KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, June 10, 2010

Radio, TV sasa kulipia kazi zote za wasanii

SERIKALI imesema kuanzia sasa vyombo vyote vya habari nchini, hasa vituo vya televisheni na radio, vitalazimika kuwalipa wasanii kila vitakapokuwa vikitumia kazi zao.
Msimamo huo wa serikali ulitolewa mwishoni mwa wiki iliyopita na Ofisa Mtendaji Mkuu wa Chama cha Hakimiliki Tanzania (COSOTA), Yustus Mkinga alipokuwa akizungumza kwenye kipindi cha Kipima Joto, kilichorushwa hewani na kituo cha televisheni cha ITV.
Mkinga alisema tayari wameshafanya mazungumzo na wamiliki wa vyombo hivyo vya habari ili waanze kulipia kazi za wasanii, badala ya utaratibu uliopo sasa, ambapo hakuna malipo yoyote yanayotolewa kwa wasanii.
“Hii ni sheria, haikwepeki. Ni kweli kwamba kwa sasa vyombo hivyo vinatumia kazi za wasanii bila kuwalipa, hili ni kosa kisheria,”alisema.
Akichangia mada hiyo, kiongozi wa bendi ya muziki wa dansi ya The Kilimanjaro, Waziri Ally alisema, si kweli kwamba vyombo vya habari vimekuwa vikiwapromoti wasanii kwa kutumia kazi zao.
“Hiyo si kweli hata kidogo, vinapaswa kutulipa. Wasanii na vyombo vya habari tunafanyakazi kwa kutegemeana,” alisema Waziri, mmoja wa wanamuziki wakongwe nchini, aliyewahi kupigia bendi ya Msondo Ngoma miaka ya 1970.
Waziri alisema wanamuziki wengi wakongwe nchini wamekuwa wakiifanyiakazi serikali tangu miaka ya 1950, lakini hakuna faida yoyote waliyoipata na wengi wao wamekufa wakiwa maskini.
“Umefika wakati sasa tuviambie vyombo hivi vya habari kwamba hapana, wakati wetu umepita hatukunufaika lolote, lakini sasa lazima tuwatengenezee mazingira mazuri vizazi vijavyo,”alisema.
Mmoja wa wasambazaji maarufu wa kazi za wasanii nchini, Ignas Kambarage alisema, Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), haitekelezi majukumu yake ipasavyo kutokana na kuruhusu biashara hiyo ifanyike holela.
Ignas alisema kazi nyingi feki za wasanii zimekuwa zikiingizwa nchini kutoka nchini jirani ya Kenya na China, lakini TRA imekuwa haichukui hatua zozote kuwashughulikia wahusika.
Alihoji iwapo ni kweli CD za filamu na muziki mchanganyiko zinazouzwa nchini, wasanii husika wanafahamu kuwepo kwake na pia iwapo wamelipwa chochote.

No comments:

Post a Comment