KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Sunday, June 6, 2010

Kanu aionya Argentina

JOHANNESBURG, Afrika Kusini
MSHAMBULIAJI wa kimataifa wa Nigeria, Nwankwo Kanu ameionya Argentina kwamba isiwadharau na kutarajia kushinda kirahisi mechi kati yao.
Nigeria na Argentina zinatarajiwa kukutana Juni 12 mwaka huu katika mechi ya ufunguzi ya kundi G ya michuano ya fainali za Kombe la Dunia, itakayochezwa mjini Johannesburg.
Nahodha huyo wa Nigeria alisisitiza kuwa, timu yao inao uwezo wa kufanya maajabu dhidi ya miamba hiyo ya dunia kutoka bara la Amerika ya Kusini.
Nchi hizo mbili zimepangwa kundi moja, sanjari na timu za Ugiriki na Korea Kusini.
Nigeria, inayofundishwa na Kocha Lars Lagerback, iliwasili Afrika Kusini mapema wiki hii, ikiwa na kikosi cha wachezaji 23 tayari kwa maandalizi ya mwisho ya fainali hizo.
Mabingwa hao wa zamani wa Afrika, maarufu kwa jina la Super Eagles, wanatarajiwa kucheza mechi ya mwisho ya kujipima nguvu leo dhidi ya Korea Kaskazini.
“Swali sio ni jinsi gani tutapona kwa Argentina, bali ni jinsi gani wao watapona kwetu,”alisema nahodha huyo wa Nigeria kwenye kambi ya timu hiyo iliyopo mjini Durban.
“Hakuna anayeweza kufahamu nini kitatokea siku ya mchezo, lakini kila timu inayo nafasi ya kushinda. Tumejiandaa vyema na tupo tayari kukabiliana nao,”aliongeza mshambuliaji huyo, anayechezea klabu ya Portsmouth ya England.
Nigeria haijashinda mechi zake mbili ilizocheza ikiwa chini ya Kocha Lars, lakini hilo halimpi hofu mshambuliaji huyo, ambaye amejigamba kuwa, wamepania kuonyesha maajabu katika mechi ya ufunguzi.
Kikosi cha Nigeria kinaundwa na makipa: Dele Aiyenugba (Bnei Yehuda), Austin Ejide (Hapoel Petah Tikvah), Vincent Enyeama (Hapoel Tel Aviv).
Mabeki ni Dele Adeleye (Sparta Rotterdam), Rabiu Afolabi (Red Bull Salzburg), Elderson Echiejile (Stade Rennes), Chidi Odiah (CSKA Moscow), Danny Shittu (Bolton Wanderers), Taye Taiwo (Olympique Marseille), Joseph Yobo (Everton).
Viungo ni Yusuf Ayila (Dynamo Kiev), Dickson Etuhu (Fulham), Sani Kaita (Alania Vladikavhaz), Nwankwo Kanu (Portsmouth), Haruna Lukman (Monaco), John Obi Mikel (Chelsea), Kalu Uche (Almeria), John Utaka (Portsmouth).
Washambuliaji ni Yakubu Aiyegbeni (Everton), Obafemi Martins (VfL Wolfsburg), Obinna Nsofor (Malaga), Chinedu Obasi (Hoffenheim), Peter Odemwingie (Lokomotiv Moscow).
Wakati Nigeria ikijigamba kushinda mechi hiyo, Kocha Mkuu wa Argentina, Diego Maradona amesema wiki hii kuwa, bado hana hakika na kikosi chake cha kwanza kitakachocheza fainali za mwaka huu za Kombe la Dunia.
Kauli hiyo ya Maradona ilikuja siku 11 kabla ya Argentina kushuka dimbani kucheza mechi yake ya kwanza ya michuano hiyo dhidi ya Nigeria.
Maradona aliitisha mkutano wake wa kwanza na waandishi wa habari wiki hii mjini Johannesburg na kusema hatatangaza kikosi hicho hadi siku chache kabla ya kucheza na Nigeria.
Kocha huyo alisema kwa sasa bado anawatafutia nafasi kwenye kikosi hicho wachezaji wake wote nyota, wakiwemo Lionel Messi, Carlos Tevez, Gonzalo Higuain na Diego Milito.
“Itakuwa siku chache kabla ya mchezo wetu wa ufunguzi, nitaelewa nini la kufanya,”alisema Maradona. “Nina wachezaji 23 ambao wote uwezo wao ni mkubwa uwanjani.”
Maradona alisema kikosi chake cha sasa ni kizuri kuliko cha mwaka 1986, alichokiongoza kutwaa kombe hilo.
“Mwaka 1986 kulikuwa na wasiwasi mkubwa kuhusu kikosi chetu. Lakini wachezaji tulionao sasa wapo kwenye kiwango cha juu kuliko wa mwaka 86 na wanaelewa mambo vizuri kuliko sisi tulivyokuwa,”alisema.
Kocha huyo alisema pia kuwa, ushindani wa wachezaji wakati wa mazoezi ni mkubwa kwa vile kila mchezaji anafanya kila analoweza ili apewe nafasi kwenye kikosi cha kwanza.
Naye mshambuliaji Carlos Tevez wa Argentina amesema, ameamua kupunguza uzito kwa kula zaidi matunda na mboga za majani kwa lengo la kujiweka.
“Nataka kufurahia fainali hizi za Kombe la Dunia,” alisema mshambuliaji huyo wa klabu ya Manchester City ya England.
Teves alisema amekodisha mtaalamu wa lishe kutokana na tatizo lake la kuongezeka uzito, ambalo hataki litokee wakati wa michuano hiyo.
“Napenda niwe mwanasoka halisi wa kulipwa katika fainali hizi, napaswa kuwajibika,”aliongeza.
“Nataka kucheza katika mechi ya kwanza dhidi ya Nigeria, lakini Lionel Messi na Higuan wapo kwenye kiwango cha juu. Tunao washambuliaji wazuri duniani, lakini tunapaswa kuonyesha hilo katika fainali za Kombe la Dunia,”alisema.

No comments:

Post a Comment