KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, June 10, 2010

Witness awashangaa wanaonenepesha makalio



MSANII machachari wa muziki wa kizazi kipya nchini, Witness Maliwigi ameeleza kukerwa na tabia za baadhi ya wanawake nchini kuongeza makalio yao kwa kutumia dawa za kichina.
Witness alielezea dukuduku lake hilo mwishoni mwa wiki iliyopita alipokuwa akihojiwa katika kipindi cha Friday Nite Live kilichorushwa hewani na kituo cha televisheni cha East Africa.
Alisema haelewi kwa nini wanawake hao wanapenda kuwa na makalio makubwa kinyume na maumbile aliyowaumba nayo Mwenyezi Mungu.
Witness alisema inashangaza kuona kuwa, Wachina wanatengeneza dawa za kunenepesha makalio na maumbile mengine ya mwanadamu, lakini wao hawazitumii.
“Ni vizuri kwa mwanamke kubaki kama ulivyoumbwa na Mungu, uwe mbantu halisi. Kwa mfano, nilivyo mimi hapa si mbaya, huu uafrika halisi, si wa Kichina,” alisema mwanadada huyo aliyejazia vyema kimwili akiwa na makalio ya asili.
“Hii ni orijono prodakti kutoka Mbeya, kilikuwepo kabla ya Wachina kuanza kuuza dawa zao. Hatuhitaji kujibadilisha, kaka zetu ndio wanaopenda haya mambo,”aliongeza.
Witness alisema pia kuwa, siku zote katika maisha yake amekuwa akipendelea kuvaa mavazi anayoyapenda na kusisitiza kuwa, mwonekane wake si rahisi kuwaridhisha watu wengi.
Alisema siku zote anaamini kuwa, ukipendwa na wengi, lazima utakuwa na matatizo, tofauti na wakikuchukia kwa sababu itakusaidia kujua kasoro zako na kujirekebisha.
Msanii huyo alisema si rahisi kwa binadamu kuishi kwa lengo la kuwaridhisha watu fulani na kusisitiza matatizo yapo siku zote, hayawezi kukwepeka.

Banza achengua mashabiki Dar

MWIMBAJI mahiri wa muziki wa dansi nchini, Ramadhani Masanja 'Banza Stone' mwishoni mwa wiki iliyopita aliwateka mamia ya wapenzi wa burudani baada ya kupanda jukwaani na kuimba kwa dakika tatu wimbo wake wa 'Mtu pesa'.
Banza, ambaye amekuwa kimya kwa muda mrefu kutokana na kusumbuliwa na maradhi, aliibuka ghafla kwenye ukumbi wa Vatican City, Sinza, Dar es Salaam, wakati wa uzinduzi wa bendi ya Bwagamoyo Sound International.
Mwimbaji huyo aliyepata umaarufu mkubwa alipokuwa bendi ya Twanga Pepeta kutokana na kipaji chake cha uimbaji, aliingia ukumbini saa sita usiku na kushangiliwa na mamia ya wapenzi waliohudhuria uzinduzi huo.
Baada ya kuingia ukumbini hapo, Mkurugenzi wa bendi ya Bwagamoyo, Mwinjuma Muumini alimtambulisha kwa wapenzi waliokuwa na shauku ya kutaka kumuona akipanda jukwaani na kuimba japo kwa dakika moja.
Banza, ambaye hadi sasa anasifika kutokana na uwezo mkubwa wa kutawala jukwaa na tungo zake nzuri, alilazimika kupanda jukwaani na kuimba beti mbili za wimbo huo, ambao uliteka hisia za wapenzi wa muziki waliohudhuria onyesho hilo.
Kupanda jukwaani kwa Banza kuliwafanya mashabiki hao kumsogelea kwa karibu zaidi huku wengine wakitaka kushikana naye mikono kwa lengo la kumpongeza.
"Huyu jamaa ni noma kweli, hakuna mwimbaji anayeweza kumfikia, tunamuombea kwa Mungu apate nafuu haraka arudi kwenye gemu," alisikika akisema mmoja wa wapenzi hao, aliyekuwepo ukumbini hapo.
Akizungumza wakati wa onyesho hilo, Banza alisema hali yake kwa sasa inaendelea vizuri na kwamba yupo mbioni kuzindua bendi yake itakayoitwa Sony Sound.
"Niko poa kwa sasa, tayari nimetunga wimbo wangu unaofahamika kwa jina la 'Falsafa', ambao umekamilika, ninawaomba mashabiki na wapenzi wangu wajiandae," alisema huku akiwa na tabasamu kubwa.

Mzee Yusuph haninyimi usingizi-Leila

MWIMBAJI mahiri wa kikundi cha taarab cha Jahazi, 'Wana wa Nakshinakshi', Leila Rashid ametoa ya moyoni kwa kutamka kuwa, tabia ya mume wake, Mzee Yusuph kuoa mara kwa mara haimsumbui.
Leila, ambaye aliolewa na Mzee miaka minne iliyopita alisema, ameizoea tabia hiyo ya mumewe na kusisitiza kuwa, hana presha na jambo hilo.
"Sipati tabu hata kidogo ninaposikia Mzee ameoa, kwani najua dini yetu imeruhusu mwanaume kuoa wake hata wanne, sasa nitashaangaa nini?” Alihoji mwimbaji huyo.
Leila, mmoja wa waimbaji waliojaaliwa kuwa na mvuto wa hali ya juu na sauti murua alisema, wanaheshimiana na kupendana na mumewe,tofauti na wanavyofikiria watu wa nje.
Mwanamama huyo, anayetamba na wimbo wa 'Ubinadamu Kazi', alisema mume wake anapotaka kufunga ndoa, anamshirikisha kabla ya kumpa ruksa.
"Tangu aliponiona, mume wangu hafanyi jambo bila kunishirikisha. Anapotaka kufunga ndoa, hunitaarifu na mimi humpa ruksa, najua ni hiari kwa kila muislamu kuoa mke zaidi ya mmoja kama ana uwezo," alisema mwimbaji huyo.
Leila alisema pia kuwa, haoni tatizo kufanyakazi kikundi kimoja na mumewe, ambaye ndiye mkurugenzi wa Jahazi Modern Taarab. Alijiunga na kikundi hicho akitokea East African Melody.
Akizungumzia kibao chake cha kwanza kinachokwenda kwa jina la ‘Maneno ya mkosaji’, Leila alikiri kwamba ndicho kilichompandisha chati na kumfanya we kwenye matawi ya juu.

No comments:

Post a Comment