KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Friday, May 11, 2012

Wachezaji Yanga wapasua ya moyoni



BAADHI ya wachezaji wa timu ya soka ya Yanga wamekanusha madai kuwa, walicheza chini ya kiwango katika mechi yao dhidi ya Simba kwa lengo la kuwahujumu viongozi.
Wachezaji hao wamesema kipigo cha mabao 5-0 walichokipata kutoka kwa Simba mwishoni mwa wiki iliyopita kilitokana na kuzidiwa kimchezo na pia baadhi yao kukosa ari.
Wakizungumza na Burudani wiki hii kwa masharti ya kutotajwa majina yao, wachezaji hao walisema viongozi wa Yanga wameshindwa kuwalipa madeni wanayodai kwa miezi kadhaa.
Mmoja wa wachezaji hao alisema, uongozi uliahidi kuwalipa madeni hayo mara baada ya mechi kati yao na Simba, lakini hadi sasa wapo kimya.
Akifafanua kuhusu madeni hayo, mchezaji huyo alisema wanadai mishahara ya miezi mitatu na posho za mechi 15.
Alisema wakati timu ilipokwenda kambini Bagamoyo, uongozi uliwapatia sh. 100,000 kila mchezaji kwa ajili ya kuacha nyumbani.
Mchezaji huyo alisema pia kuwa, kabla ya mechi yao dhidi ya Simba, uongozi uliamua kuwalipa wachezaji sh. 300,000 kila mmoja baada ya kugoma kwenda uwanjani.
Nyota mwingine wa timu hiyo alisema, wamesikitishwa na kitendo cha viongozi wao kuwatekeleza baada ya pambano hilo kumalizika.
‘Hali ni mbaya kwa wachezaji na mapenzi ya kuichezea Yanga msimu ujao kwa baadhi yetu yameanza kupungua,’ alisema.
Mchezaji huyo alisema anahisi uongozi huenda ukashindwa kuwalipa madai yao kutokana na kipigo walichokipata kutoka kwa Simba.
Pambano kati ya Simba na Yanga lililochezwa kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, liliingiza sh. milioni 260 na kila timu ilipata mgawo wa sh. milioni 62.

No comments:

Post a Comment