KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, June 10, 2010

Wachezaji Stars watoboa siri nzito

WACHEZAJI wa timu ya soka ya Taifa ya Tanzania, Taifa Stars wamelionya Shirikisho la Soka nchini (TFF), kuacha tabia ya kuingilia masuala ya ufundi yanayoihusu timu hiyo.
Walitoa onyo hilo mwishoni mwa wiki iliyopita mara baada ya Taifa Stars kuchapwa mabao 5-1 na Brazil katika mechi ya kirafiki ya kimataifa, iliyochezwa kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Wakizungumza kwa masharti ya kutotajwa majina yao, wachezaji hao walisema tabia hiyo imekuwa ikichangia kuleta madhara makubwa kwenye timu hiyo.
Kauli ya wachezaji hao imekuja siku chache baada ya TFF kumtangaza Jan Borge Poulsen kutoka Denmark kuwa kocha mkuu mpya wa timu hiyo, akichukua nafasi ya Marcio Maximo, anayetarajiwa kumaliza mkataba wake Julai 31 mwaka huu.
“Ukweli ni kwamba kocha wetu wa sasa Maximo amekuwa akitupiwa lawama nyingi kutokana na timu kufanya vibaya katika michuano mbalimbali, lakini kuna baadhi ya mambo alikuwa akikwamishwa na viongozi wa TFF,” alisema mmoja wa wachezaji hao.
Mbali na kukwamishwa kwa Maximo, wachezaji hao walisema kwa kipindi kirefu sasa wamekuwa wakicheleweshewa malipo yao, hali inayochangia kumvunja moyo kocha huyo katika kutekeleza majukumu yake.
Wachezaji hao walisema pia kuwa, Maximo amekuwa akikwamishwa kwenda kuzichunguza timu pinzani kabla ya kupambana na Taifa Stars na hivyo kushindwa kujua mbinu zao.
“Wapo baadhi ya viongozi walikuwa wakijaribu kuingilia mambo ya kiufundi, ikiwemo kutaka baadhi ya wachezaji waitwe ama watemwe kwenye kikosi cha Taifa Stars kwa matakwa yao,” alisema mchezaji mwingine.
Walionya kuwa, iwapo tabia hiyo itaendelea, itakuwa vigumu kwa kocha mpya, Poulsen kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi kama ilivyokuwa kwa Maximo.

No comments:

Post a Comment