KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, May 3, 2012

Wachezaji Simba wapigwa mkwara


PG 3
UONGOZI wa klabu ya Simba umewaonya wachezaji wa timu hiyo kuepuka vishawishi vyovyote vinavyoweza kuwafanya wahujumu pambano lao dhidi ya Yanga kwa kucheza chini ya kiwango.
Onyo hilo limetolewa na Mwenyekiti wa Simba, Ismail Aden Rage alipokuwa akizungumza na Burudani jana kuhusu maandalizi ya pambano hilo, litakalochezwa keshokutwa kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Rage alisema pambano hilo ni muhimu kwa Simba kushinda ili iweze kutawazwa kuwa mabingwa wa ligi hiyo msimu huu.
Alisema iwapo Simba itafungwa, upo uwezekano mkubwa kwa taji hilo kunyakuliwa na Azam, iwapo itashinda pambano lake dhidi ya Kagera Sugar kwa idadi kubwa ya mabao.
Mbali na kuwepo kwa hofu ya kuhujumiwa, Rage alisema wamewaelekeza wachezaji wao kucheza kwa tahadhari kubwa kwa hofu ya kuumizwa.
Simba inaongoza ligi hiyo kwa kuwa na pointi 59 baada ya kucheza mechi 25, ikifuatiwa na Azam yenye pointi 56. Iwapo Simba itafungwa na Yanga, Azam inaweza kutwaa ubingwa kwa tofauti ya mabao ya kufunga na kufungwa kati yake na Simba.
“Ni lazima tuwashinde ndugu zetu wa Yanga ili tuwe na uhakika mkubwa wa ubingwa, hivyo tumewatahadharisha wachezaji wetu wasikubali kulaghaiwa kwa njia yoyote kwa sababu wataifedhehesha Simba,”alisema.
Tahadhari hiyo ya Rage imekuja huku kukiwepo na taarifa kwamba, uongozi wa Azam umekuwa ukihaha kuweka mambo sawa ili timu yao iweze kuipiku Simba na kutwaa ubingwa.
Akizungumzia hofu ya wachezaji wao kuumizwa, Rage alisema upo uwezekano mkubwa wa kutokea jambo hilo kwa lengo la kuwaharibia ushiriki wao katika michuano ya Kombe la Shirikisho.
Simba inajiandaa kurudiana na Al-Ahly Shandy ya Sudan wiki mbili zijazo baada ya kushinda pambano lao la awali lililochezwa mwishoni mwa wiki iliyopita kwa mabao 3-0.
Rage alisema wamewaelekeza wachezaji wao kutokaa na mpira kwa muda mrefu na hilo litawasaidia kuepuka kuumizwa na wachezaji wa timu pinzani.
Hata hivyo, Rage alikiri kuwa Yanga ni timu nzuri na wanaiheshimu kutokana na kuundwa na wachezaji wengi nyota, hivyo lolote linaweza kutokea.
“Ninachoweza kusema ni kwamba mchezo utakuwa mzuri kwa vile kila timu itakuwa na malengo ya kulinda heshima yake huku sisi tukitaka ubingwa,”alisema.
Wakati huo huo, Rage amesema kikosi cha Simba kinatarajiwa kuondoka nchini Jumatatu kwenda Sudan kwa ajili ya pambano lao la marudiano dhidi ya Al-Ahly Shandy.
Rage alisema wameamua kwenda Sudan mapema kwa ajili ya kuzoea hali ya hewa ya huko ili isiweze kuwaathiri wachezaji katika pambano hilo.
Alisema Simba itakwenda huko ikiwa na msafara mkubwa wa viongozi na wadau wa timu hiyo kwa lengo la kuhakikisha wanakabiliana vyema na hujuma zozote.

No comments:

Post a Comment