KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Monday, October 31, 2011

Simba, Yanga zaingiza mil 337/-



Mechi namba 78 ya Ligi Kuu ya Vodacom kati ya Yanga na Simba iliyochezwa Oktoba 29 mwaka huu Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam imeingiza sh. 337,537,000.

Watazamaji waliokata tiketi kushuhudia mechi hiyo walikuwa 53,366 ambapo kiingilio kilikuwa sh. 5,000, sh. 7,000, sh. 10,000, sh. 15,000 na sh. 20,000 kwa VIP A.

Baada ya kuondoa gharama za mchezo na Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) ambayo ni sh. 51,488,694 na gharama za awali za mchezo sh. 27,405,250 kila timu ilipata sh. 77,592,916.

Mgawo mwingine ulikwenda kwa uwanja (sh. 25,864,305), TFF (sh. 25,864,305), Mfuko wa Maendeleo ya Mpira wa Miguu- FDF (sh. 12,932,152), gharama za mchezo (sh. 25,864,305), Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Dar es Salaam- DRFA (sh. 10,345,722) na Baraza la Michezo la Taifa- BMT (sh. 2,586,430).


TAIFA STARS YAPANGIWA MSUMBIJI CAN 2013

Tanzania (Taifa Stars) imepangwa kucheza na Msumbiji katika kinyang’anyiro cha kutafuta tiketi ya kucheza fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika zitakazofanyika mwaka 2013 nchini Afrika Kusini.

Upangaji ratiba wa mechi hizo za mchujo ulifanywa juzi (Oktoba 28 mwaka huu) na kamati ndogo ya michuano hiyo mjini Malabo, Equatorial Guinea. Jumla ya nchi 47 ikiwemo mwenyeji Afrika Kusini ndizo zilizothibitisha kucheza michuano hiyo.

Nchi 16 zilizofuzu kucheza fainali za mwakani nchini Gabon na Equatorial Guinea zenyewe zimepitishwa moja kwa moja hadi raundi ya mwisho ya mchujo itakayoanza baada ya fainali za 2012.

Raundi ya kwanza ya awali itahusisha nchi nne ambazo kwenye ubora wa viwango ndizo ziko chini ili kupata mbili zitakazoingia raundi ya pili ya awali itakayokuwa na nchi 28. Nchi hizo ni Swaziland, Sao Tome, Lesotho na Shelisheli.

Stars imepangiwa kucheza na Msumbiji katika raundi hiyo ya pili ya awali. Tarehe za mechi hizo ambazo zitachezwa katika nusu ya kwanza ya mwaka 2012 zitatangazwa baadaye.

Mechi nyingine za raundi hiyo zitakuwa kati ya Ethiopia na Benin, Rwanda na Nigeria, Congo na Uganda, Burundi na Zimbabwe, Algeria na Gambia, Kenya na Togo, Sierra Leone na mshindi kati ya Sao Tome na Lesotho.

Nyingine ni Guinea Bissau na Cameroon, Chad na Malawi, mshindi kati ya Shelisheli na Swaziland dhidi ya Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo, Jamhuri ya Afrika ya Kati na Misri, Madagascar na Cape Verde na Liberia na Namibia.

Timu 14 zitakazopita hatua hiyo zitaungana na 16 zilizofuzu kwa ajili ya fainali za Gabon/Equatorial Guinea kucheza raundi ya mwisho kupata 15 zitakazoungana na wenyeji Afrika Kusini kwa ajili ya fainali za 2013. Raundi hiyo itachezwa kati ya Septemba na Oktoba mwakani.

No comments:

Post a Comment