KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, October 20, 2011

Mtanzania anayekipiga Chelsea, ruksa kuichezea Taifa Stars


SHIRIKISHO la Soka Tanzania (TFF) limesema, milango ipo wazi kwa mchezaji chipukizi, Adam Nditi, anayecheza soka ya kulipwa England, kuichezea timu ya Taifa, Taifa Stars.
Nditi ni mmoja wa wachezaji wanaounda timu ya vijana wa chini ya umri wa miaka 21 ya Chelsea na umahiri wake katika kuwazuia washambuliaji wa timu pinzani umempatia sifa lukuki.
Ofisa Habari wa TFF, Boniface Wambura alisema mjini Dar es Salaam wiki hii kuwa, mwenye jukumu la kumwita mchezaji huyo ni Kocha Mkuu wa Taifa Stars, Jan Poulsen.
“Kwa taratibu zilivyo, mwenye jukumu la kuteua wachezaji wa Taifa Stars ni kocha,”alisema ofisa huyo wa TFF.
“Baada ya uteuzi, inachokifanya TFF ni kuhakikisha wachezaji walioteuliwa wanapatikana. Poulsen hajawahi kumteua Nditi,”aliongeza.
Kocha Mkuu mpya wa Chelsea, Villas-Boas hivi karibuni alimpandisha Nditi kutoka kwenye kikosi cha vijana wa chini ya miaka 18 kwenda cha vijana wa chini ya miaka 21.
Jina la mchezaji huyo limo kwenye orodha ya wachezaji wa timu hiyo ya Chelsea, iliyowasilishwa kwenye Chama cha Soka cha England.
Kupandishwa daraja kwa mchezaji huyo wa Kitanzania kunamaanisha kwamba, anaendelea vizuri katika klabu hiyo tajiri ya England.
Nditi alianza kucheza soka katika chuo cha kukuza vipaji cha klabu hiyo, ambapo amekuwa mchezaji wa kutumainiwa katika kikosi cha vijana wa chini ya miaka 18 kwa zaidi ya misimu mitatu.
Akiwa katika chuo hicho, Nditi alikuwa chini ya kocha Muingereza, Neil Bath, lakini baada ya kupandishwa, sasa atakuwa chini ya kocha mwingine, Muingereza Adrian Viveash.
Nditi alizaliwa Septemba 18, 1994 huko Kikwajuni, Zanzibar kabla ya kwenda Uingereza, ambako alijiunga na chuo cha soka cha Chelsea.
Hata hivyo, kumezuka wasiwasi iwapo Nditi anaweza kuichezea Taifa Stars baada ya kuwepo taarifa kwamba, tayari kijana huyo ameshapara uraia wa Uingereza.
Sheria zilizopo sasa hapa nchini haziruhusu Mtanzania kuwa na uraia wa nchi mbili. Marekebisho ya sheria hiyo bado yanaendelea kufanyika kwa lengo la kuruhusu watanzania kuwa na uraia wa nchi mbili.
Marekebisho hayo yamelenga kuwawezesha watanzania waliopo nje, kuwekeza hapa nchini kwa lengo la kukuza uchumi.
Nditi amejipatia umaarufu mkubwa kwa klabu ya Chelsea kutokana na kuimudu vyema nafasi ya beki wa kushoto na kiungo mshambuliaji. Alijiunga na Chelsea mwaka 2008.
Alianza kuichezea timu ya chuo cha soka cha Chelsea msimu wa 2010/11 katika mechi dhidi ya Tottenham. Akiwa kwenye kikosi hicho, alicheza zaidi nafasi ya beki wa kushoto.
Alifunga bao lake la kwanza Aprili mwaka 2011 wakati timu ya chuo hicho ya Chelsea ilipomenyana na Norwich.
Nditi pia alikuwemo kwenye kikosi cha vijana cha Chelsea kilichomenyana na Arsenal Januari 20 mwaka huu katika mechi ya Kombe la FA la vijana na kutoka sare ya bao 1-1. Mechi hiyo ilipigwa kwenye uwanja wa Stamford Bridge.
Majina yake halisi ni Adam Eric Richard Nditi.

No comments:

Post a Comment