KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Wednesday, February 1, 2012

Victor Costa atoka kifungoni



BEKI mahiri wa klabu ya Simba, Victor Costa amerejeshwa kwenye kikosi cha timu hiyo baada ya uongozi kuamua kumsamehe.
Costa alisimamishwa kuichezea timu hiyo kwa muda usiojulikana kwa makosa ya tuhuma za utovu wa nidhamu.
Beki huyo wa zamani wa timu ya taifa, Taifa Stars, anadaiwa kutenda vitendo hivyo wakati timu hiyo ilipokwenda Zanzibar kushiriki michuano ya Kombe la Mapinduzi.
Ofisa Habari wa Simba, Ezekiel Kamwaga alisema mjini Dar es Salaam jana kuwa, tayari beki huyo ameshaanza mazoezi na wenzake.
Kwa mujibu wa Kamwaga, Costa alisimamishwa kutokana na kukiuka masharti ya kambi wakati timu ilipokuwa Zanzibar.
Kamwaga alisema uamuzi wa kumsamehe Costa ulifikiwa katika kikao cha kamati ya utendaji ya klabu hiyo kilichofanyika hivi karibuni mjini Dar es Salaam.
Licha ya kusamehewa, Kamwaga alisema kamati ya utendaji ya Simba imeamua mchezaji huyo akatwe nusu ya mshahara wake wa mwezi Januari.
Mbali na kukatwa mshahara, kamati hiyo pia imeamua kumpa mchezaji huyo onyo kali na iwapo atarudia tena kosa hilo, mkataba wake utakatishwa.
Beki huyo jana alionekana akiwa na wachezaji wenzake kwenye kambi ya timu hiyo iliyopo hoteli ya Lamada, Ilala, Dar es Salaam.
Simba ipo kambini kwa ajili ya kujiandaa kwa mechi yake ya michuano ya Kombe la Shirikisho dhidi ya Kiyovu ya Rwanda. Mechi ya awali itapigwa Februari 18 mjini Kigali naya marudiano wiki mbili baadaye mjini Dar es Salaam.

No comments:

Post a Comment