KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, October 27, 2011

DK. SHENI: Serikali kujenga studio ya kisasa Zenj


RAIS wa Zanzibar Dk. Ali Mohammed Sheni amesema, serikali yake imetenga bajeti maalumu kwa ajili ya kujenga studio ya kisasa ya muziki visiwani humo.
Dk. Sheni amesema lengo la kujengwa kwa studio hiyo ni kuwawezesha wasanii wa muziki wa taarab kurekodi nyimbo za kiasili za muziki huo.
Kwa mujibu wa Dk. Sheni, studio hiyo pia itakuwa wazi kwa wasanii wa aina nyingine ya muziki katika visiwa hivyo.
Dk. Sheni alisema hayo mwishoni mwa wiki iliyopita wakati wa uzinduzi wa kikundi cha taarab cha Tausi Women Musical Club uliofanyika kwenye hoteli ya Bwawani mjini hapa.
"Tumepanga katika bajeti ijayo, kuweka fungu maalumu kwa ajili ya kujenga studio, ambayo itawasaidia wasanii wa muziki wa taarab na mingineyo kurekodi nyimbo zao kwa gharama nafuu,”alisema.
Dk. Sheni alisema lengo la serikali ni kuendelea kuuenzi utamaduni wa Zanzibar, hasa muziki wa asili wa taarab ili usipotee.
Alisema serikali yake inathamini mchango mkubwa wa muziki wa taarab asilia kwa vile ni utamaduni pekee unaosaidia kuvitangaza visiwa hivyo kimataifa.
Aliupongeza uongozi wa kikundi hicho cha Tausi kwa uamuzi waliochukua katika kuendeleza muziki wa taarab asilia na kuongeza kuwa, serikali ina kila sababu ya kukiunga mkono.
"Napenda kutoa shukurani za dhati na pongezi kwa uongozi wa Tausi kutokana na kusimama kwao kidete katika kuuendeleza utamaduni wa Zanzibar kupitia muziki wa taarab asilia,”alisema.
Dk. Sheni aliwapongeza wasanii wa Tausi, kikundi kinachoundwa na akina mama watupu kwamba na kuongeza kuwa, anaamini kitadumu kwa muda mrefu.
Mkurugenzi wa kikundi hicho, Maryam Hamdani alisema, kilianzishwa mwaka 2009, kikiwa na wasanii 22, wote wakiwa wanawake watupu.

No comments:

Post a Comment