KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Friday, June 25, 2010

Simba yapata mrithi wa Kaduguda


Malinzi sasa mlezi wa klabuL Rage kuwania ubunge Tabora

KLABU ya Simba imemtangaza Evodius Mtawala kuwa Katibu Mkuu mpya wa klabu hiyo, akichukua nafasi ya Mwina Kaduguda.
Mwenyekiti wa Simba, Ismail Aden Rage aliwaambia waandishi wa habari mjini Dar es Salaam jana kuwa, Mtawala atafanya kazi chini ya uangalizi kwa kipindi cha miezi mitatu akiwa ofisa utawala kabla ya kuendelea na majukumu yake.
Rage alisema lengo la kufanya hivyo ni kupima uwezo wake kikazi na kutambua kama atamudu majukumu yake kwa sababu ni mgeni katika uongozi wa soka.
Alisema kamati ya utendaji iliyokutana wiki hii iliamua kumteua Mtawala kushika wadhifa huo baada ya kuridhishwa na sifa zake kielimu.
Kwa mujibu wa Rage, Mtawala alizaliwa Agosti 1984 na kupata elimu ya msingi na sekondari katika mikoa ya Bukoba na Morogoro. Kwa sasa, Mtawala ana taaluma ya sheria aliyoipata katika Chuo Kikuu cha Cambrige cha Uingereza.
Mbali ya kufanya uteuzi huo, Rage alisema kamati hiyo pia imemuidhinisha Dioniz Malinzi kuwa mlezi wa klabu ya Simba na kuwapitisha wajumbe wanne kuunda bodi ya udhamini.
Aliwataja wajumbe hao kuwa ni Ramesh Patel, Hamis Kilomoni, Abbas Sykes na Abdulwahab. Alisema mhasibu na ofisa habari wa klabu hiyo watatangazwa baadae.
Wakati huo huo, Rage ametangaza nia ya kuwania ubunge katika jimbo la Tabora Mjini kwa tiketi ya Chama cha Mapinduzi (CCM) katika uchaguzi mkuu utakaofanyika Oktoba mwaka huu.
Rage alisema jana kuwa, amemua kuwania nafasi hiyo ili kutekeleza demokrasia ndani ya chama kwa vile uongozi ni suala la kupokezana kama mbio za vijiti.
Rage aliwania nafasi hiyo katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2005 na kushinda kura za maoni, lakini alienguliwa na nafasi yake kuchukuliwa na Siraji Kaboyonga.

No comments:

Post a Comment