kama babu au mtoto mtukutu.
Sifa yake nyingine ni kujibadilisha kuwa kama binti ama mwanamke pashkuna. Hana tofauti na yule msanii maarufu wa vichekesho barani Ulaya, marehemu Charle Chaplin.
Pengine kikubwa zaidi kilichompa umaarufu ni ule ubunifu wake wa staili ya utembeaji, ambayo imekuwa ikipendwa na vijana wengi. Hata waimbaji taarabu wameisifu na kuiimba staili hiyo kwenye nyimbo zao.
Akihojiwa na mtandao wa Filamucenter hivi karibuni, Joti alisema kwa kawaida, anapokuwa kazini, lazima ahakikishe kuwa, anafanyakazi kwa nguvu zote ili kazi yake iwe bora.
Joti alisema yeye ni tofauti na wasanii wengine, ambao hujisahau baada ya kuwa na mashabiki wengi na kubweteka kwa mafanikio waliyoyapata.
Kwa mujibu wa Joti, sera za kundi lake la Ze Komedi Orijino ni kazi na si kuchekesha pekee. Alisema kila wanapokuwa kazini, huheshimu kazi yao.
“Kuna watu hawapendi kuambiwa ukweli kuhusu wanachokifanya. Wao wanapenda sana sifa, ambazo si mali yao,”alisema.
“Unapokuwa Ze Komedi Orijino, ni kazi tu mtindo mmoja, ndiyo maana Joti unayekutana naye kitaani (mtaani) si Joti wa TBC 1,” aliongeza.
“Nikiwa kazini, nalima tu. Si unajua kuwa mimi ni Jembe, ukiniweka popote nalima. Babu, mtoto, nakamua. Si unajua maisha na hasa ukichukulia kwamba, sanaa hivi sasa inachemka,” alisema msanii huyo.
Joti alisema yeye na wasanii wenzake wa Ze Komedi Orijino wamekuwa wakitumia muda mwingi kujituma kwenye kazi sa sanaa ili kunufaika na si vinginevyo ndio sababu thamani yao ipo juu.
Kwa upande wake, Meneja Uzalishaji wa kundi hilo, Sekioni Davidi, maarufu kwa jina la Seki, alisema kundi lake limepata mafanikio makubwa kutokana na kutambua thamani ya sanaa.
Seki alisema ni kutokana na kutambua hilo, wamepanga viwango vya juu katika malipo yao kwenye maonyesho mbalimbali, ambayo huwa wakialikwa kuyafanya.
Mbali na kupata fedha kutokana na matangazo yanayorushwa kwenye kipindi chao cha Orijino Komedi, Seki alisema wamekuwa wakipata fedha nyingi kupitia maonyesho.
“Yeyote anayelihitaji kundi letu kwenye onyesho, lazima achukulie sanaa yetu kama kazi. Hatutaki mtu anayeichukulia sanaa kama zamani, tunataka mialiko michache, lakini yenye thamani kubwa kwetu,” aliongeza Seki.

No comments:

Post a Comment