KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, February 16, 2012

Mzee Yusuph, Ally J, Thabiti kumalizana ubishi Machi 2

MZEE Yusuph

THABITI Abdul

ALLY J


WASANII nguli wa kupiga kinanda katika muziki wa taarab nchini, Mzee Yusuph, Ally J na Thabiti Abdul wanatarajia kumaliza ubishi kati yao Machi 2 mwaka huu.
Pambano hilo linalosubiriwa kwa hamu kubwa na mashabiki wa muziki huo, limepangwa kufanyika kwenye ukumbi wa Dar Live uliopo Mbagala, Dar es Salaam.
Yusuph ni kiongozi wa kundi la Jahazi, Ally J ni rais wa kundi la Five Stars wakati Thabiti ni mmoja wa wakurugenzi wa kundi la Mashauzi Classic.
Magwiji hao wa kupapasa kinanda, wamekubaliana kupambana kwa lengo la kumaliza ubishi wa muda mrefu juu ya nani mkali kati yao.
Akizungumza mjini Dar es Salaam wiki hii, Ally J alisema pambano hilo limeandaliwa kwa ushirikiano kati ya mameneja wao.
“Kusema ule ukweli, Mzee Yusuph ni mdogo kwangu. Wakati anaanza kupiga kinanda East African Melody na baadaye Zanzibar Stars, mimi ndiye niliyemshauri aachane na fani hiyo, nikamtaka ajikite zaidi katika uimbaji,”alisema Ally J.
Aliongeza kuwa, alimpa ushauri huo Yusuph baada ya kuona uwezo wake katika kupiga kinanda ni mdogo na kipaji chake kipo kwenye uimbaji zaidi.
Ally J alisema amepiga kinanda katika nyimbo nyingi zilizoimbwa na Yusuph kama vile Kipendacho roho, Pwani ya Kiwengwa na nyinginezo, na alikuwa akimpa shavu kwa kumwita jina lake katika nyimbo hizo kutokana na ukali wake.
“Sasa nashangaa anaposema yeye ndiye kanifundisha kupiga kinanda. Asingeweza kunitaja kwenye nyimbo zake kama nisingempigia kinanda vizuri,”alisema.
Ally J alisema inawezekana Yusuph na Thabiti wamemzidi umri, lakini katika kupiga kinanda, hakuna anayemuweza kati yao.
Alisema hata kama ataamshwa saa 10 usiku kutoka usingizini, ana uwezo wa kupiga kinanda katika wimbo wowote.
Majigambo hayo ya Ally J yamekuja siku chache baada ya Yusuph kumponda yeye na Thabiti kwa madai kuwa ni wachanga katika fani ya upigaji wa kinanda katika taarab.
Yusuph alisema pia kuwa, yupo tayari kupambanishwa na wasanii hao wawili wakati wowote na mahali popote kwa vile ana uhakika mkubwa wa kuwatoa nishai.
Juhudi za kumtafuta Thabiti ili kuzungumzia pambano hilo hazikuweza kufanikiwa kwa vile simu yake ilikuwa ikiita bila kupokelewa.

No comments:

Post a Comment