KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Friday, June 25, 2010

JABIR: Nimeondoka Simba kutafuta maslahi bora zaidi

JABIR Azizi akipachika bao pekee la Taifa Stars ilipomenyana na Brazil kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam. Katika mechi hiyo, Stars ilichapwa mabao 5-1.

JABIR Azizi (kulia) akiwa na wachezaji wenzake wa timu ya taifa, Taifa Stars. Kutoka kushoto ni Mrisho Ngasa, Mussa Hassan Mgosi na Jerryson Tegete.
WANACHAMA na mashabiki wa klabu ya Simba hivi karibuni walipigwa na butwaa baada ya kupata taarifa kuwa, mshambuliaji Jabir Azizi ameitosa timu hiyo na kujiunga na Azam FC. Katika makala hii iliyoandikwa na Mwandishi Wetu Athanas Kazige, mchezaji huyo anaelezea kuhusu uamuzi wake huo na mipango yake ya baadaye.
SWALI: Kipi kilichokufanya ufikie uamuzi wa kuondoka Simba na kujiunga na Azam FC kwa ajili ya msimu ujao wa ligi?
JIBU: Kwa kweli nimeamua kuondoka Simba kwa lengo la kutafuta maslahi bora zaidi, ambayo nimeahidiwa na viongozi wa Azam. Sikugombana na mtu Simba, isipokuwa viongozi wa Azam walinifuata na kuniomba nijiunge na timu yao kwa ahadi mbalimbali, ambazo kwangu naziona ni nzuri na zitaboresha maisha yangu.
SWALI: Unataka kusema kwamba maslahi uliyokuwa ukiyapata Simba ni madogo ikilinganishwa na yale uliyoahidiwa na viongozi wa Azam au kuna tatizo jingine?
JIBU: Azam wameahidi kunipa maslahi mazuri, ambayo hakuna timu yoyote hapa Tanzania inayoweza kumpa mchezaji wake. Licha ya jambo hilo, mimi sijawahi kugombana na kiongozi yeyote wa Simba, wachezaji wenzangu au wanachama. Nimekaa Simba vizuri na nimeondoka bila ya kukwaruzana na mtu yeyote.Lakini jambo la msingi ni kwamba, nimefanikiwa kutimiza malengo yangu ya kupata maslahi bora na nina imani nitacheza soka kwa nguvu zote.
SWALI: Huoni kama kuondoka kwako Simba kutawaumiza viongozi, wanachama na wachezaji wenzako wa klabu hiyo?
JIBU:Kwa kweli inawabidi wanielewe kwani nimefuata maendeleo kwa vile soka ndio sehemu ya maisha yangu ya kila siku.
SWALI: Ni mafanikio gani uliyoyapata Simba na ambayo unaweza kujivunia nayo? Na ni kipi ulichojifunza ulipokuwa katika klabu hiyo?
JIBU: Nimejifunza mambo mengi sana, ambayo mengine siwezi kuyaelezea kwa vile yapo mazuri na mabaya, lakini kwa ujumla nimenifunza mengi sana kuhusu soka.
SWALI: Jambo gani baya ulilowahi kukumbana nalo ndani ya Simba baada ya kujiunga na klabu hiyo ukitokea Ashanti?
JIBU: Ninachoweza kusema ni kwamba yapo machache mabaya, ambayo nimeyaona, lakini sipendi kuyaanika na kuyapa nafasi kwenye vyombo vya habari. Binafsi ninapasha kuishukuru Simba na wanachama wake na wachezaji wote niliokutana nao pale.
SWALI: Katika kipindi chote ulichoichezea klabu ya Simba, kipi kilikufurahisha zaidi?
JIBU: Nilifurahishwa na kitendo cha kuwepo ushindani wa namba kwenye kikosi cha kwanza miongoni mwa wachezaji. Hiyo ndiyo siri kubwa ya Simba kupata mafanikio msimu uliopita.
SWALI: Mara nyingi ulikuwa unashindwa kuitumikia Simba katika michuano mbalimbali kutokana na kuwa majeruhi kwa muda mrefu. Unazungumza nini kuhusu hilo? JIBU: Ni kweli nilishindwa kucheza mechi nyingi msimu uliopita kutokana na kuwa majeruhi kwa muda mrefu, lakini kila nilipopata nafasi ya kucheza, nilijitahidi kuhakikisha kwamba nafanya kweli kwa kuonyesha uwezo mkubwa ndani ya dimba.
SWALI: Unapenda kuwaahidi nini viongozi, mashabiki na wachezaji wenzako wa Azam msimu ujao? Nini wakitegemee kutoka kwako?
JIBU: Nimekuwa nikijifua kwa nguvu ili kuhakikisha ninakuwa fiti kwa lengo la kukabiliana na changamoto ya kuwania namba kwenye kikosi cha kwanza. Najua ndani ya Azam wapo wachezaji wengi wakali, lakini nitahakikisha ninapambana nao ili lengo langu liweze kutimia.
SWALI: Una maoni gani kuhusu kuondoka kwa Kocha Mkuu wa timu ya Taifa, Taifa Stars, Marcio Maximo, ambaye anamaliza mkataba wa kuinoa timu hiyo mwezi ujao?
JIBU: Kwa kweli mimi binafsi nasikitika sana kwa kuondoka kwake kwa sababu ameweza kuleta maendeleo na mageuzi makubwa katika soka ya Tanzania na pia kufufua mapenzi ya Watanzania kwa timu ya Taifa Stars.
Ni kweli kwamba yapo baadhi ya mapungufu aliyokuwa nayo kama kocha, lakini lazima tukiri kwamba mimi na wachezaji wenzangu wengi wa Taifa Stars tutamkumbuka kocha huyo kwa kipindi kirefu.
Kupitia kwake, nimeweza kujifunza mambo mengi, ikiwa ni pamoja na uchezaji soka makini, nidhamu na bidii ndani na nje ya uwanja. Hivyo ni miongoni mwa vitu, ambavyo Maximo alikuwa akivisisitiza sana kwetu.
SWALI: Kitu gani ulichokipata kutoka kwa kocha huyo na ambacho unajivunia hivi sasa katika maisha yako kisoka?
JIBU: Nimepata vitu vingi. Kama si yeye kuniita katika timu ya Taifa Stars, nisingeweza kupata nafasi ya kucheza na wachezaji bora ulimwenguni. Na kwa bahati nzuri, Mungu alinisaidia nikafunga bao la kufuta machozi kwa nchi yangu katika mechi dhidi ya Brazil.
SWALI: Ulijisikiaje baada ya kufunga bao hilo mara baada ya mchezo huo kumalizika, hasa ikizingatiwa kwamba ulikuwa umetokea benchi kuchukua nafasi ya Abdulrahim Humoud?
JIBU: Mechi hiyo ni kumbukumbu kubwa katika maisha yangu yote. Sikutegemea hata siku moja kukutana na wachezaji nyota kama Kaka, Lucio na wengine na hata kufunga bao katika mechi dhidi ya Brazil.
Lakini bado nina imani kwamba Tanzania tunavyo vipaji vingi vya soka, ambavyo vikipata malezi bora, ipo siku tutacheza hata fainali zijazo za Kombe la Dunia.
SWALI: Je una matarajio gani kuhusu kocha mpya wa Taifa Stars, Jan Borge Poulsen, ambaye ataanza kazi hivi karibuni ya kuinoa timu hiyo?
JIBU: Nina imani kubwa kwamba ujio wake utaendeleza mafanikio tuliyoyapata kutoka kwa Maximo. Tunachohitaji kukifanya ni kumpa ushirikiano wa kutosha ili aweze kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi.
SWALI: Una maoni gani kuhusu mchakato wa kuwapata wachezaji wa Taifa Stars? Au nini kifanyike ili wapatikane wachezaji wenye vipaji?
JIBU: Ninachoweza kushauri ni kwamba, mara atakapokuja kocha huyo na kuanza kazi, apewe nafasi ya kuzunguka mikoa yote nchini kwa lengo la kusaka vipaji. Asichaguliwe wachezaji. Tunayo mashindano mengi hivi sasa, naamini akipata nafasi ya kuyashuhudia, ataweza kupata wachezaji wengi wazuri.
SWALI: Serikali imekuwa inawekeza zaidi katika soka, ni mapungufu gani uliyoweza kuyabaini, ambayo ni kikwazo kwa maendeleo ya mchezo huo nchini?
JIBU: Napenda kumpongeza sana Rais Jakaya Kikwete kwani ameleta changamoto kubwa na kuchangia kwa kiasi kikubwa maendeleo ya soka hapa nchini. Hii ni kwa sababu alikubali kumlipa mshahara Kocha Marcio Maximo na kufanikisha ujio wa timu za Brazil na Ivory Coast, ambazo tulicheza nazo mechi za kirafiki.
Mbali na Rais Kikwete, ninampongeza sana Rais wa awamu ya pili, Benjamin Mkapa kwa kufanikisha ujenzi wa Uwanja wa Taifa wa Dar es Salaam. Uwanja huo umesaidia watu wengi kujitokeza kwenda kushuhudia mechi za kimataifa kwa sababu wana uhakika watakaa kwa raha uwanjani.

No comments:

Post a Comment