KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, October 20, 2011

NCHUNGA: Tutawekeana mipaka na Manji


SWALI: Tunaomba ufafanuzi kutoka kwako, je ni kweli mmemuomba mfadhili wa zamani wa Yanga, Yusuf Manji kurejea kuisaidia klabu yenu?
JIBU: Ni kweli tumefanya hivyo na tumewahi kuwa na mazungumzo naye kabla hajasafiri kwenda nje ya nchi kwa shughuli zake za biashara na sasa tayari amerejea na wakati wowote tutafanya naye kikao kingine.
Pamoja na ukweli wa jambo hilo, tumeangalia kwa kina sababu, ambazo awali zilimfanya ajiweke pembeni kuisaidia klabu yetu na timu kwa jumla.
Sio siri kwamba, klabu yetu kwa sasa ina hali mbaya sana, hivyo tumeona kuna umuhimu wa kumuomba mfadhili huyo arejee kuisaidia klabu kwa moyo wake wote.
SWALI: Binafsi unadhani ni sababu zipi zilizochangia kumfanya Manji ajiweke pembeni? Inawezekana ni lugha chafu kutoka kwa baadhi ya wanachama au kuna mambo mengine?
JIBU: Kwa kweli yapo mambo mengi, yakiwemo hayo uliyoyataja.Wapo baadhi ya wanachama walifikia hatua ya kutoa lugha chafu kwake wakati yeye ndiye anayetoa pesa zake wakati wanachama hao wamekuwa wakishindwa kuchangia hata shilingi mia tano kwa ajili ya maji ya kunywa ya wachezaji.
Ulifika wakati uongozi ukaona kwamba, ni vyema tumuombe Manji arejee kutusaidia kuiendesha Yanga kwa sababu klabu hii ni mali ya watanzania wengi, matajiri na masikini. Hao wanachama wachache wenye upeo mdogo wa kuelewa mambo, tutawadhibiti, hatuwezi kuwaacha watuyumbishe.
Vilevile tupo mbioni kufanya mambo mengi muhimu ili kuhakikisha wanachama wakorofi hawapati nafasi ya kufanya ama kuonyesha vitendo vya utovu wa nidhamu kwa watu, ambao wamekuwa wakijitolea pesa zao kuisaidia Yanga. Tunataka kuona Yanga ikipata mafanikio.
Hebu fikiria, Manji alishafanya mazungumzo na baadhi ya wafadhili wa ndani na nje ya nchi wakiwemo Wajapan kwa ajili ya kuwekeza Yanga. Lakini baada ya kujiengua kwa sababu ya kashfa za hawa wanachama, mpango huo ulikufa.
Hatupendi kuona hili likitokea tena. Tutajipanga vizuri kushirikiana naye ili tuweze kupata watu watakaoisaidia Yanga na kuiwezesha kuwa klabu ya kimataifa.
SWALI: Moja ya malalamiko yaliyokuwepo huko nyuma ni kwamba, Manji alikuwa akiingilia madaraka ya uongozi. Je, mna mpango wowote wa kuweka mipaka ya utendaji kati ya uongozi na mfadhili huyo endapo atakubali kuisaidia tena klabu yenu?
JIBU: Kwa kweli jambo hilo tumeliangalia kwa umakini mkubwa, ndio maana kabla ya kuingia naye mkataba mpya wa kuisaidia klabu yetu, itabidi akutane na kamati ya utendaji ya Yanga.
Hapo tutaweza kumpa nafasi na kumueleza kazi zake ndani ya klabu na mipaka yake na sisi viongozi tutafahamishana mipaka kati yetu na mfadhili huyo.
Hili jambo litasaidia sana kuondosha mkanganyiko wa kiutendaji na kujenga Yanga imara na yenye umoja badala ya kuendelea kuwepo utengano.
Unajua mwakani tunaiwakilisha nchi katika mashindano ya kimataifa, hivyo tunahitaji utulivu ili tuweze kuifanya Yanga ifanye vizuri katika michuano ya klabu bingwa Afrika.
Nina imani Manji ataweza kutoa mchango mkubwa kuhakikisha ndoto yetu inatimia bila ya hofu yoyote, ikiwemo kutuwezesha kwenda nje ya nchi kucheza michezo kadhaa ya kirafiki na kuwapa uzoefu zaidi wachezaji wetu.
SWALI: Vipi kuhusu mipango yenu ya kutaka kujitegemea zaidi kwa sababu Manji ni binadamu, anaweza kuwepo au asiwepo, sasa mmepanga kufanya nini?
JIBU: Tumeanza kujipanga kuandaa hafla ya chakula cha usiku kwa ajili ya kuichangia klabu. Tayari tumemwandia barua Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jakaya Kikwete ili awe mgeni rasmi katika hafla hiyo. Tunasubiri kujibiwa na Ikulu. Baada ya majibu hayo, ndipo tutapanga tarehe ya kuandaa chakula hicho. Nina hakika tutaweza kuchangiwa pesa nyingi tu.
Kwa hesabu za haraka haraka, tunahitaji karibu shilingi bilioni sita ili tuweze kukamilisha programu zetu za ujenzi wa uwanja, jengo la Mafia na mambo mengine.
SWALI: Unapenda kuwaeleza nini wanachama na wapenzi wa klabu ya Yanga?
JIBU: Kwanza kabisa nawaomba manachama na wapenzi wa Yanga tuwe kitu kimoja ili tuweze kushirikiana na Manji na watu wengine wenye nia ya kutaka kuisaidia klabu yetu. Tusiwape nafasi watu wenye nia ya kutaka kutuvuruga.
Ni vyema wale wote wenye kuitakia mabaya Yanga katika kipindi hiki, wakae pembeni, waache uongozi na wanachama wenye nia ya kuiendeleza Yanga wafanye kazi zao, hatutaki kuona wanatuchanganya, tuna mambo mengi ya kufanya.

No comments:

Post a Comment