KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Tuesday, March 25, 2014

KAZI IPO KESHO, YANGA NA PRISONS DAR, AZAM NA MGAMBO JKT TANGA



Timu za Azam na Yanga ambazo zinachuana kileleni mwa msimamo wa Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) kuwania ubingwa wa Tanzania Bara zinashuka tena viwanjani kesho (Machi 26 mwaka huu) kuwania pointi tatu.

Azam yenye pointi 47 itakuwa mgeni wa Mgambo Shooting katika mechi itakayochezwa Uwanja wa Mkwakwani jijini Tanga. Mgambo Shooting ipo katika nafasi ya kumi na moja kwenye msimamo wa VPL ikiwa na pointi 19.

Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam utakuwa mwenyeji wa mechi kati ya Yanga na Tanzania Prisons kuanzia saa 10.30 jioni. Yanga ipo nyuma ya Azam kwenye msimamo wa ligi hiyo ikiwa na pointi 47. Hata hivyo, timu hiyo ina mchezo mmoja mkononi.

Tanzania Prisons ambayo ipo chini ya Kocha David Mwamaja hivi sasa ina pointi 22 ikiwa katika nafasi ya kumi. Timu tatu za mwisho katika ligi hiyo itakayomalizika Aprili 19 mwaka huu zitashuka kurudi Ligi Daraja la Kwanza (FDL).

Ligi itaendelea tena Jumamosi (Machi 29 mwaka huu) kwa mechi kati ya Ashanti United na Oljoro JKT itakayofanyika Uwanja wa Azam Complex uliopo Chamazi, Dar es Salaam.

Jumapili (Machi 30 mwaka huu) kutakuwa na mechi kati ya Mbeya City na Tanzania Prisons (Uwanja wa Sokoine), Kagera Sugar na Ruvu Shooting (Uwanja wa Kaitaba), Mtibwa Sugar na Coastal Union (Uwanja wa Manungu), JKT Ruvu na Rhino Rangers (Uwanja wa Azam Complex), Azam na Simba (Uwanja wa Taifa) na Mgambo Shooting na Yanga (Uwanja wa Mkwakwani).

KAMATI YA SHERIA KUPITIA MAREKEBISHO YA KATIBA
Kamati ya Sheria na Hadhi za Wachezaji ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) inatarajia kukutana mwishoni mwa wiki kupitia taarifa ya utekelezaji wa agizo la wanachama kurekebisha katiba zao.

TFF tulitoa agizo kwa wanachama wetu kufanyia marekebisho katiba ikiwemo kuingiza Kamati ya Maadili. Mwisho wa utekelezaji wa agizo hilo ulikuwa Machi 20 mwaka huu.

Hivyo, Kamati ya Sheria na Hadhi za Wachezaji itapokea taarifa ya utekelezaji wa agizo hilo kutoka kwa Sekretarieti, na baadaye kutoa mwongozo wa hatua inayofuata.

No comments:

Post a Comment