KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Friday, June 25, 2010

Ghana yafungwa, lakini yasonga mbele

JOHANNESBURG, Afrika Kusini
GHANA imekuwa timu ya kwanza ya Afrika kufuzu kucheza raundi ya pili ya michuano ya soka ya Kombe la Dunia, licha ya kuchapwa bao 1-0 na Ujerumani katika mechi ya kundi D iliyochezwa juzi kwenye uwanja wa Soccer City mjini hapa.
Bao pekee na la ushindi la Ujerumani lilipatikana katika kipindi cha pili kupitia kwa mshambuliaji Mesut Ozil. Alifunga bao hilo baada ya kupokea pasi kutoka kwa Cacau, ambaye alikuwa mwiba kwa mabeki wa Ghana.
Ushindi huo uliiwezesha Ujerumani kumaliza mechi za kundi hilo ikiwa ya kwanza kwa kuwa na pointi sita baada ya kucheza mechi tatu, ikifuatiwa na Ghana na Australia, ambazo zilipata pointi nne kila moja, lakini zinatofautiana kwa mabao ya kufunga na kufungwa.
Kwa matokeo hayo, Ghana sasa itacheza raundi ya pili kwa kuvaana na Marekani katika mechi itakayochezwa kesho kwenye uwanja wa Rustenburg wakati Ujerumani itavaana na England siku inayofuata mjini Bloemfontein.
Wakati huo huo, Australia juzi iliichapa Serbia mabao 2-1 katika mechi ya mwisho ya kundi D iliyochezwa mjini Nelspruit.
Pamoja na kuibuka na ushindi huo, Australia imeshindwa kusonga mbele kutokana na kuzidiwa na Ghana kwa uwiano wa mabao ya kufunga na kufungwa.
Mabao ya Australia yalifungwa na Tim Cahil na Brett Holman wakati bao la kujifariji la Serbia lilifungwa na Marko Pamtelie.
Ratiba ya mechi zingine za raundi ya pili inaonyesha kuwa, Uruguay itavaana na Korea Kusini kesho mjini Port Elizabeth wakati Argentina itavaana na Mexico keshokutwa mjini Johannesburg.

No comments:

Post a Comment