KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Monday, May 7, 2012

Azam yafanya mambo mazito


MKURUGENZI wa Michezo wa Wizara ya Habari Utamaduni na Michezo, Leonard Thadeo amesema
kwamba wachezaji wa Tanzania wanacheza tu soka bila ya kuwa ndoto, jambo ambalo limewafanya
wasifike mbali
Akizungumza katika hafla maalum ya kuwapongeza wachezaji wa Azam FC kwa kushika
nafasi ya pili katika Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara, Thadeo ambaye ni beki wa zamani wa Yanga,
amesema kwamba kutokuwa na ndoto kwa wachezaji wa Tanzania ni tatizo kubwa.
Akizungumza katika
hafla hiyo iliyoandaliwa na Azam FC kwenye hoteli ya JB Belmonte katikati ya Jiji la Dar es Salaam,
Thadeo aliwataka viongozi kuchangia ndoto zao za kuwa timu tishio Tanzania na wachezaji
wao.
Alisema iwapo Azam itakuwa na ndoto ya kufika mbali bila ya wachezaji wao na ndoto hiyo
itakuwa ni sawa na kuchukua sukari na kumwaga baharini.“Lazima wachezaji wa Azam wawe na ndoto
ya kufika mbali, ndipo ndoto za Azam FC zitatimia kwa urahisi,”alisema Thadeo.
Aidha, Thadeo
aliwataka Azam wasiogope mkwara wa Mwenyekiti wa Simba, Alhaj Ismail Aden Rage ambaye mapema
akizungumza kwenye hafla hiyo, alisema Azam wacheze ligi wakigombea nafasi ya pili tu, wakithubutu
kuchukua ubingwa timu yao itakufa.“Katika historia, timu zote zilizochukua ubingwa msimu uliofuata
zilishuka na kufa kabisa kasoro Mtibwa Sugar tu, hivyo nawaomba Azam wacheze ligi wakigombea
nafasi ya pili tu kila mwaka,”alisema Rage.
Akimjibu Rage, Thadeo alisema; “Madai kwamba mkichukua ubingwa timu yenu itakufa, ilikuwa wakati
huo, siyo sasa, hizo timu zilizokufa zilikuwa hazina misingi bora, hazikuwa na academy, hawakuwekeza,
ila Azam iko imara.
Nawapongeza sana na nawaomba endeleeni na juhudi zenu hivyo hivyo.Pamoja na
madai ya Rage, timu zikichukua ubingwa zinakufa, lakini msimu huu mbali na Mtibwa Sugar,
mabingwa mara mbili mfululizo 1999 na 2000, msimu huu wa ligi ukiacha Simba na Yanga, ulishirikisha
bingwa mwingine wa zamani wa ligi hiyo, Coastal Union ya Tanga waliochukua taji hilo mwaka
1988.
Timu zilizowahi kuchukua ubingwa na sasa hazipo kwenye ramani ya soka ni Mseto mwaka 1975
na Tukuyu Stars mwaka 1986, Pan African imeshuka tu daraja na inapigania kurejea Ligi Kuu, ingawa
haina makali ya awali na hiyo ni kama alivyoseam Thadeo hawajawekeza.
Naye Mwenyekiti wa Azam FC, Abubakar Bakhresa alilaani hila na njama ilizokuwa ikifanyiwa timu yake masimu huu ili kuwadhoofisha, ikiwemo kuwapiga marefa wa mechi zao.
Abubakar alisema kwamba pamoja na hila hizo hawakukata tamaa, walipigana hadi dakika ya mwisho na kufanikiwa kupata nafasi ya pili kwenye ligi, ambayo itawawezesha kushiriki Kombe la Shirikisho la Soka Afrika mwakani.“Soka Tanzania sasa inainuka na imekuwa ajira nzuri na wachezaji wengi sasa wanavutiwa kucheza Tanzania. Mchezaji anaona bora kuja kucheza Azam, kuliko kwenda kuhangaika sehemu nyingine.Wachezaji wa Azam wanalipwa vizuri, wanaishi vizuri na wanafurahia maisha na ajira yao nzuri,”alisema.Alisema wakati wanashiriki Ligi Kuu msimu wa kwanza, ndoto zao zilikuwa kucheza ili kubaki kwenye ligi, lakini msimu wao wa nne, wanashika nafasi ya pili na hayo wanayachukulia kama mafanikio makubwa.Alisema mafanikio haya ni mwendelezo wa mafanikio yaliyoanzia kwenye kutwaa Kombe la Mapinduzi mapema mwaka huu visiwani Zanzibar mbele ya vigogo wa soka Tanzania, Simba na Yanga.Abubakar alisema dhamira ya Azam msimu ujao ni kutwaa ubingwa wa Ligi Kuu na kufanya vizuri kwenye Kombe la Shirikisho.
Akimalizia hotuba yake, Abubakar aliwataka wachezaji wa Azam kutumia vizuri kipindi chao cha likizo
kwa kujitunza, ili warejee msimu ujao wakiwa vizuri. Akaagana kabisa na wachezaji ambao
hawatasajiliwa tena timu hiyo, akisema anawatakia maisha mema popote waendako.
HABARI HII KWA HISANI YA BLOGU YA MAMA PIPIRO

No comments:

Post a Comment