KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, May 3, 2012

Zawadi Kombe la Ester zaongezwa


MBUNGE wa Viti Maalumu (CCM) mkoa wa Mara, Ester Bulaya ameamua kuongeza zawadi kwa ajili ya washindi watatu wa kwanza wa mashindano ya Kombe la Ester.
Akizungumza na waandishi wa habari mjini Dar es Salaam jana, Ester alisema bingwa wa kwanza mwaka huu atazawadiwa kitita cha sh. 500,000 na kikombe.
Ester alisema mshindi wa pili atapata sh. 250,000 na kikombe, mshindi wa tatu atapata sh. 150,000, mfungaji bora na mchezaji bora watapata sh. 50,000 kila mmoja wakati timu yenye nidhamu itapata sh. 100,000.
Kwa mujibu wa Ester, mashindano hayo yalizinduliwa rasmi juzi na yatafanyika katika jimbo la Bunda mkoani Mara. Hii ni mara ya pili kwa Ester kuandaa mashindano hayo.
Mashindano hayo yalianzishwa mwaka jana, yakizishirikisha timu 15 za soka kutoka katika kata zote za Jimbo la Bunda. Bingwa wa mwaka jana ilikuwa timu ya Bunda Store.
Ester alisema kutokana na hamasa ya mashindano hayo, idadi ya timu mwaka huu imeongezeka. Alisema mashindano ya mwaka huu yatazishirikisha timu 21 za jimbo hilo.
Mbunge huyo alisema mashindano ya mwaka huu yatagharimu sh. milioni 6.5, zikiwemo fedha za zawadi, vifaa vya michezo na matumizi ya uendeshaji wa ligi hiyo kama vile malipo ya waamuzi, huduma ya kwanza na viwanja. Alisema kila timu itapatiwa seti moja ya jezi na mpira.
Wakati huo huo, Ester amesema ataendelea na utaratibu wake wa kugawa vifaa vya michezo kwa kila kata za mkoa wa Mara kwa lengo la kuendeleza michezo.
Ester alisema jana kuwa, safari hii atatoa vifaa hivyo katika wilaya za Musoma Mjini yenye kata 13. Alisema kila kata itapata seti ya jezi na mipira miwili, ambavyo thamani yake ni sh. milioni 4.2.
"Kama, ambavyo nilieleza mwaka jana wakati nazindua mashindano ya Ester Cup, pamoja na mradi wa kugawa vifaa vya michezo, lengo kuu ni kukuza vipaji vya vijana kwenye Jimbo la Bunda na mkoa mzima wa Mara,"alisema.
"Tunatambua kuwa michezo ni ajira, afya, vilevile inakuza umoja naushirikiano, kwa hiyo nataka kuhakikisha naliweka hai soko la ajirakwa vijana, kupitia michezo, kadhalika kudumisha ushirikiano na afya zao," aliongeza.

No comments:

Post a Comment