KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Friday, June 25, 2010

BARNABAS: Mama haupendi wimbo wa Wrong Number


MSANII machachari wa muziki wa kizazi kipya nchini, Elias Barnabas amekiri kuwa, mama yake mzazi haupendi wimbo wake wa ‘Wrong Number’.
Barnabas alisema mjini Dar es Salaam wiki hii kuwa, wakati mama yake anauchukia wimbo huo, hali ni tofauti kwa baba yake, ambaye anaufagilia ile mbaya.
"Mama hataki kabisa kuusikia huu wimbo, lakini baba hana tatizo lolote," anasema Barnabas, akimaanisha kwamba ni vigumu wimbo huo kusikika redioni nyumbani kwao wakati mama yake akiwepo.
Msanii huyo kutoka kundi la Tanzania House of Talent (THT) alisema, anahisi mama yake haupendi wimbo huo kwa sababu unasimulia kisa cha kweli kuhusu baba yake, ambacho kilimtokea huku mama yake akishuhudia.
Kibao hicho, ambacho kimekuwa kikipendwa na mashabiki wengi wa muziki wa kizazi kipya, kinazungumzia udanganyifi wa kimapenzi kwa wawili waliotengana.
Mashabiki wengi wa muziki huo wamekuwa wakijiuliza, ni vipi Barnabas, kijana mwembamba na mwenye urefu wa wastani, alipata wazo la kutunga kibao hicho?
Msanii huyo ameieleza Burudani kuwa, tukio alilosimulia kwenye kibao hicho ni la kweli na kwamba lilimtokea baba yake mzazi. Alisema alichokifanya ni kulielezea tukio hilo kimafumbo.
Msanii huyo, ambaye ana uwezo mkubwa wa kuimba na kupiga gita alisema, alishuhudia kisa hicho kati ya baba na mama yake, ambacho kilisababishwa na ujumbe mfupi wa simu ya mkononi.
Barnabas anasema ugomvi huo ulitokea siku za hivi karibuni saa nane usiku, nyumbani kwao Kigogo Makuburi, Dar es Salaam na chanzo kilikuwa ujumbe uliokutwa na mama yake kwenye simu ya baba yake, ukielezea masuala ya mapenzi ndipo mama yake akahisi amesalitiwa.
"Siku hiyo nikiwa nimelala, mara baba na mama wakaanza kugombana, nilisikia mama akimtuhumu baba kuwa ametumiwa ujumbe wa mapenzi na alitaka kufahamu ulitokea wapi," anasema Barnabas.
"Mama alipofanya uchunguzi, aligundua kwamba ujumbe huo ulitumwa na mwanamke mmoja anayeishi mtaani kwetu, ambaye alikuwa akimtaka baba kimapenzi,”aliongeza.
"Unajua baba ameokoka na anasali kanisa la Jangwani Makuburi, mama ni mkatoliki. Baba ni mcheshi wakati wote kanisani na nyumbani, jambo hilo huwavutia wasichana, ambao baadhi humtaka kimapenzi," alisema Barnabas.
Barnabas, ambaye aliwahi kutamba na wimbo wa 'Njia Panda' aliomshirikisha Dorine 'Pipi' anasema, ucheshi wa baba yake ulikaribia kumponza kwani mwanamke huyo wa mtaani alianza kumzoea kwa kasi, lakini Mungu alimuepusha kwani baba hakuwa na nia mbaya," alisema Barnabas akimtetea baba yake.
Wanamuziki hao ambao pia walikuwemo katika kinyang'anyiro cha kuwania Tuzo za Muziki za Kili na kutoka mikono mitupu wanasema hilo haliwapi presha kwani wanaamini wakati wao bado haujafika ingawa wanakiri kuwa wapo juu.
Akizungumzia kushindwa kwake kutwaa tuzo ya Kilimanjaro mwaka huu, Baranabas alisema hilo ni jambo la kawaida kwa msanii na ni lazima akubali matokeo.
"Nawapongeza waliochukua tuzo kwani ndio walionekana wanastahili, mimi nasubiri wakati wangu haujafika, ukifika nami naweza kuwa mshindi,”alisema Barnabas.
Alisema kitendo cha kuwemo katika kinyang'anyiro bado ni faraja kubwa kwake na amewataka wasanii walioshinda tuzo mbalimbali, wasibweteke na kujisahau kwani wanaweza kuanguka.
"Ukiingia kwenye kuwania tuzo, ujue wewe ni mkali, naamimi mimi ni mkali, lakini asiyekubali kushindwa si mshindani, ila ninachowaambia waliochukua tuzo hizo, wasilale ili wasianguke halafu ikawa balaa,”alisema.
Barnabas alikiri kuwa, washindi wa mwaka huu walipatikana kihalali kwa sababu mashabiki ndio walioamua baada ya kuwaona wanastahili.
Msanii huyo amekiri kuwa, heshima na uvumilivu ni miongoni mwa vitu vilivyomwezesha kufikia mafanikio aliyonayo sasa kimuziki, kiasi cha kualikwa kurekodi na mwanamuziki Fally Ipupa kutoka Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo. Hivi karibuni, Barnabas alishirikiana na msanii Amini Mwinyimkuu kurekodi albamu ya pamoja, itakayokuwa na nyimbo 14. Wamerekodi baadhi ya nyimbo zilizomo kwenye albamu hiyo kwa kushirikiana na wasanii wa kundi la THT na Nyota Ndogo kutoka Kenya.
Baadhi ya nyimbo zilizomo kwenye albamu hiyo ni 'Njia Panda', 'Muongo', 'Nimelimisi, Mbalamwezi', 'Mama Vanesa', 'Robo Saa', 'Wrong Number' na ‘So so’.
Barnabas alizaliwa miaka 19 iliyopita katika jiji la Dar es Salaam.Wazazi wake ni wenyeji wa mkoa wa Morogoro na kabila lao ni Wapogoro.
Elias, ambaye ni mtoto wa kwanza katika familia yao, alipata bahati ya kumaliza elimu ya msingi na baada ya hapo alijiunga na sekondari ya Mikoji, lakini aliacha shule alipofika kidato cha pili na kuamua kujikita katika fani ya muziki.
Uamuzi wake huo ulipingwa vikali na wazazi wake, ambao walitegemea angejikita zaidi kwenye elimu kwa kuwa waliamini ndio msingi wa maisha.
Licha ya kuonekana kuwa na kipaji cha hali ya juu cha muziki, Barnabas hakuweza kujua apite wapi ili afike kileleni. Ni baada ya kujiunga na kundi la THT mwaka 2007 ndipo Mungu alipoanza kumuonyesha njia.
Jukumu la kwanza la THT lilikuwa kumsaidia kimawazo na kumpa elimu ya muziki, ambayo hivi sasa anamini ndio sababu kubwa ya mafanikio yake.

No comments:

Post a Comment