KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Sunday, June 6, 2010

KAKA: Nipo tayari kuiongoza Brazil

JOHANNESBURG, Afrika Kusini
MSHAMBULIAJI Ricardo Kaka wa Brazil amesema, hana wasiwasi kuhusu afya yake na kusisitiza kuwa, yupo tayari kuchukua jukumu la kuwa kiongozi wa timu hiyo katika fainali za mwaka huu za Kombe la Dunia.
Kaka atashiriki katika fainali hizo akiwa mchezaji pekee nyota wa Brazil, lakini amekuwa akikabiliwa na maumivu ya mara kwa mara yanayotishia kiwango chake katika fainali hizo.
Hata hivyo, mshambuliaji huyo wa klabu ya Real Madrid ya Hispania anaamini kuwa, atakuwa katika hali nzuri wakati fainali za Kombe la Dunia zitakapoanza.
“Afya yangu inaimarika kila siku. Maumivu hayanisumbui tena. Nimekuwa nikifanya kila kitu kilichopangwa hadi sasa na hadi itakapofika siku ya mechi yetu ya ufunguzi, nitakuwa katika hali nzuri zaidi,”alisema. Maumivu, ambayo yamekuwa yakimkumba Kaka mara kwa mara, yalisababisha ashindwe kuonyesha kiwango chake katika klabu ya Real Madrid msimu huu.
Mshambuliaji huyo wa zamani wa AC Milan ya Italia, alikuwa akikabiliwa na maumivu ya kifundo cha mguu na misuli, ambayo yalisababisha awe benchi kwa siku 45.
Madaktari wa Brazil wamesema, maumivu ya kifundo cha mguu kwa sasa si tatizo tena kwa mchezaji huyo na kwamba maumivu ya paja hayawezi kumfanya kumfanya asiwemo kwenye kikosi cha kwanza katika mechi ya ufunguzi dhidi ya Korea Kaskazini, itakayochezwa Juni 15 mwaka huu.
Kaka amekuwa akifanya mazoezi ya pamoja na wachezaji wenzake wa Brazil tangu timu hiyo ilipowasili Afrika Kusini, Mei 27 mwaka huu, lakini amekuwa akiendelea kupatiwa matibabu wakati wachezaji wenzake wanapokuwa mapumziko.
Mchezaji huyo alicheza kwa dakika 45 siku Brazil ilipoichapa Zimbabwe mabao 3-0 katika mechi ya kirafiki ya kimataifa iliyochezwa Jumatano iliyopita.
Kutokuwemo kwa wachezaji Ronaldinho Gaucho, Ronaldo de Lima, Roberto Carlos na Adriano kunayafanya macho yote ya Wabrazil yawe kwa Kaka.

No comments:

Post a Comment