KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, May 3, 2012

Okwi, Niyonzima watikisa ligi kuu


LIGI kuu ya soka ya Tanzania Bara inatarajiwa kufikia ukingoni Jumamosi wiki hii huku kitendawili cha timu ipi itakayotwaa ubingwa kikiwa bado hakijateguliwa.
Kwa mujibu wa ratiba, timu zote 14 zinazoshiriki katika ligi hiyo msimu huu, zinatarajiwa kushuka dimbani siku hiyo huku mechi kati ya Simba na Yanga na ile kati ya Azam na Kagera Sugar zikitarajiwa kutoa bingwa.
Hadi sasa, Simba inaongoza ligi hiyo kwa kuwa na pointi 59 baada ya kucheza mechi 25, ikifuatiwa na Azam yenye pointi 56 baada ya kucheza idadi hiyo ya mechi. Yanga inashika nafasi ya tatu kwa kuwa na pointi 49.
Kimahesabu, Simba inahitaji sare katika pambano kati yake na Yanga ili iweze kuwa bingwa kwa vile itafikisha pointi 60, ambazo Azam haitaweza kuzifikia. Azam ina uwezo wa kufikisha pointi 59.
Lakini iwapo Simba itafungwa na Yanga na Azam kuibuka na ushindi katika mechi kati yake na Kagera Sugar, kwa mara ya kwanza huenda taji hilo likaenda kwa Wanarambaramba, lakini kwa kutegemea uwiano wa magoli ya kufunga na kufungwa.
Simba hadi sasa imefunga mabao 42 na kufungwa mabao 12 wakati Azam imefunga mabao 40 na kufungwa mabao 12.
Wakati ligi hiyo ikiwa inaelekea ukingoni, tayari timu za Polisi Dodoma na Moro United zimeshateremka daraja baada ya kushika nafasi mbili za mwisho. Timu ya tatu huenda ikawa Villa Squad, African Lyon na Toto African.
Katika ligi ya msimu huu, timu saba kati ya 14 ziliweka maskani yake mjini Dar es Salaam na kucheza mechi zake kwenye Uwanja wa Taifa na Chamazi. Timu hizo ni Simba, Yanga, Azam, African Lyon, Moro United, Villa Squad, JKT Ruvu na Ruvu Shooting. Timu zilizoshiriki kutoka mikoani ni Kagera Sugar, Mtibwa Sugar, Toto African, Polisi Dodoma, JKT Oljoro na Coastal Union.
Timu za Simba, Yanga na Azam, ambazo zinafundishwa na makocha wa kigeni, ndizo pekee zilizofanya vizuri na kushika nafasi tatu za kwanza. Simba inanolewa na Milovan Cirkovic kutoka Serbia kama ilivyo kwa Yanga, inayonolewa na Kostadin Papic. Azam inanolewa na Stewart Hall kutoka Uingereza.
Kadhalika, timu zilizokuwa na wachezaji wengi wa kigeni ndizo zilizofanya vizuri katika ligi hiyo msimu huu. Simba iliwatumia Emmanuel Okwi kutoka Uganda, Felix Sunzu kutoka Zambia na Gervas Kago kutoka Jamhuri ya Afrika ya Kati.
Wachezaji wa kigeni walioichezea Yanga msimu huu ni kipa Yaw Berko na Kenneth Asamoah kutoka Ghana, Davis Mwape kutoka Zambia, Haruna Niyonzima kutoka Rwanda, Hamisi Kiiza kutoka Uganda.
Wageni wengine waliocheza ligi ya msimu huu ni Gideon Ssekamwa kutoka Uganda, Chika Chimaobi Chukwu na Enyinna Darlinton Ariwood walioichezea Toto African na Mosse William Musoke,
Michael Katende na Hannington Kalyeswebula walioichezea Kagera Sugar.
Wengine ni Ibrahim Shikanda kutoka Uganda, Tchetche Hermann na Brice Kipre kutoka Ivory Coast, Awudu Nafiu na Wahab Yahya kutoka Ghana na kipa Obren Curkovic kutoka Serbia walioichezea Azam. Lyon ilimsajili Hood Mayanja kutoka Uganda.
Nyota wengine wa kigeni waliokuja kusakata kabumbu katika ligi hiyo ni Abubakar Shamshudin Hussein, Ben Mwalala na Edwin Mukenya kutoka Kenya, Samuel Tonnyson Temi na Felix Amechi Stanley kutoka Nigeria, ambao waliichezea Coastal Union.
Pamoja na kuwepo kwa wanasoka wengi wa kigeni, ni wachache walioweza kuziletea mafanikio timu zao. Hao ni Okwi, Sunzu na Mafisango wa Simba, Niyonzima na Kiiza wa Yanga na Kipre Tcheche wa Azam.
Okwi, Mafisango na Sunzu walikuwa na mchango mkubwa kwa Simba katika mechi za ligi na michuano ya Kombe la Shirikisho, ambapo waliifungia mabao mengi muhimu.
Ushirikiano wa nyota hao watatu pamoja na wanasoka wazalendo kama vile Haruna Moshi, Mwinyi Kazimoto, Uhuru Selemani na Machaku Salum, umeifanya safu ya ushambuliaji ya timu hiyo iwe tishio na kuzifunga timu ngumu za Kiyovu ya Rwanda, ES Setif ya Algeria na Al-Ahly Shandy ya Sudan katika michuano ya Kombe la Shirikisho.
Kadhalika Niyonzima na Kiiza wamekuwa na msaada mkubwa kwa Yanga kutokana na kuonyesha soka ya kiwango cha juu. Niyonzima ni muunganishaji mzuri wa mipira wakati Kiiza ameifungia Yanga mabao kadhaa muhimu.
Lakini baadhi ya wachezaji wa kigeni kama vile Kago wa Simba, Asamoah na Mwape wa Yanga, ambao walisajiliwa kwa pesa nyingi na klabu hizo, walionekana kuwa mzigo na upo uwezekano mkubwa wa kutemwa msimu ujao.
Asamoah na Mwape wamekuwa wakilalamikiwa kwa muda mrefu na mashabiki wa Yanga kwa kushindwa kuifungia mabao katika mechi muhimu, likiwepo pambano lao la awali la michuano ya klabu bingwa Afrika dhidi ya Zamalek ya Misri. Yanga ilitolewa kwa ushindi wa jumla wa mabao 2-1.
Kipa Berko wa Yanga naye ameshindwa kuonyesha cheche zake, hasa katika mzunguko wa pili wa ligi hiyo kutokana na kuwa majeruhi kwa muda mrefu.
Nyota wa kigeni waliosajiliwa na Toto African, Kagera Sugar na Coastal Union nao wameshindwa kuonyesha cheche zao, badala yake walionekana mzigo mkubwa kwa klabu hizo.
Kipa Curkovic wa Azam pamoja na beki Nafiu na mshambuliaji Wahab wa Azam nao walishindwa kudhihirisha makali yao. Wachezaji hao watatu walitemwa baada ya kumalizika kwa mzunguko wa kwanza wa ligi hiyo.
Beki wa zamani wa Yanga na Simba, Mukenya aliamua kuitosa Coastal Union kabla ya ligi kumalizika, lakini Mwalala na Mnigeria, Felix walikuwa msaada mkubwa kwa timu hiyo na kuinusuru kushuka daraja.

No comments:

Post a Comment