KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, June 10, 2010

Kaka: Brazil bado kiwango


JOHANNESBURG, Afrika Kusini
MSHAMBULIAJI wa kimataifa wa Brazil, Ricardo Kaka amekiri kuwa, bado kikosi chao hakijakamilika kwa ajili ya fainali za Kombe la Dunia zinazotarajiwa kuanza kesho nchini Afrika Kusini.
Kaka alisema hayo alipokuwa akihojiwa na waandishi wa habari waliofuatana na timu hiyo nchini kwa ajili ya pambano la kimataifa la kirafiki dhidi ya timu ya Tanzania, Taifa Stars.
Katika pambano hilo lililochezwa mwanzoni mwa wiki hii kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, Brazil iliicharaza Taifa Stars mabao 5-1.
“Bado kuna kitu kinachokosekana. Lakini bado tuna wiki moja kabla ya mechi yetu ya ufunguzi na tutalazimika kufanyakazi ya ziada ili tuwe katika hali nzuri,”alisema Kaka, ambaye alifunga moja kati ya mabao matano ya Brazil katika mechi hiyo.
Japokuwa hakufafanua kuhusu kauli yake hiyo, wadau wengi wa soka nchini Brazil wamelalamikia kitendo cha Kocha Carlos Dunga kumwacha kwenye kikosi hicho kiungo Ronaldinho Gaucho.
Katika mechi hiyo, mshambuliaji Robinho de Souza alifunga mabao mawili, kama ilivyokuwa kwa Ramirez, aliyeingia kipindi cha pili, yakiwa mabao yake ya kwanza kwa timu hiyo. Bao la Taifa Stars lilifungwa na Jabir Azizi.
Ilikuwa mara ya kwanza kwa Brazil kufungwa bao katika mechi tano. Kwa mara ya mwisho, ilifungwa bao Oktoba mwaka jana, ilipofungwa mabao 2-1 na Bolivia katika mechi ya kuwania kufuzu kucheza fainali hizo, iliyopigwa mjini La Paz.
Brazil imepangwa kundi C pamoja na timu za Korea Kaskazini, Ivory Coast na Ureno. Itacheza mechi yake ya kwanza Juni 15 kwa kupambana na Korea Kaskazini.
Katika hatua nyingine, mshambuliaji Ramires wa Brazil mwanzoni mwa wiki hii alimpigia simu mama yake, akimjulisha kuhusu mabao mawili aliyoifungia timu hiyo dhidi ya Taifa Stars.
Ilikuwa mara ya kwanza kwa Ramires, ambaye ni mchezaji wa akiba, kuifungia mabao Brazil katika mechi za kimataifa.
Mara baada ya pambano hilo kumalizika, Ramires alimtwangia simu mama yake mzazi, Judith kumwelezea furaha aliyokuwa nayo kwa kutimiza ndoto yake,
Akihojiwa na mtandao wa Yahoo mara baada ya timu hiyo kurejea Afrika Kusini juzi, Ramires alisema alitaka kusherehekea pamoja mabao hayo na mama yake, anayeishi kwenye kitongoji cha Barra do Pirai kilichopo mjini Rio de Janeiro.
“Pia nilizungumza na kaka zangu. Wote walikuwa wakisherehekea mabao yangu na inawezekana bado wanashangilia,”alisema mchezaji huyo wa klabu ya Benfica ya Ureno.
Ramires (23), ambaye aliingia uwanjani kipindi cha pili kuchukua nafasi ya Felipe Melo alisema, lilikuwa jambo la kufurahisha kwake kwa sababu lengo lake lilikuwa angalau kufunga bao moja, lakini akapata mawili.
Mshambuliaji huyo alisema yupo tayari kucheza nafasi yoyote, lakini hawezi kulalamika kwa kutopata namba kwenye kikosi cha kwanza wakati wa fainali za Kombe la Dunia.
“Kuwemo kwangu kwenye kikosi hiki pekee hunijaza furaha. Hupata zawadi kila wakati ninapoingia uwanjani na kuisaidia timu,”alisema Ramires, ambaye ameichezea Brazil mechi 14 za kimataifa.

No comments:

Post a Comment