KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Sunday, June 6, 2010

Kaka na Dada wanaotamba katika taarab


TANGU muziki wa taarab ulipoanza kupigwa hapa nchini, hasa katika visiwa vya Zanzibar, imewahi kutokea kwa baadhi ya vikundi kuwa na wasanii wa familia moja.
Imewahi kutokea kwa baadhi ya vikundi kama vile TOT mama kuimba na mwanawe, kama ilivyokuwa kwa Khadija Kopa na marehemu Omar Kopa.
Pia imetokea kwa mwimbaji Eshe Mashauzi wa Jahazi Modern Taarab kurekodi albamu kwa kushirikiana na mama yake, Rukia Juma, ambaye aliwahi kuimbia kundi la TOT.
Kiongozi wa Jahazi, Mzee Yusuph naye amewahi kuimba kundi moja na dada yake, Khadija Yussuf wakiwa East African Melody na Jahazi kabla ya kutengana na kila mmoja kuamua kuwa kivyakevyake.
Na sasa wapo waimbaji ndugu wawili, Omar Tego na Maua Tego, ambao ni waanzilishi na wamiliki wa kundi la Coast Modern Taarab, ambalo limetokea kuteka hisia za mashabiki wengi wa muziki huo kutokana na nyimbo zake nzuri.
Kundi la Coast lilianzishwa mwaka 1998. Wakati lilipoanzishwa, kundi hilo halikuweza kupata umaarufu kutokana na kutokuwa na waimbaji mahiri na wenye mvuto. Lilipiga muziki wake kwenye kumbi za vichochoroni.
Lakini hivi sasa, kundi hilo limepata umaarufu mkubwa kutokana na vibao vyake vitamu vinavyoimbwa na Maua na kaka yake, Omar. Vibao hivyo vimekuwa vikipigwa mara kwa mara kwenye vituo vya radio na televisheni hapa nchini.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti mjini Dar es Salaam hivi karibuni, ndugu hao walikiri kuwa, muziki huo umewawezesha kupata mafanikio makubwa.
Wakati kundi hilo lilipoanzishwa, Maua alianza kung’ara kwa vibao vyake vya ‘Kayaona mambo’ na ‘Full kujiachia’. Vibao hivyo ndivyo vilivyomsafishia nyota na kumfanya afahamike kwa mashabiki. Hata hivyo, Maua alikihama kikundi hicho siku miezi michache baadaye na kuhamia Zanzibar Stars. Alisema sababu kubwa iliyomfanya ahame ni kutafuta maslahi mazuri zaidi.
Pamoja na kujiunga na kundi hilo, hakufanikiwa kurekodi nalo wimbo wowote. Lakini anakiri kwamba, lilimwezesha kuongeza ujuzi zaidi wa muziki huo kutokana na kuundwa na wanamuziki kadhaa wakongwe.
Alirejea Coast mwaka 2004 akiwa ameiva kiusanii. Alitaja baadhi ya sababu zilizomfanya aondoke Zanzibar Stars kuwa ni pamoja na kukithiri kwa majungu na maslahi madogo.
"Ukubwa wa pua sio wingi wa makamasi. Ni kweli Zanzibar Stars ni kundi kubwa, lakini kwangu halikuwa na maslahi, nilinyimwa nafasi ya kurekodi nyimbo zangu ndio sababu nikaachana nalo,”alisema.
Mara baada ya kurejea Coast, aliibuka na kibao cha ‘Kuvuja kwa pakacha, nafuu ya mchukuzi’, ambacho kililiweka kundi hilo kwenye chati ya juu na kumfanya azidi kufahamika kwa mashabiki.
Kwa sasa, Maua anajiandaa kuachia kibao cha ‘Damu nzito’, ambacho atakiimba kwa kushirikiana na kaka yake, Omar. Pia anatarajia kuibuka na kibao kingine cha ‘Gubu la mawifi’.
Maua alisema yeye na kaka yake, Omar wanapenda na hawajawahi kugombana na ndio sababu wamemudu kufanyakazi pamoja kwa muda mrefu.
Mwanamama huyo mwenye watoto wawili, anavutiwa na waimbaji Mwanahawa Ally na Omar, ambaye pia ni maarufu kwa jina la Special One.
Naye Omar, ambaye ana uwezo wa kuimba, kupiga kinanda, gita la solo na kutunga nyimbo amesema albamu ya ‘I’m Crazy for you’, waliyeirekodi mwanzoni mwa mwaka 2004 ndiyo iliyowapa umaarufu zaidi.
"Kwa kweli baada ya kuachia albamu hiyo, mashabiki wengi walinikubali sana na ndio ilikuwa mwanzo wa jina langu kusikika kwenye masikio ya mashabiki wa muziki huu," anasema.
Hivi karibuni, aliachia albamu yake ya pili inayojulikana kwa jina la ‘Chongeni furniture, ambayo hadi sasa ipo kwenye chati ya juu katika muziki huo.
Mwanamuziki huyo, ambaye ni kipenzi cha mashabiki wengi, anasema amepiga hatua kubwa kupitia muziki huo na anaamini ataendelea ‘kutesa’ kwa kipindi kirefu.
Omar amekiri kuwa, muziki huo umemwezesha kujulikana sana hapa nchini na pia kunufaika kimaisha, tofauti na wakati alipoanza muziki huo miaka ya 1990. Kwa sasa, Omar amejenga nyumba na anamiliki gari la kutembelea.
“Nimetokea mbali sana, awali nilikuwa nikipiga muziki kule Temeke tu, lakini hivi sasa nafahamika karibu mikoa yote Tanzania na nina wapenzi wengi," anasema mwanamuziki huyo mwenye umbo la kuvutia.
Omar anavutiwa zaidi na uimbaji wa Eshe Mashauzi na Khadija Kopa.
0000

No comments:

Post a Comment