KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Friday, May 11, 2012

CHAMBUA: Moto wa Simba si mchezo


KIPIGO cha mabao 5-0 ilichokipata Yanga kutoka kwa Simba kimepokelewa kwa hisia tofauti na mashabiki wa soka nchini. Wapo wanaowalaumu wachezaji kwa uzembe na wengine wamewatupia lawama viongozi kwa kutoihudumia timu ipasavyo. Mshambuliaji wa zamani wa Yanga na timu ya Taifa, Taifa Stars, Sekilojo Chambua amekielezea kipigo hicho kuwa ni aibu kubwa katika historia ya Yanga katika miaka ya hivi karibuni. Katika makala hii ya ana kwa ana iliyoandikwa na Mwandishi Wetu ATHANAS KAZIGE, mchezaji huyo anaelezea alivyokipokea kipigo hicho.
SWALI: Wiki iliyopita, timu yako ya zamani ya Yanga ilicheza na Simba na kupokea kipigo cha mabao 5-0. Umekipokeaje kipigo hicho na unadhani nini chanzo cha maafa hayo?
JIBU: Kusema ule ukweli, kipigo hicho kimenisikitisha sana kwa sababu haijawahi kutokea kwa miaka mingi Simba kuifunga Yanga idadi hiyo ya mabao. Wakati mimi nachezea Yanga, hatukuwahi kupatwa na aibu hii. Hii ni aibu ya mwaka na siwezi kukisahau kipigo hicho katika maisha yangu.
Naweza kusema kwamba kipigo hicho kimetokana na matatizo mengi, yakiwemo ya uongozi kushindwa kufuata ushauri au programu za kocha wa timu hiyo, ambaye amemaliza mkataba wake hivi karibuni, Kostadin Papic. Aliporejea nchini mwaka jana, Papic alikuja na vitu vingi vizuri, lakini utekelezaji wake ulikuwa sifuri.
Kwa mfano, kuna wakati alitaka timu ikaweke kambi Mwanza kwa ajili ya kujiandaa na ligi kuu, lakini viongozi walikataa. Lengo lake kubwa lilikuwa kutaka kupata nafasi ya kuwaona wachezaji wapya ambao, walisajiliwa na Kocha Sam Timbe kutoka Uganda.
Sababu zingine zilizoifanya Yanga ifanye vibaya katika ligi ni kutokana na kuwepo kwa baadhi ya wachezaji, ambao hawana uwezo wa kuichezea timu hiyo. Kitimu, Simba walikuwa na timu nzuri zaidi msimu huu kuliko Yanga.Tatizo lingine lililokuwepo Yanga ni baadhi ya viongozi wa klabu
kutotaka kusikiliza ushauri. Awali waliwahi kupewa taarifa ya kutomchezesha Nadir Haroub 'Cannavaro' katika mechi yao dhidi ya Coastal Union kule Tanga, lakini walipuuza na kujikuta wakipoteza pointi tatu.
Kwa upande wa Simba, napenda kukiri wazi kwamba, timu yao ipo vizuri na imekamilika kila idara na ilikuwa na uwezo mkubwa wa kushinda mchezo huo kutokana na kuwa fiti kwa asilimia 100 kuliko Yanga, ambayo maandalizi yake kwa ajili ya mchezo huo yalikuwa ya zima moto kuliko wapinzani wetu, ambao msimu huu wapo makini kila kukicha.
SWALI: Kwa maana hiyo, ulichokigundua ni kwamba wapo baadhi ya wachezaji, ambao ni wabovu ndani ya kikosi cha Yanga?
JIBU: Ukweli huo upo dhahiri na ulianza kuonekana tangu Yanga ilipocheza na Zamalek ya Misri katika mechi ya michuano ya klabu bingwa Afrika. Inasikitisha kuona kuwa, wachezaji wanaolipwa mamilioni ya pesa, hasa wale wanaotoka nje, wameshindwa kutoa msaada wowote kwa timu yao na kukosa mabao mengi ya wazi na kusababisha tutolewe mapema. Binafsi naamini wakati umefika kwa viongozi wa benchi la ufundi la Yanga na timu nyingine za soka hapa nchini, kuwa makini na wachezaji, ambao zinataka kuwasajili kwa kupima kwanza uwezo wao kabla ya kufikia uamuzi huo.
Tatizo lingine la Yanga lilikuwa ni wachezaji wake kuonyesha utovu wa nidhamu wa hali ya juu, hasa katika mchezo wao dhidi ya Azam, ambapo walimpiga mwamuzi Israel Nkongo. Katika mechi hiyo, wachezaji wa Yanga hawakuandaliwa kisaikolojia.
Wengi waliingia ndani ya mchezo huo wakiwa na mawazo ya kukosa pesa zao, matokeo yake ni kujazba, ambayo ilichangia timu kufungwa kwa kufanya madhambi, ambayo walikuwa na uwezo wa kuyaepuka badala ya kusababisha penaliti tatu. Nadhani pia kuwa, kocha Fred Felix Minziro alipaswa kubadili mfumo wa uchezaji, hasa katika kipindi cha pili. Yanga haikupaswa kuiga aina ya uchezaji ya Simba. Ilitakiwa kutumia staili tofauti.
Pengine kikubwa zaidi ni kwamba, mgogoro uliopo Yanga baina ya viongozi na wanachama ulichangia kuwaathiri wachezaji. Nadhani ni vyema ufike wakati viongozi wasajili wachezaji wenye mapenzi na klabu badala ya kuokoteza wachezaji holela.
SWALI: Wewe ni mchezaji wa zamani, unafikiri mgogoro kati ya wazee na viongozi ulichangia Yanga kupokea kipigo hicho? Na unadhani ni sahihi kwa viongozi waliopo madarakani kujiuzulu?
JIBU: Nadhani yapo matatizo ndani ya uongozi wa Yanga, lakini bado ninajiuliza kwa nini wachezaji nao waingie kwenye mgogoro huo, wakati wao ni waajiriwa na tayari wameshaisababishia klabu aibu.
Ni kweli yapo matatizo ya wazi na kila mtu anajua kwamba hali ndani ya klabu hiyo kongwe ya soka nchini sio nzuri, hivyo umefika wakati kwa uongozi kujitazama upya ili kuepusha kutokea matatizo makubwa zaidi.
Balaa, ambalo naliona linaweza kutokea ni Yanga kupoteza wachezaji wengi wazuri msimu ujao na pengine amani kutoweka klabuni. Hivyo nawashauri viongozi wa Yanga kulifikiria kwa makini jambo hili.
SWALI: Wewe ni mmoja kati ya wachezaji wa zamani wa Taifa Stars, una maoni gani kuhusu kujitoa kwa mshambuliaji Jonh Bocco wa Azam kwenye timu hiyo baada ya kuzomewa na mashabiki na kisha TFF kumuomba afute mawazo hayo?
JIBU: Binafsi nimekerwa sana na tabia ya baadhi ya mashabiki wa soka kuwazomea wachezaji, hasa wanapofanya vibaya ndani ya kikosi cha Taifa Stars. Tabia hiyo inawavuruga sana wachezaji ndani ya dimba na pengine kuwatoa kabisa kwenye mchezo.
Unajua mchezo wa soka ipo siku unamkubali mchezaji, lakini wakati mwingine unakataa na hata kusababisha kocha amgundue mapema na kumtoa kwenye timu. Lakini napenda kusema kwamba, Bocco bado ni mdogo na ni muhimu kuendelea kuwepo katika kikosi hicho.
Napenda kuchukua fursa hii kuwaonya wadogo zangu (wachezaji wa sasa) kujichunga na kulinda vipaji vyao kwa vile huo ndio mtaji wa kuanzisha biashara katika maisha yao ya siku zijazo.
Wapo wachezaji wazuri, ambao wameanza kupoteza mwelekeo kama ilivyo kwa Jerryson Tegete, ambaye nina imani kwamba inabidi afanye kazi ya ziada ili kurejesha kiwango chake cha zamani. Pamoja na kufungiwa, bado naamini Tegete amepotea kidogo katika soka.
SWALI: Uliwahi kuwa kocha wa timu ya Polisi Dodoma miaka michache iliyopita. Unadhani ni kipi kilichosababisha timu hiyo ifanye vibaya katika ligi msimu huu na kushuka daraja?
JIBU: Kushuka daraja kwa Polisi Dodoma kumetokana na hali mbaya ya kuchumi. Uwezo wa jeshi hilo kuihudumia Polisi ulipungua. Tatizo hili linanikumbusha umuhimu wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) kuangalia uwezekano wa kuzitafutia wadhamini timu zote za ligi kuu badala ya kutegemea udhamini wa Vodacom pekee.
Zamani kulikuwepo na timu kama vile Sigara, ambayo ilikuwa ikimilikiwa na Kampuni ya Sigara Tanzania (TCC) na idadi kubwa ya wachezaji wao walikuwa waajiriwa wa kampuni hiyo.
Pia zilikuwepo timu kama vile Pamba, iliyokuwa inamilikiwa na Mamlaka ya Pamba Tanzania, RTC Kagera, Ushirikia ya Moshi, Ndovu na Pilsner, ambazo zote zilikuwa zikimilikiwa na kampuni mbalimbali na ziliweza kutoa mchango mkubwa katika maendeleo ya soka, lakini zote hizo hazipo hivi sasa.
Yaliyoikuta Polisi ni sawa na yale yaliyozikuta Moro United na Villa Squad, ambazo nazo zimeshuka daraja. Ni matatizo ya pesa. Nadhani wakati umefika kwa timu za aina hii kuanza kusaidiwa kwa udhamini

No comments:

Post a Comment