KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Sunday, June 20, 2010

Khadija: Sina ugomvi na Mzee Yussuf


MWIMBAJI nyota wa muziki wa taarab nchini, Khadija Yussuf ameanika hadharani sababu za kuondoka kwake katika kundi la Jahazi Modern Taarab, linaloongozwa na kaka yake, Mzee Yussuf.
Akizungumza mjini Dar es Salaam mwishoni mwa wiki iliyopita, Khadija alisema alijiengua katika kundi hilo kwa sababu ya maslahi duni si vinginevyo.
Khadija alisema si kweli kwamba aliondoka katika kundi hilo kutokana na kushindwa kuelewana na Mzee, hasa katika mambo ya maslahi.
Mwanamama huyo tipwatipwa alijiengua katika kundi la Jahazi mwaka mwishoni mwa mwaka jana na kujiunga na kundi jipya la Five Stars Modern Taarab.
"Sina ugomvi wowote na Mzee, yeye ni kaka yangu, tunaheshimiana sana na tunaelewana sana, lakini nilihama katika kundi lake kutokana na uchache wa maslahi," alisema.
Mwimbaji huyo anayependwa na mashabiki wengi kutokana na sauti yake maridhawa alisema, yupo tayari kufanya maonyesho na kaka yake iwapo atatakiwa kufanya hivyo.
Alisema tangu ajiunge na kundi la Five Stars, linaloongozwa na Ally Jay, mambo yake yamekuwa mazuri na hana matatizo kama alivyokuwa Jahazi.
"Hivi sasa mambo yangu yanakwenda vizuri, tofauti na nilipokuwa Jahazi, namshuruku Mungu malengo yangu yametimia," alisema.
Khadija aliwahi kutamba kwa vibao vyake vitamu kama vile Mkuki kwa Nguruwe, Zilipendwa, Hayanifiki, Hamchoki kusema, Riziki mwanzo wa chuki.
Alikiri kwamba kibao kilichompandisha chati na kumpatia umaarufu mkubwa ni Mkodombwe, alichokiimba wakati akiwa katika kundi la East African Melody.
Khadija alisema kwa sasa anajipanga upya kabla ya kuibuka na kibao chake kipya kitakachojulikana kwa jina la Ukisema cha nini.
"Ninawaahidi mashabiki wangu wakae mkao wa kula kwani niko mbioni kuachia tungo yangu mpya, ambayo bila shaka itakuwa gumzo hapa nchini," alisema.

Siamini, najihisi nipo ndotoni-AT

SIKU chache baada ya kupokea tuzo ya Kilimanjaro ya wimbo bora wa korabo, msanii Ali Ramadhani, maarufu kwa jina la AT amesema, haamini mafanikio aliyoyapata hadi sasa.
AT, ambaye amekuwa akitamba kwa kibao chake cha Nipigie, alichomshirikisha mkongwe Stara Thomas, amesema hadi sasa bado anajihisi kama yupo ndotoni.
Msanii huyo anayetamba kwenye vituo mbalimbali vya radio na televisheni hapa nchini, alisema mjini Dar es Salaam wiki hii kuwa, kamwe hakuwahi kufikiria katika maisha yake iwapo anaweza kuwapagawisha mashabiki kwa singo yake moja.
"Mafanikio ya singo hiyo yamenifanya niwe na kiburi, najiona ninaweza muziki na ndoto zangu za kuwa mmoja wa watawala katika fani hii zipo mbioni kutimia,"alisema.
"Hivi sasa napata shoo za kufa mtu mpaka zingine nazikataa, yaani naringa, najaa kiburi kutokana na wimbo huo," aliongeza.
Msanii huyo mwenye asili ya Pemba alisema, hatua aliyofikia sasa ni kubwa na kwamba ameanza kuwatetemesha wakali wengine wa muziki huo na wenye majina makubwa.
"Wakati nilipoanza muziki, wengi hawakuamini kama ningefanya vema, sasa wengi wanakubali sikuwa nikifanya utani," alisema na kuongeza kuwa, matunda ya wimbo huo yamemfanya atunze wazazi wake waliopo Zanzibar na vilevile anaishi vema pamoja na mchumba wake (hakutaka kumtaja jina).
"Nimetoka kwenye familia ya kimasikini, hilo silikatai, nalikubali tena kwa moyo mmoja, ninapopata mafanikio, anajiona mwenye amani zaidi," alisema.
"Japokuwa siwasaidii wazazi wangu kwa kila kitu, lakini nawapa kile kidogo ninachokipata kutokana na muziki, hasa wimbo wa Nipigie," alisema AT.
Alisema ingawa yeye ni mtu wa watu, wimbo huo umemfanya atembee mabega juu zaidi. "Kuna maringo ya kujisikia na ya kujiamini, mimi nina maringo ya kujiamini, ndiyo maana ni mtu wa watu, napenda kukaa uswahilini, kujichanganya na watu kwa sababu hao ndiyo wanaonifanya niwe juu,"alisema. AT alisema anaamini amepata tuzo ya muziki ya Kilimanjaro kutokana na ushirikiano alioupata kutoka kwa watu wa mitaani.
Msanii huyo anatarajia kuzindua albamu yake, iliyobeba jina la 'Nipigie' yenye nyimbo 14 hivi karibuni. Albamu hiyo ina vionjo vya sauti za wasanii Nyota Ndogo, Nameless, Ngoni, Shircom, Stara Thomas,Tina, Khadija Kopa na Joti.

No comments:

Post a Comment