KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Friday, June 25, 2010

MAICON DOUGLAS SISENANDO



Sikutarajia kama ningeweza kutembea tena
Aligongwa na gari na kuvunjika miguu yote miwili
JOHANNESBURG, Afrika Kusini
HAKUNA jambo lililomfurahisha beki Maicon Douglas Sisenando wa Brazil kama kuitwa kwenye kikosi cha timu ya taifa ya nchi hiyo, kinachoshiriki katika michuano ya fainali za Kombe la Dunia, inayoendelea nchini Afrika Kusini.
Beki huyo wa kimataifa wa Brazil nusura apoteze miguu yake yote miwili wakati alipokuwa na umri wa miaka 10 baada ya kupatwa na ajali ya kugongwa na gari.
Maicon (26) alikumbana na ajali hiyo wakati alipokuwa akienda kwenye baa ya jirani na nyumbani kwao kwa lengo la kumkabidhi funguo za nyumba baba yake.
Kufuatia ajali hiyo, Maicon hakuweza kutembea kwa miezi kadhaa. Alikuwa akifanya kila kitu kwa msaada wa baba yake, ikiwa ni pamoja na kubebwa na kulazwa kitandani.
Waswahili wanasema Mungu si Athumani. Baada ya takriban mwaka mmoja, Maicon aliweza kupona kabisa, japokuwa alishakuwa na mawazo kwamba asingeweza kutembea tena.
Kuwepo kwake nchini Afrika Kusini ndiko kulikomfanya akumbukie tukio hilo lililotokea miaka kadhaa iliyopita. Bado anakumbuka jinsi alivyokuwa akitembea kwa tabu kutoka kwenye sofa kwenda mahali ilipokuwa televisheni nyumbani kwao Novo Hamburgo.
Miaka minane baada ya kupatwa na ajali hiyo, Maicon aliweza kujumuika tena na vijana wenzake kucheza soka. Ni beki aliyerithi mikoba ya Carlos Alberto, Josimar na Cafu, akiwa ameichezea Brazil mechi 59 za kimataifa na kutwaa ubingwa wa Ulaya akiwa na klabu ya Inter Milan ya Italia.
Maicon ni miongoni mwa wachezaji wa Brazil waliong’ara wakati timu hiyo ilipoichapa Korea Kaskazini mabao 2-1 katika mechi ya ufunguzi ya kundi G. Alifunga moja ya mabao hayo mawili ya Brazil kwa shuti kali la mbali.
“Nalikumbuka vizuri tukio zima la ajali ile,”alisema Maicon alipozungumza na gazeti la News of The World.
“Nilikuwa nikikimbia na kuanguka katikati ya mtaa na nikagongwa na gali. Mama yangu aliona kila kitu na alichanganyikiwa,”aliongeza.
“Baba yangu alipatwa na ghadhabu kwa sababu alishanieleza kwamba sipaswi kukimbia ninapokatiza mtaani. Wazazi wangu walipatwa na wasiwasi mkubwa kuhusu mimi,”alisema Maicon.
“Walishampoteza mtoto wa kiume, aliyeitwa Elton Luis katika ajali ya gari kabla mimi sijazaliwa. Alikuwa na umri wa miaka minane na alikuwa akiendesha baiskeli wakati alipogongwa na gari,”alisema beki huyo wa klabu ya Inter Milan. “Hivyo wazazi wangu hawakuwa tayari kupoteza mtoto mwingine. Nakumbuka nilikuwa nimelala barabarani na baba yangu alikuwa akilia na kuniuliza ‘Upo hai, upo hai?’” Alisema.
“Nilijaribu kumjibu kwa kumwambia ‘Nipo salama, hakuna kibaya kilichotokea’, lakini hakuwa akinisikiliza. Kwa wakati huo, niligundua ni jinsi gani kifo cha kaka yangu kilivyowaumiza mioyo yao na jinsi gani walivyokuwa na uchungu.
“Sikuweza kutembea wala kujiinua baada ya ajali ile. Nilipoteza nguvu za miguu yangu. Baada ya kutibiwa na kurejea nyumbani, nakumbuka nilitumia muda mwingi bila kutembea kwa miguu yangu,”alisema.
“Kwa mfano, sikuweza kutembea kutoka kwenye sofa nilipotaka kutazama TV, hivyo baba yangu alipaswa kunibeba. Na nilipotaka kulala, baba yangu alinibeba kunipeleka kitandani. Sikuweza kutembea kwa miguu yangu na sikuweza kuelewa nini kilitokea kwangu. Nilikuwa na wasiwasi kwamba nisingeweza kutembea tena,”aliongeza.
Baba wa mchezaji huyo, Manoel alikuwa beki wa kati wa klabu ya Novo Hamburgo na wakati alipokuwa kocha wa timu ya Criciuma, aliamua kumchukua Maicon na kuanza kumfundisha soka. Ndiye aliyembadili Maicon kucheza kutoka nafasi ya kiungo kwenda beki. Baadaye, Maicon alijiunga na klabu ya Cruzeiro ya Brazil kabla ya kujiunga na Monaco ya Ufaransa mwaka 2004. Miaka minne baadaye, Maicon alijiunga na Inter Milan ilipokuwa chini ya Kocha Roberto Mancini.
“Nilikuwa mnyonge na mwenye masikitiko makubwa kwa sababu sikutaka kuiangusha familia yangu. Nakumbuka kuna siku nilirudi nyumbani nikilia kwa sababu nilitaka kuchezea klabu ya Gremio,”alisema.
“Wakati huo, baba yangu alikuwa na mawasiliano na klabu ya Criciuma, hivyo nikaenda kule. Miezi michache baadaye, baba aliajiriwa kama kocha. Siku moja, beki wetu wa kulia hakuweza kupatikana. Hivyo baba yangu aliniambia, ‘unapaswa kucheza nafasi hiyo kwa sababu huchezi vizuri nafasi ya kiungo.’
“Alikuwa na mawazo kwamba sikuwa na kasi ya kucheza nafasi ya kiungo na ningeweza kucheza vizuri nikiwa beki wa kulia. Alikuwa sahihi,”alisema Maicon.
Maicon alizaliwa Julai 26, 1981 katika kitongoji cha Cricium kilichopo mji wa Santa Catarina. Aliitwa kwa mara ya kwanza kwenye kikosi cha Brazil mwaka 2004 baada ya kujiunga na klabu ya Monaco.

No comments:

Post a Comment