KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, October 20, 2011

Isha Mashauzi amuangukia Mzee Yussuf


MSANII nyota wa muziki wa taarab nchini, Isha Ramadhani 'Mashauzi' ametamka hadharani kwamba, alifanya kosa kubwa kuondoka katika kikundi cha Jahazi.
Isha alisema hayo mwishoni mwa wiki iliyopita wakati kundi la Jahazi, chini ya mkurugenzi wake, Mzee Yussuf lilipofanya onyesho kwenye ukumbi wa Travertine, Magomeni, Dar es Salaam.
Mwanamama huyo mwenye mbwembwe na madaha awapo jukwaani, alikuwa mwimbaji nguli katika kundi hilo na kujipatia umaarufu mkubwa kutokana na tungo zake kukubalika na mashabiki wengi.
Baada ya kuondoka katika kundi hilo, msanii huyo aliamua kuanzisha kundi lake la Mashauzi Classic na tangu hapo alikuwa haonekani katika maonyesho ya Jahazi.
Kuondoka kwa mwimbaji huyo katika kundi la Jahazi, kuliibua maswali mengi na baadhi ya mashabiki walijenga hisia kwamba, huenda alikuwa na ugomvi na Yussuf.
Lakini Isha aliamua kuvunja ukimya mwishoni mwa wiki iliyopita kwa kusema kuwa, kitendo alichofanya hakikuwa cha kiungwana.
Isha alitumia fursa hiyo kumuomba radhi Yussuf pamoja na wasanii wengine wa kundi la Jahazi, kauli iliyopokelewa kwa shangwe nyingi na mashabiki waliohudhuria onyesho hilo.
Mbali ya kuomba radhi, Isha alipanda jukwaani wakati wa onyesho hilo na kuimba moja ya vibao vyake vya zamani, alipokuwa Jahazi.
Tukio hilo liliwafanya mashabiki na wapenzi wa muziki huo kumpongeza Isha kwa kitendo chake hicho cha kiungwana cha kuomba radhi baada ya kutambua amefanya kosa.
Isha alisema si vyema kwa sasa kuendeleza malumbano na kujengeana chuki baina ya wasanii kwa vile kufanya hivyo hakuna faida yoyote kwao zaidi ya kudumaza soko la muziki huo na maendeleo yake.

No comments:

Post a Comment