KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, May 3, 2012

Simba, Yanga sasa kucheza J'pili, Azam kurudiana na Mtibwa leo


UNAWEZA kuiita vita. Na hivyo ndivyo itakavyokuwa wakati Simba na Azam zitakaposhuka dimbani kwenye viwanja viwili tofauti kumenyana na Yanga na Kagera Sugar katika mechi za mwisho za ligi kuu ya Tanzania.
Awali, mechi hizo ilikuwa zichezwe kesho, lakini kufuatia uamuzi wa kamati ya nidhamu na usuluhishi ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), mechi hizo sasa zitachezwa Jumapili badala ya Jumamosi.
Kamati hiyo, inayoongozwa na Kamanda Mstaafu wa Jeshi la Polisi kanda maalumu ya Dar es Salaam, Alfred Tibaigana, ilifikia uamuzi huo kufuatia rufani iliyokatwa na African Lyon.
Katika rufani hiyo, Lyon ilipinga uamuzi wa kamati ya ligi ya TFF kuipa Azam ushindi wa pointi tatu na mabao mawili katika mechi yake dhidi ya Mtibwa Sugar, badala yake ilitaka Mtibwa Sugar ishushwe daraja kwa kususia mechi hiyo.
Pambano kati ya Mtibwa na Azam lilivunjika dakika ya 89 baada ya wachezaji wa Mtibwa Sugar kugomea penalti iliyotolewa kwa Azam na mwamuzi Rashid Msangi kwa madai kuwa, haikuwa halali. Hadi pambano hilo lilipovunjika, timu hizo zilikuwa sare ya bao 1-1.
Kufuatia Mtibwa kugomea penalti hiyo, kamati ya ligi iliamua kuipa Azam ushindi wa pointi tatu na mabao mawili, lakini ilimfungia mwamuzi Msangi kwa madai kuwa, ripoti yake haikueleza iwapo alivunja pambano hilo baada ya kusubiri kwa dakika 15.
Katika uamuzi wake, kamati ya rufani imesema, kamati ya ligi haikuwa sahihi kuiadhibu Mtibwa kwa sababu si kweli kwamba waligomea pambano hilo, bali wachezaji wake walikuwa ndani ya uwanja hadi mwamuzi alipoamua kulivunja.
Kutokana na uamuzi huo wa kamati ya nidhamu, pambano la Mtibwa na Azam sasa litarudiwa leo kwenye uwanja wa Taifa, Dar es Salaam na mechi za mwisho za ligi sasa zitachezwa Jumapili.
Katika mechi hizo, Simba itavaana na watani wao wa jadi Yanga kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam wakati Azam itamenyana na Kagera Sugar kwenye uwanja wa Chamazi.
Mechi hizo mbili zinatarajiwa kuvuta hisia za mashabiki wengi wa soka kwa kuwa ndizo zitakazotoa bingwa wa ligi hiyo msimu huu baada ya mchuano mkali uliodumu kwa miezi kadhaa.
Simba na Azam ndizo pekee zenye nafasi ya kutwaa ubingwa wa ligi hiyo, kutokana na kutofautiana kwa pointi tatu. Lakini Simba ndiyo yenye nafasi kubwa zaidi kwa vile inahitaji sare tu kwa Yanga.
Hadi sasa, Simba inaongoza ligi hiyo kwa kuwa na pointi 59 baada ya kucheza mechi 25 wakati Azam ni ya pili kwa kuwa na pointi 56. Timu hizo mbili zinatofautiana kwa mabao mawili ya kufunga huku kila moja ikiwa imefungwa mabao 12.
Iwapo Simba itaifunga Yanga ama kutoka nayo sare ya aina yoyote, itatawazwa kuwa mabingwa wapya wa ligi hiyo msimu huu. Lakini iwapo Simba itafungwa na Yanga na wakati huo huo Azam kuishinda Kagera Sugar kwa zaidi ya mabao matatu, ubingwa huenda ukatua kwa wanalambalamba.
Habari zaidi zimeeleza kuwa, viongozi wa Simba na Azam wamekuwa wakihaha huku na kule kwa ajili ya kuweka mambo sawa ili kushinda mechi zao za keshokutwa.
Kuna habari kuwa, viongozi wa Azam wamekuwa wakiwasiliana na wachezaji wa Yanga ili kuwashawishi wacheze kufa na kupona na kuibuka na pambano lao dhidi ya Simba.
Mbali na mkakati huo, kuna habari pia Azam imeshajitengenezea mazingira mazuri kwa Kagera Sugar ili iweze kupata ushindi mnono wa mabao.
Habari za uhakika zimeeleza kuwa, Azam imeigharamia Kagera Sugar gharama za malazi na chakula kwenye hoteli moja iliyopo Manzese, Dar es Salaam na pia imewalipa posho wachezaji wake.
Baada ya kushtukia dili hiyo, uongozi wa Simba umeamua kuwachimbia mkwara wachezaji wao na kuwaonya kuwa, yeyote atakayeihujumu katika mechi dhidi ya Yanga, atashughulikiwa.

No comments:

Post a Comment